Wednesday 14 January 2015

Mfanyabiashara wa samaki auawa kwa risasi



Na Ahmed Makongo, Bunda

MFANYABIASHARA wa samaki ameuawa kwa kupigwa risasi na mwingine kujeruhiwa kwa risasi katika matukio mawili tofauti, yaliyotokea wilayani Bunda mkoani Mara.

Kamanda wa Polisi mkoani Mara, Philpo Kalangi, alithibitisha jana kutokea kwa matukio hayo alipozungumza na Uhuru kwa njia ya simu.

Alisema tukio la kwanza lilitokea juzi saa 3:00 usiku, katika eneo la Nyasura mjini hapa.

Alisema mfanyabiashara huyo, Mkome Marwa (39), akiwa na mke wake, wakati wakirejea nyumbani kwao, alipigwa risasi na mtu au watu wasiofahamika.

Kilangi alisema katika tukio hilo, muuaji hakupora kitu chochote na kwamba ofisi yake imetuma askari katika wilaya ya Bunda  kufanya uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo na kumsaka muuaji.

Kamanda Kalangi alisema Marwa, ambaye ni mkazi wa mtaa wa Nyasura mjini Bunda, alipoteza maisha usiku huo huo wakati akipewa matibabu katika Hospitali ya Rufani ya Bugando jijini Mwanza.

Akisimulia tukio hilo, Kalangi alisema baada ya kupigwa risasi, mfanyabiashara huyo na mkewee walikimbilia katika nyumba ya jirani kuomba msaada, lakini wenye nyumba walifunga geti.

Katika tukio la pili, Kamanda Kalangi, alisema lilitokea eneo la Bunda Day, ambapo  Ndaro Malemi (25), alijeruhiwa kwa risasi  na mtu asiyefahamika wakati akielekea nyumbani kwake.

Akisimulia mkasa huo akiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Bunda, Malemi alisema alimuona mwanaume huyo, aliyekuwa amevaa koti jeusi, ambaye alimvizia njiani na kumwamuru ampatie kila kitu alichokuwa nacho.

Alisema alipoona hivyo, aliamua kukimbia na ndipo alipopigwa  risasi mbili na mtu huyo, ambaye alitokomea kusikojulikana bila kuchukua kitu chochote.


“Aliniweka chini ya ulinzi na kuniambia nitowe kila kitu, mimi niliposikia hivyo na kuona bastola, niliiacha baiskeli yangu, nikatimua mbio, ndipo akanipiga risasi mbili,”alisema.


Akizungumza na Uhuru, daktari wa zamu, Dk. Amosi Manya, alisema  walipokea majeruhi wawili hospitalini hapo, ambapo mmoja alikuwa na hali mbaya na kupelekwa Bugando, lakini alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu.

Dk. Amosi alisema hali ya Maleni inaendelea vizuri baada ya kupatiwa matibabu hospitalini hapo. Maleni alipigwa risasi kifuani.

Kwa mujibu wa Kamanda Kilengi, hakuna aliyekamatwa na polisi kuhusu matukio hayo na bado wanaendelea na uchunguzi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru