Tuesday 17 September 2013

Mkataba kufua umeme mto Kagera watiwa saini


NA ANGELA SEBASTIAN, BUKOBA
MAWAZIRI watatu wa nchi za Afrika Mashariki, wametia saini mikataba miwili inayohusu utekelezaji wa mradi wa kufua umeme wa maji katika mto Kagera.
Mradi huo utajengwa katika eneo la Rusomo mpakani mwa Tanzania na Rwanda.
Mikataba hiyo, ilitowa saini jana mjini hapa na mawaziri wa nchi za Rwanda, Burundi na Tanzania, katika ukumbi wa mikutano wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Magharibi.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kutiwa saini kwa mikataba hiyo kumetengeneza historia mpya, kwani mradi huo ulianzishwa tangu mwaka 1974, lakini ulikwama kutokana na sababu mbalimbalia, ikiwemo ukosefu wa fedha.
Alisema mwaka 2005, mawaziri wa nishati na madini wa nchi hizo walikaa na kujadili jinsi ya kuutekeleza, mazungumzo yakiendelea, huku wakipanga mikakati ya kupata fedha, na kwamba hivi sasa unatarajiwa kuanza rasmi 2015.
Kwa mujibu wa Profesa Muhongo, mradi huo unatarajiwa kukamilika mwaka 2018, na kwamba uko katika awamu mbili ambapo ya kwanza ni kufunga mtambo wa kufua umeme utakaogharimu dola za Marekani milioni 340 zikiwa ni mkopo kutoka Benki ya Dunia.
Alisema awamu ya pili ni ujenzi wa njia za usafirishaji wa umeme kutoka Rusumo hadi Nyakanazi, Rusumo hadi Kigali na Rusumo hadi Burundi, sambamba na kulipa fidia kwa wananchi walioathiriwa na mradi huo.
Akizungumzia kuhusu mgogoro uliokuwepo juu ya mradi huo kati ya nchi hizo, waziri huyo alisema walijadili suala hilo kwa uwazi, ambapo mwanzo ilibainika ulifanywa na Wanyarwanda tu, ambapo uamuzi wa hivi sasa  kila nchi itatoa asilimia 30 ya wafanyakazi katika kutekeleza mradi huo na asilimia 10 watapewa wafanyakazi kutoka nje ya nchi hizo.
Kwa upande wake Naibu Kamishna Msaidizi wa Nishati ya Umeme nchini, Innocent Luoga, alisema mradi huo unaratajiwa kuzalisha megawati 80, ambapo kila nchi itapata megawati 27.
Waziri wa Miundombinu wa Rwanda, Profesa Silas Rwakabamba na Waziri wa Nishati wa Burundi, Manirakiza CĂ­ome, walisema mradi huo umekuja kwa wakati muafaka na itakuwa chachu ya maendeleo ya uchumi wa nchi hizo, kwani utaongeza pato kwa wananchi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru