Friday 24 October 2014

Risasi zarindima Dar



  •  Polisi, genge la mihadarati wapimana ubavu 
  •  ‘Wazungu wa unga’ watano watiwa mbaroni 

NA MWANDISHI WETU
MILIO ya risasi ilirindima kwa dakika kadhaa wakati Polisi wa Kikosi cha Kuzuia Dawa za Kulevya, walipokuwa wakiwakamata watu wanaotuhumiwa kuwa vigogo wa dawa za kulevya.
Kundi kubwa la wananchi lililokuwa likishughudia tukio hilo, lililazimika kutawanyika baada ya polisi kufyatua risasi hewani huku watuhumiwa nao wakijibu kwa kufyatua risasi pia.
Habari za kuaminika zinasema polisi hao walikuwa kwenye operesheni maalumu ya kuwasaka vigogo wa dawa za kulevya, ambapo katika tukio hilo, watuhumiwa watano walitiwa mbaroni.
Watuhumiwa hao wanadaiwa kuwa ni vinara wa kuingiza na kusafirisha dawa za kulevya nchini.
Hata hivyo, kabla ya kusalimu amri watuhumiwa hao walikaidi amri ya polisi kujisalimisha kwa madai ya kutaka kuzungumza kwanza na mtoto wa kigogo mmoja (jina linahifadhiwa).
Watuhumiwa waliotiwa mbaroni ni Muhalani Abdalla (Chonja), ambaye alidaiwa kugoma kutii amri ya polisi hivyo kuzusha tafrani kubwa iliyowafanya watu kujazana kutaka kujua kulikoni.
Mtuhumiwa huyo ambaye ni maarufu jijini Dar es Salaam na anayedaiwa kudaiwa kumiliki idadi kubwa ya nyumba kwenye mtaa mmoja, aliwaongoza wenzake kukaidi amri ya polisi.
Kutokana na kukaidi huko, polisi walitaka kutumia nguvu hivyo kusababisha wananchi kujongea ili kufahamu kinachoendelea, ndipo walipofyatua risasi hewani kwa lengo la kuwatawanya.
Wakati polisi wakifyatua risasi kuwatawanya wananchi, watuhumiwa hao nao walianza kufyatua risasi hewani kujibu mapigo.
Mabishano hayo ya risasi yalidumu kwa dakika kadhaa kisha hali ikatulia kidogo na hatimaye polisi kufanikiwa kuwadhibiti na kuwatia mbaroni.
Mtuhumiwa wa kwanza kutiwa mbaroni alikuwa Chonja, ambapo baada ya wenzake kuona amedhibitiwa na polisi, walijisalimisha na kupandishwa kwenye gari la polisi.
Kamanda wa Polisi wa Kikosi Maalumu cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kukamatwa kwa watuhumiwa hao.
Alisema watuhumiwa hao wanadaiwa kuwa vinara wa kusafisha dawa za kulevya ndani na nje ya nchi na kwamba walikuwa wakisakwa kwa muda mrefu.
Aliwataja watuhumiwa wengine waliokamatwa ni kuwa ni Maric Zuber, Tanaka Adam, Rehani Mursal na Abdu Abdallah, ambao kwa sasa wanashikiliwa na polisi.
Pia alisema watuhumiwa hao walikutwa na dawa za kulevya aina ya heroin kilo saba, ambazo zimechukuliwa kama uthibitisho.
“Oparesheni hii ni endelevu na ninawaasa wananchi watusaidie kwa kutupa taarifa sahihi ili kuwatia mbaroni hawa vinara. Tulikuwa  tunawasaka hawa kwa muda mrefu kutokana na kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya ndani na nje ya nchi.
“Hii ni hatua muhimu na nzuri kwetu kwa kuwa itatusaidia kuubaini mtandao wote ili kuusambaratisha,” alisema Nzowa.
Habari zaidi zinadai kuwa, kuna mtandao mkubwa wa dawa za kulevya nchini ambao unahusisha wafanyabiashara wakubwa katika nchi za Pakistani, China na Falme za Kiarabu, ambapo husafirisha vijana wa Kitanzania kuwekwa rehani.
Vijana wa Kitanzania wanapowekwa rehani, wafanyabiashara hupewa kiasi kikubwa cha dawa za kulevya kwa ajili ya kusambaza na kuuza kisha kurejesha fedha na inapotokea wametoweka, vijana hao hupewa mateso makali.
Habari zaidi zinasema vijana wanaopelekwa kwenye nchi hizo kuwekwa rehani, hupata mgawo wa kati ya asilimia 20 na 25 katika kila mzigo, ambapo mkataba maalumu huriwa saini na wahusika.
Imeelezwa kuwa baadhi ya vigogo wa dawa hizo wamekuwa wakiwatosa vijana hao, hivyo wengine huuawa kwa mateso. Vijana kutoka Tanzania, Afrika Kusini na Nigeria ndio wamekuwa vinara wa kuwekwa rehani nchini Pakistan.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru