Tuesday 23 December 2014

MAONI YA MHARIRI



Taasisi zilizoagizwa kuwachunguza watuhumiwa wa Escrow zitende haki.....!


"HATIMAYE Rais Jakaya Kikwete ameweka hadharani mambo yote kuhusiana na sakata la akaunti ya Tegeta Escrow na kuchukua hatua kwa baadhi ya watendaji.
Akihutubia mkutano wa Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam, Rais Kikwete, alimvua uwaziri Profesa Anna Tibaijuka kutokana na kuhusishwa katika kashfa hiyo na watendaji wengine wakiendelea kuchunguzwa.
Pia, aliagiza hatua kadhaa kuchukuliwa ili kuhakikisha serikali inapata halali yake kwenye mambo ambayo yalizusha utata baada ya sakata hilo kuibuka na kutikisa nchi.
Kabla ya hatua hiyo, sakata la akaunti ya Tegeta Escrow lilifikishwa kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambaye baada ya uchunguzi aliwasilisha ripoti iliyopelekwa bungeni na ambako maazimio kadhaa yalifikiwa.
Ni ukweli usiopingika kuwa katika sakata hilo kuna baadhi ya watu na wanasiasa ambao walitaka kulikuza na kuliongeza chumvi, lengo likiwa kuwakomoa baadhi ya watendaji kwa kutaka wawajibishwe.
Walio katika kundi hilo, walihakikisha wanatumia mbinu na kila aina ikiwemo kuvumisha na kusingizia wengine uongo huku wakijua wanafanya hivyo kwa makosa, lakini walitaka kushinikiza malengo yao kutimia.
Wapo waliotetea na kutaka kuona haki inatendeka na ambao baadhi yao walijitoa kimasomaso kuhakikisha waliotenda makosa wanaadhibiwa badala ya kuwahusisha waliokuwemo na wasiokuwemo kwa mkumbo.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) Jaji Frederick Werema, kwa kutambua kuwa ushauri wake haukueleweka kiasi cha kusababisha mtafaruku kwa busara aliamua kujiuzulu.
Hata hivyo, kutokana na sababu ambazo baadhi ya wahusika wanazijua, walishinikiza kutaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, nao wajiuzulu kwa sababu walisema fedha zile hazikuwa za umma.
Kauli ya Rais Kikwete kuwa fedha zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow hazikuwa za umma bali za Kampuni ya Independent Power Tanzania (IPTL) inamaliza utata ulioibuka kuhusiana na fedha hizo.
Kwa hiyo, suala hilo limewekwa hadharani na kila kitu kimeelezwa, hivyo kilichobaki ni kuacha kuumiza vichwa kwa jambo ambalo limeshapatiwa ufumbuzi kwani mwenye fedha ameshachukua na kinachotakiwa sasa ni kuendelea kuumiza vichwa ili kuona ni kwa namna gani wananchi wengi watanufaika na nishati ya umeme tena kwa bei nafuu.
Pia, utaratibu unaotaka kuota mizizi hivi sasa na hasa kwa wafanyabiashara na wanasiasa kuviziana na ‘kuumizana’ kwa sababu za maslahi binafsi unapaswa kuepukwa ili kuweza kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
Escrow imefungwa na watu wanapaswa kuacha nongwa na badala yake kujikita katika jitihada za kujikwamua kiuchumi badala ya kuendelea kulumbana kwa mambo ambayo hayana faida.
Kwa mamlaka zilizopewa majukumu ya uchunguzi, zinapaswa kukamilisha majukumu yake na kujendelea na taratibu nyingine ili kuona haki ikitendeka."
 

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru