Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Sunday, 10 August 2014

Bunge ladhibiti posho kwa wajumbe watoro

  • JUKATA laonya katiba si mradi binafsi
  • Mrema: Nina akili timamu sio za UKAWA

    NA WAANDISHI WETU
    BUNGE Maalum la Katiba limeweka udhibiti mkali kwa wajumbe wenye tabia ya kusaini posho bila kuhudhuria vikao.
    Wabunge wa bunge maalum la katiba wakiendelea na vikao
    Limesema kuwa lilishitukia mbinu hizo mapema kabla ya kuanza kwa vikao huku baadhi ya wajumbe wa kundi la Katiba ya Wananchi (UKAWA) kuwa ndio wamekuwa na mchezo huo.
    Kutokana na hali hiyo, mfumo wa malipo kwa wajumbe kwa sasa umebadilika ili kuhakikisha wanaolipwa ni wale wanaostahili kwa maana ya kushiriki vikao vya bunge hilo.
    Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Yusuph Khamis Hamad, alisema jana kuwa wajumbe ambao wamejisajili bila kushiriki vikao hawakulipwa na msimamo huo utaendelea.
    Awali, katika vikao vya bunge la katiba vilivyopita, utaratibu wa malipo uliwahusu wote ambao walijiandikisha, ambapo wengine walilipwa bila kuhudhuria baadhi ya vikao.
    Hamad alisema sasa wamedhibiti mchezo huo na kuwa utaratibu wa kuwalipa kwa wiki mbili kwa mkupuo, ambao ulitumika awali umesitishwa badala yake sasa malipo ni kwa wiki moja tu.
    "Tulishaona hiyo hatari mapema na kuamua kuchukua tahadhari na sasa mambo yanakwenda vizuri, wajumbe watakaokuja kujisajili tu kisha kutoweka, hawalipwi posho,” alisema.
    Akizungumzia kuhusu wajumbe wanaoingia kwa kofia ya ubunge wa bunge la Jamhuri, wanaotishiwa kufukuzwa na vyama vyao vinavyounda UKAWA, alisema kisheria mbunge huyo akivuliwa ubunge basi atapoteza sifa ya kuwa mujumbe wa bunge maalum la katiba.
    "Lakini sidhani kama mtu anaweza kuvuliwa ubunge kirahisi, kisa kafukuzwa na chama chake kwa kushiriki vikao vya bunge maalum, natumai hilo suala mahakama inaweza kuamua vizuri tu,na kusimamia haki," aliongeza.
    Alisema wajumbe wote wanaotoka katika UKAWA  ambao wamehudhuria vikao vya bunge hilo, wanaelewa kuhusu maslahi ya nchi kwanza, ni  wazalendo na hawapaswi kukashifiwa.



    Mrema: Nina akili timamu

    Mbunge wa Vunjo, Agustino Mrema amewaeleza wananchi wake kuwa ana akili timamu na hawezi kususia vikao kama wajumbe wa UKAWA.
    Mrema, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TLP, alisema jana kuwa kitendo cha UKAWA kususa bunge hilo ni kuwanyima haki za msingi za uwakilishi kwa wananchi waliowachagua.
    Alisema yeye amechaguliwa na wananchi wa Vunjo kwa ajili ya kuwatetea na kuwasemea matatizo yao, kama anavyofanya katika vikao mbalimbali vya bunge na sio kugomea vikao na kutoka nje.

    “Wapo watu wamekuwa wakinisema kuwa sifai kuwaongoza wananchi wangu, kwa sababu natumiwa na CCM kuwakandamiza ndio maana sijaungana na UKAWA, lakini najua hao wamekosa ya kusema,” alisema Mrema.



    JUKATA laonya katiba si mradi
    Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA) limesema mchakato wa kuandika katiba mpya sio mradi wa mtu binafsi au chama chochote bali ni mradi endelevu wa watanzania wote.
    Mwenyekiti wa Jukwaa hilo Deus Kibamba, aliyasema hayo jana alipokuwa akiongea na waandishi wa habari mjini hapa kuhusiana na mchakato wa katiba.
    Kibamba alisema katiba mpya ya kidemokrasia na yenye viwango vya kimataifa vilivyowekwa na Rais Jakaya kikwete wakati wa kuanzisha kwa mchakato huo ni muhimu kuzingatiwa.
    Alisema hakuna sababu ya kuharakisha kupatikana kwa katiba hiyo ili itumike katika uchaguzi mkuu ujao kwani muda uliobaki ni mfupi kukamilisha katiba.
    Aidha Kibamba alisema bado kunahitajika mazungumzo ya kina ili kufikia maridhiano kati ya UKAWA na bunge katika kuhakikisha katiba inapatikana.
    Alisema hivi sasa pamoja na kuendelea kwa juhudi mbalimbali bado UKAWA wameonyesha kutorejea na hivyo kuvitaka vyama hivyo kujali maslahi ya watanzania.
    Kwa mujibu wa Kibamba hivi sasa kuna mpasuko ndani ya UKAWA kwani, baadhi ya wabunge wanaoamini kuwa Bunge maalumu la katiba halipaswi kuendelea kwa sasa lakini pia wapo ambao wameona ni vyema kuhudhuria.

    "Haikuwa  kwa mashangao kushuhudia wajumbe watatu kutoka kundi la UKAWA wakitinga bungeni na kujiandikisha ili kuendelea na vikao," alisema.
     
     


     
     

Thursday, 7 August 2014

UKAWA yapasuka



  • Wabunge CHADEMA wahudhuria bungeni
  • Hotuba ya Sitta gumzo, zaidi watarajiwa
  • Kamati zaanza kujadili Sura ya 12 ya Rasimu 

NA WAANDISHI WETU, DODOMA
MPASUKO miongoni mwa wajumbe wa kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), umezidi kushika kasi huku baadhi wakiamua kuasi na kuhudhuria vikao vya Bunge Maalumu la Katiba.
Kundi la UKAWA, ambalo limesusia kushiriki vikao vya bunge hilo, linaundwa na wajumbe kutoka vyama vya CHADEMA, NCCR-Mageuzi na CUF, ambapo jitihada za makundi mbalimbali nchini, wakiwemo viongozi wa dini kuwataka kurejea bungeni na kushindana kwa hoja, zimeonekana kugonga mwamba.
WAJUMBE  wa Bunge Maalumu la Katika ambao pia ni Wabunge wa Bunge la Tanzania, Letcia Nyerere (Viti Maalumu -CHADEMA) na Mbunge wa Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani 'Profesa Majimarefu', wakiwasili Viwanja vya Bunge, Dodoma, jana.
Hata hivyo, kuna madai ambayo mpaka sasa yameshindwa kuthibitishwa ama kukanushwa na kundi hilo kuwa, wamekuwa wakiwezeshwa na taasisi fulani za nje kwa lengo la kukwamisha mchakato wa kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.
Imebainika kuwa baadhi ya wajumbe wanaounda kundi hilo, wameanza kujisajili mmoja baada ya mwingine kurejea bungeni, huku usiri mkubwa ukitawala. Hatua hiyo imetokana na tishio lililowekwa na viongozi wa UKAWA kuwa wajumbe watakaosaliti watakiona cha moto.
Miongoni wa wajumbe hao ni Leticia Nyerere (Viti Maalumu-CHADEMA), ambaye jana alifika ofisi za Bunge mjini hapa kujisajili tayari kwa kushiriki vikao hivyo.
Mapema wiki hii, Leticia alikaririwa akisema kuwa, anajali maslahi ya taifa kwanza na kwamba, kushiriki ama kutoshiriki kwenye bunge hilo kutategemea maamuzi ya viongozi wake.
Jana, mbunge huyo alionekana katika viunga vya viwanja vya Bunge akienda kujisajili, lakini aligoma kuzungumza baada ya kutakiwa kueleza sababu za kupuuza agizo la viongozi wake wa UKAWA.
Jitihada za waandishi wa habari kumbana mbunge huyo hazikuzaa matunda, kutokana na muda wote kuzungumza na simu yake ya mkononi huku akitokomea.
Mbali na Leticia, mwingine ambaye anadaiwa kuwa tayari amejisajili kuhudhuria vikao hivyo ni Mbunge wa Maswa Magharibi (CHADEMA), John  Shibuda.
Habari zaidi zimedai kuwa, Shibuda ambaye siku zote amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya taifa, alijisajili juzi asubuhi licha ya kuwa hajaonekana kwenye vikao vinavyoendelea.
Hata hivyo, jitihada za kumpata Shibuda kuzungumzia suala hilo hazikuweza kufanikiwa kwani hata alipotafutwa kupitia simu yake ya kiganjani, ilikuwa ikiita bila kupokewa kabla ya muda mfupi kuzimwa kabisa.

Kamati zaanza kazi
Wajumbe wa bunge hilo jana walianza vikao vya kamati kujadili sura 12 za Rasimu ya Mabadiliko ya Katiba huku hali ya utulivu na maelewano ikitawala.
Baadhi ya wajumbe wamesema hali hiyo inaongeza matumaini kuwa, kazi ya kuandaa Katiba Mpya ya Watanzania iliyo bora itafanyika kwa umakini mkubwa.
Abdalah Bulembo, alisema vikao vimeanza katika hali ya utulivu na Watanzania wategemee Katiba Mpya bora na yenye kujali maslahi ya wanyonge.
Alisema wajumbe wamekuwa na ari kubwa na hotuba ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta aliyoitoa juzi wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, imewaweka sawa kimawazo na kuwafumbua macho walio wengi, hasa kutokana na kauli za uchochezi na ghiliba zinazofanywa na UKAWA.
‘’Katiba bora na yenye kujali maslahi ya wanyonge itapatikana bila wachache wenye malengo na mitizamo binafsi. Hotuba ya Sitta imezidi kuwafumbua watu macho na sasa utulivu na umakini kwa wajumbe wote ni mkubwa,” alisema.
Kuhusu upigaji kura ili kupata theluthi mbili kila upande wa Jamhuri katika maamuzi ya kupitisha Sura za Rasimu, Bulembo alisema hilo si tatizo na kwamba theluthi mbili itapatikana.
Hata hivyo, alisema iwapo hilo litashindikana kutoka kila upande, wajumbe wamekamilisha kazi ya kufanya marekebisho na wananchi ndio watakuwa waamuzi wa mwisho.
‘’Tusitumie unajimu katika upatikanaji wa hizo theluthi mbili, wacha tumalize kazi tuliyotumwa na kama kuna lolote, wananchi wapo wataamua nini cha kufanya wakati wa kupiga kura,” alisema na kuongeza: 
“Watanzania wengi wanatambua nani anafanya nini katika kulinda na kudumisha taifa. Hawa wenzetu wamekuwa na ugomvi na CCM, lakini hii Katiba si ya CCM, ni ya wananchi, hivyo wanapaswa kuweka pembeni tofauti hiyo na kuweka mbele maslahi ya wananchi.’’
Naye Mansour Sharif, alisema upigaji wa kura si suluhisho katika kupata katiba iliyo bora kwani, bado wananchi wana nafasi katika kuangalia utungaji huo.
Alisema siku 60 walizopewa na Rais ni siku muhimu katika kufanya kazi hiyo ya wananchi na kamwe wananchi wasipotoshwe kuwa kazi hiyo haitawezekana.
Stephen Ngonyani, alisema kuna umuhimu wa kuanzisha utaratibu wa kutoa Katiba kwa wananchi mara inapopatikana ili waweze kuisoma na kuelewa kabla ya kufanyiwa marekebisho.
Alisema kwa sasa hali hiyo imejitokeza kwa wananchi walio wengi kutoijua Katiba Katiba ya sasa kikamilifu hivyo kuwa rahisi kupotoshwa.

Pinda atoa agizo kubadili wafugaji

Na Happiness Mtweve, Dodoma
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, ameagiza watendaji kuhakikisha wanabadili fikra za wafugaji ili kuwawezesha kuendesha ufugaji wa kisasa na wa kibiashara, badala ya kuendelea na ule uliozoeleka, ambao hauna tija kubwa katika kukabiliana na umasikini.

Alitoa agizo hilo jana wakati akizindua mashindano ya Maonyesho ya Mifugo, ambayo kitaifa yanafanyika Dodoma katika viwanja vya Maonyesho ya Nanenane vilivyopo Nzuguni mjini hapa.
Pinda alisema ni lazima wizara ibadili fikra za wafugaji kwa maendeleo ya taifa.
Alisema iwapo agizo hilo litasimamiwa kwa umakini kwa kutoa elimu ya ufugaji bora na wa kisasa kwa wafugaji nchini, itawawezesha wafugaji kujikwamua na umasikini na kuchangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa.
Alifafanua kuwa bado hitaji la mifugo bora hapa nchini ni changamoto kubwa licha ya Tanzania kuwa na idadi nyingi ya mifugo, lakini pia mchango wake kwa pato la Taifa ni mdogo.
Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk. Titus  Kamani, alisema kwa sasa wamekamilisha ujenzi wa maabara ya uhamilishaji katika wilaya ya Mpwapwa.
Alisema lengo la kujenga maabara hiyo ni kupata mbegu bora ya mifugo na kuongeza wigo wa huduma hiyo.
“Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunakuomba utusaidie kuongea na taaisis za fedha ili ziwe na sera moja ya fedha na kuwawezesha wafugaji kukopesheka,” alisema.

Ofisa Usalama kizimbani kwa mauaji ya bosi wake


NA FURAHA OMARY
OFISA Usalama wa Taifa, Mohammed Kazembe, anayetuhumiwa kumuua bosi wake, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwa shitaka la mauaji, akiwa hoi hajiwezi.
Kazembe (33), alifikishwa mahakamani hapo jana asubuhi, akiwa amebebwa na watu wawili huku mguu wake wa kushoto ukiwa umefungwa bandeji kutoka kwenye kisigino hadi ugokoni na mkononi alikuwa na njia ya kuwekea dripu ya maji.
Mshitakiwa huyo, mkazi wa Mwananyamala, ambaye hakuwa na uwezo wowote wa kutembea, alifikishwa mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi, Frank Moshi, akiwa na washitakiwa wenzake watatu.
Washitakiwa hao ni mfanyabiashara Lucy Mwafongo (43), mkazi wa Vingunguti, madereva Omary Liwanga au maarufu kwa jina la Sheikh Ponda (26), mkazi wa Mbagala Mwandege na Kelvin Lilai (28), mkazi wa Mbagala Kiburugwa.
Kazembe anayetetewa na Wakili Deiniol Msemwa na wenzake, walisomewa shitaka hilo na Wakili wa Serikali, Celina Kapange.
Celina alidai Aprili 29, mwaka huu, maeneo ya Njia Panda ya Uwanja wa Ndege, wilayani Ilala, mkoani Dar es Salaam, kwa makusudi, walimuua Silvanus Mzeru, ambaye alikuwa Ofisa Usalama wa Taifa.
Washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu lolote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo. Celina alidai upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Hata hivyo, kabla ya kuahirishwa kwa kesi hiyo, Wakili wa Kazembe, Msemwa, alidai mteja wake ni mgonjwa na ana majeraha makubwa, hivyo aliomba upande wa Jamhuri kukamilisha upelelezi mapema ili shauri liende Mahakama Kuu ya Tanzania.
Pia aliomba mshitakiwa kutokana na hali yake, awekewe mazingira mazuri.
Alidai mshitakiwa huyo kabla ya kuingizwa katika chumba cha mahakama, aliwekwa katika korido ambapo kila mtu alikuwa akiruka katika mguu wake.
Hakimu Moshi aliusisitiza upande wa Jamhuri kuhakikisha kuwa mshitakiwa analetwa katika mazingira salama na maradhi yanayomkabili yatashughulikiwa na Jeshi la Magereza.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Agosti 20, mwaka huu.
Baada ya kumaliza kusomewa shitaka hilo, Kazembe, Lilai, dereva Revocatus Rugarabamu (23), mkazi wa Tabata Segerea na Lucy, walipanda tena kizimbani mbele ya Hakimu Frank, wakikabiliwa na kesi nyingine ya mauaji.
Wakili Celina alidai Julai 25, mwaka huu, maeneo ya barabara ya Haile Sellaise, Oysterbay, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, walimuua Frank Silayo.
Washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu lolote na walirudishwa rumande hadi Agosti 20, mwaka huu, kesi itakapotajwa.

Kinana: Tutazidi kulinda maslahi ya wafanyakazi


NA WAANDISHI WETU, DODOMA
KATIBU Mkuu wa CCM, Abrahaman Kinana, amesema Chama kitaendelea kuwa karibu na wafanyakazi katika kuhakikisha maslahi yao yanapatikana. .
Kinana alisema hayo jana alipokuwa akipokea kadi ya uanachama kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Hifadhi, Hotelini, Nyumbani, Huduma za Jamii na Ushauri (CHODAWU) katika ukumbi wa CCM Makao Makuu, mjini hapa.
Alisema mara nyingi wafanyakazi wamekuwa wakijitetea wenyewe lakini kwa sasa kutokana na kupokea kadi hiyo kunakifanya chama kuwa karibu zaidi na wafanyakazi.
Kinana alisema CCM ni chama cha  wakulima na wafanyakazi lakini kimekuwa hakipo karibu sana na wafanyakazi ila kimekuwa karibu na serikali.
“Nadhani Chama kina wajibu wa kuwa karibu na wafanyakazi kuangalia maslahi yao, haki mazingira na kuwasemea,‘’ alisema.
Alisema wakati mwingine Chama kimetakiwa kuwa kipaza sauti cha wafanyakazi na haiwezekani kufanya vyote hivyo bila ya kuwa sehemu ya wafanyakazi.
Kinana alisema Chama pamoja na yeye binafsi atahakikisha anakuwa karibu na CHODAWU na Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) ili kuwa karibu na wafanyakazi  katika maeneo yao kwa kuwa wamekuwa na malalamiko mengi.
Kwa mujibu wa Kinana alisema tangu kuchaguliwa kuwa Katibu mkuu amekuwa  karibu sana na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kwa sababu walimwandikia  barua kumwalika.
Alisema alishawahi kufanya vikao vingi nao na kila akienda  katika ziara zake anakutana na makundi mbalimbali kuzungumza nao wakiwemo walimu.
Alisema ni wajibu wa CCM sasa kama watendaji kuwa wanachama wa chama cha wafanyakazi kupitia sehemu inayowahusu na miezi michache ijayo ataanzisha tawi la chama hicho katika ofisi za CCM Makao Makuu ili wafanyakazi wapate chombo husika cha kupigania haki zao.
“Dhamira yangu ni kumfanya kila mtumishi wa Chama ambaye ataridhia kwa hiyari yake kuwa mwanachama wa CHODAWU na nina hakika watapenda,’’ alisema
Alisema kwa kuanzia ni vyema  kuanzishwa kwa tawi la Chama hicho katika Ofisi Kuu ya CCM na kuhaidi kuwa mmoja wa waanzilishi mpaka watakapopatikana viongozi watakaochaguliwa kwa njia ya  demokrasia.
“Tutaangalia muundo wa matawi yetu maana yametapakaa nchi nzima maana wanachama wana malalamiko yao lakini sina uhakika kama wanamahali pazuri pa kusemea,nimekuwa nikipokea barua watu wanalalamika kupitia chombo fulani sasa mdomo wa wengi ni bora kuliko wa mmoja mmoja,” aliongeza Kinana.
Aidha alisema anajivunia kuwa mwanachama wa CHODAWU kwa kuwa hajawahi kuwa mwanachama wa chama chochote cha wafanyakazi.
“Mimi  kwa kipindi kirefu nimekuwa jeshini, na jeshini kama mnavyojua ni amri tu na hutakiwi kuwa na mwanachama wa chama chochote,” alisema Kinana.
Kinana alitumia nafasi hiyo kumpongeza rais mpya wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi, Gratian Mukoba na kuahidi kutoa ushirikiano.

Kiongozi wa Uamsho kizimbani



  •  Ahoji kushitakiwa Bara badala ya Z’bar

NA MWANDISHI WETU
KIONGOZI wa Jumuia ya Uamsho Zanzibar, Sheikh Farid Hadi Ahmed, anayetuhumiwa kuhifadhi wahusika wa ugaidi, amesomewa mashitaka upya katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
Wakati hatua hiyo ya kisheria ikichuliwa dhidi yake, Sheikh Farid alihoji mahakamani hapo juu ya uhalali wa yeye na wenzake 20 kufikishwa katika mahakama ya Bara, wakati wamekamatwa Zanzibar, ambako ni nchi kamili.
“Tunashangaa kushitakiwa hapa, labda Zanzibar sio nchi, wakati kuna Mahakama Kuu, Mwanasheria Mkuu, Jaji na vitu vingine.
“Sote tumekamatwa Zanzibar, tunashangaa kuletwa hapa, tumeletwa Tanganyika kuonewa. Zanzibar ni nchi, kuna mwanasheria mkuu, mahakama kuu, jaji, tumeletwa huku kama Zanzibar sio nchi,” alilalamika Sheikh Farid.
Mshitakiwa huyo alitoa malalamiko hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Hellen Riwa, muda mfupi kuunganishwa na washitakiwa wenzake na kusomewa mashitaka upya.
Sheikh Farid alisomewa mashitaka upya baada yeye na Jamal Noordin Swalehe, kufutiwa mashitaka yaliyokuwa yanawakabili mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Warialwande Lema.
Mbali na Farid na Jamal, washitakiwa wengine ni Nassoro Abdallah, Hassan Suleimani, Anthari Ahmed, Mohamed Yusuph, Abdallah Hassani au Jibaba, Hussein Ally, Juma Sadala na Said Ally, Hamis Salum, Abubakar Mngodo, Salum Ali, Salum Amour, Alawi Amir, Rashid Nyange au Mapala na Amir Juma na Kassim Nassoro na Salehe Juma.
Awali, upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi Peter Njike, akishirikiana na Wakili wa Serikali Mkuu, Bernard Kongola, na Wakili wa Serikali George Barasa, uliomba kufanya mabadiliko ya hati ya awali ya mashitaka iliyokuwa ikiwakabili washitakiwa 16 kwa kuwaongeza Farid, Jamal, Kassim na Said.
Washitakiwa hao walisomewa mashitaka manne ya kula njama za kutenda kosa, kuingiza watu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutenda vitendo vya kigaidi, kutafuta watu kushiriki kufanya vitendo hivyo na kuhifadhi watu waliotenda vitendo hivyo.
Akiwasomea mashitaka Barasa alidai tarehe tofauti kati ya Januari, 2013 na Juni, 2014 katika maeneo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, washitakiwa wote walikula njama ya kutenda kosa kinyume cha Sheria ya Ugaidi ya mwaka 2002, kwa kutafuta watu wa kushiriki vitendo vya kigaidi.
Katika shitaka la pili, washitakiwa wote wanadaiwa katika kipindi hicho huku wakijua walikubaliana kuwaingiza kuwaingiza Sadick Absaloum na Farah Omary ili washiriki vitendo vya ugaidi.
Sheikh Farid anadaiwa katika kipindi hicho huku akijua aliwaingiza nchini Sadick na Farah ili kushiriki katika vitendo vya kigaidi na kwamba aliwahifadhi watu hao, huku akijua wametenda vitendo hivyo.
Washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu lolote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo. Upande wa Jamhuri ulidai upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Kabla ya  kuahirishwa kwa kesi hiyo, washitakiwa hao walilalamikia kitendo cha kunyimwa kusalimiana na ndugu na jamaa zao wawapo mahabusu gerezani.
Sheikh Farid alidai wengi wao kwa hapa hawana ndugu wa karibu kama vile mke, baba na watoto, hivyo wanaomba jamaa zao wanaokuja kuwasalimia kuruhusiwa.
Hata hivyo, Wakili Njike alidai hadhani kama kuna maelekezo ya namna hiyo ya kuwazuia washitakiwa wasionane na ndugu zao.
Hakimu Hellen alisema kutokana na upande wa Jamhuri kueleza hayo, lakini lazima kuwe na kiwango cha watu wanaozungumza nao.
Washitakiwa hao walirudishwa rumande hadi Agosti 21, mwaka huu, kesi itakapotajwa.
Sheikh Farid na wenzake waliondolewa mahakamani hapo kwenda mahabusu kwa kutumia basi kubwa la Magereza, huku likiwa na msafara wa magari matatu ya polisi na Magereza.

Mndolwa asema hana mpango na ubunge


NA MOHAMMED ISSA
MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Korogwe Vijijini, Dk. Edmund Mndolwa, amesema hafanyi ziara kwa lengo la kutaka ubunge katika jimbo la Korogwe Vijijini.
Amesema anafanya kazi kama mjumbe wa NEC, kutoka wilaya hiyo na kwamba  lengo la ziara zake ni kukijenga Chama.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini  Dar es Salaam, jana, Dk. Mndolwa alisema hajawahi kufanya kampeni yoyote katika ziara zake hizo na kwamba lengo la ziara zake ni kuangalia uhai wa Chama na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Alisema kila anapofanya ziara katika wilaya hiyo anafuatana na sekratieti ya CCM ya wilaya na amekuwa akimwalika Mbunge wa jimbo hilo, Stephen Ngonyani.
“Ziara zangu zina lenga kukijenga Chama chetu, sijawahi kufanya kampeni yoyote katika ziara zangu zote, kila ninapokuwa na ziara namualika mbunge wetu na ninakuwa na viongozi wa Chama wa wilaya,” alisema.
Alisema muda wa kufanya kampeni ndani ya Chama haujafika na viongozi wote waliochaguliwa wapo kihalali na anawaheshimu.
Dk. Mndolwa alisema mwaka 2010, aligombea ubunge katika jimbo hilo na akapata nafasi ya pili na kwamba alishiriki kumfanyia kampeni Ngonyani  bila kinyongo chochote.
“Sina kinyongo wala makundi niliposhindwa kwenye kura za maoni nilishiriki kumfanyia kampeni mbunge wa jimbo letu bila kinyongo,” alisema.
Alisema uhai wa Chama katika wilaya hiyo ni mzuri na hivi sasa wanajiandaa kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika badae mwaka huu.
Dk. Mndolwa alisema kuna kila sababu Chama kushinda katika uchaguzi wa serikali za mita na uchaguzi mkuu.
Alisema katika ziara zake hizo ametembelea kata 20, matawi 89 na kwamba kila tawi amekuwa akitoa ilani ya uchaguzi, kitabu cha maadili pamoja na bendera.

Wednesday, 6 August 2014

Kibano bungeni


  • Posho sasa kudhibitiwa, Kiti chapewa rungu
  • Kanuni kali kuwabana wajumbe watoro
  • Vinara wa zomea zomea, matusi kukiona

WAJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba, wamependekeza kuwepo kwa kanuni kali za kuwadhibiti wanaozomea na kutoa lugha chafu ili kurejesha heshima ya bunge hilo.
Pia wamependekeza wajumbe wote wanaotoroka kuhudhuria vikao vya Bunge, kutolipwa posho za vikao pamoja na kumpa rungu mwenyekiti la kuwaadhibu wote watakaokwenda kinyume.
Mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni hizo, yanatokana na kilio cha wananchi wengi baada ya wajumbe wa bunge hilo kufanya vitendo vya kitoto na visivyoendana na hadhi waliyonayo.

Tangu kuanza kwa bunge hilo Februari, mwaka huu, vitendo vya utovu wa nidhamu, ikiwemo matusi na lugha za kejeli, vimekuwa kitu cha kawaida miongoni mwa wajumbe wa bunge hilo, ambalo limepewa jukumu zito la kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.
Akiwasilisha mapendekezo ya kanuni hizo bungeni jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni, Pandu Ameir Kificho, alisema hatua hiyo imelenga kujenga na kuimarisha nidhamu ndani ya bunge.
Alisema mjumbe aliyepewa adhabu kwa mujibu wa kanuni, hatalipwa posho ya vikao ama kujikimu kwa muda wote atakaokuwa akitumikia adhabu.
Hata hivyo, alisema mjumbe ambaye atakuwa amepewa adhabu na tayari amechukua posho, hatalipwa katika vikao vinavyofuata na utaratibu husika utatumika kufidia fedha hizo.
“Mjumbe aliyepewa adhabu kwa mujibu wa kanuni, hatalipwa posho yoyote ya vikao au ya kujikimu kwa kipindi chote, na iwapo posho ilishatolewa, basi itakatwa kutoka katika malipo mengine ya mjumbe husika,” alisema Kificho.
Aidha alisema mapendekezo hayo yatakapopitishwa, kila mjumbe atapaswa kutia saini karatasi ya mahudhurio iliyoandaliwa na kwamba baadaye itawasilishwa kwa Katibu wa Bunge Maalumu.
Kanuni nyingine inayopendekezwa kufanyiwa marekebisho ni ya 36, ambayo inahusu upigaji wa kura wa ibara za Rasimu ya Katiba.
Kwa mujibu wa Kificho, bila kuathiri masharti ya Sheria na Kanuni, ibara za Sura za Rasimu ya Katiba zilizoandikwa upya, zitapigiwa kura katika muda wa siku saba.
Alisema kanuni zingine zilizopendekezwa kufanyiwa mabadiliko ni pamoja na  namba 14, 15, 32, 32b, 33,35,46,47,54,60,62 na 65.
Alisema kamati yake imeshamaliza kazi ya kujadili kanuni hizo kwa mujibu wa maelekezo ya Mwenyekiti wa Bunge.
Wakichangia mapendekezo hayo, wajumbe waliomba kuwepo kwa kanuni kali zitakazoweza kuwabana wajumbe wa Tume ya Marekebisho ya Katiba kuendelea kujadili na kutoa kauli dhidi ya Bunge.
Zainab Gama, alisema ni vyema kukawa na kanuni maalumu ambazo zitamtaka mjumbe yeyote ambaye hajahudhuria kikao kwa muda wa siku 15, afutwe nafasi hiyo.
Alisema kugomea vikao hivyo vya Bunge ni kutumia vibaya nafasi ya uwakilishi katika bunge hilo maalumu.
Kwa upande wake, Dk Ave-Maria Semakafu, alisema ni muhimu kwa bunge hilo kuhakikisha kuwa masuala ya elimu, afya na usawa wa kijinsia vinapata nafasi katika majadiliano ya rasimu hiyo.
Alisema masuala ya muundo wa uongozi si kipaumbele cha wananchi kwani nia ya wananchi ni kupata katiba inayowagusa wananchi katika mambo yao.
SITTA ALALAMA

Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, amelalamikia baadhi ya vyombo vya habari ambavyo vimekuwa vikitumika kuendesha midahalo inayowadhalilisha wajumbe wa bunge hilo.
Alisema vyombo hivyo vimekuwa vikirusha vipindi hivyo moja kwa moja, ambapo washiriki wamekuwa wakiegemea upande mmoja huku wengine wakitoa lugha chafu zenye kuudhi pamoja na kuwazomea wengine wanaoonekana kuwa upande tofauti.
ìInashangaza kuona watu hawa wanapewa nafasi na ni wale wale kila siku. Hebu Mama Mukangara (Dk. Fenella-Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo), angalia kuna nini huko, lakini pia nadhani serikali inasikia hili,” alisema.
Hivi karibuni, vituo kadhaa vya luninga vimekuwa vikirusha midahalo kuzungumzia Katiba Mpya, ambapo baadhi ya washiriki wamekuwa wakitumia lugha za kuudhi.
Mjumbe Thomas Mgoyi, alisema tume imeshafanya kazi yake na imemaliza, hivyo inabidi waachane na kulishambulia Bunge  Maalumu la Katiba.
"Watuache tufanye kazi za wananchi kuliko kutusema na kututukana maana tutashindwa kuvumilia,î alieleza.
MMANDA AZUNGUMIA RASIMU
Mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Kanuni, Evod Mmanda, alisema bunge hilo lina uwezo wa kujadili Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Jaji Warioba.
Alisema bunge hilo lina nguvu na mamlaka ya kujadili na hata kuboresha kilichowasilishwa kabla ya kwenda kupigiwa kura na wananchi.
Hata hivyo, alisema hakuna kanuni za kuwabana wanaoandaa midahalo nje ya bunge kwa kuwa, kanuni zinahusu kungíata wajumbe ndani ya bunge.
Pia alisema kanuni wala sheria hazisemi iwapo wajumbe wa kundi la 201, wanaweza kuadhibiwa iwapo watatoka ndani ya bunge kwa kuwa sheria haisemi kama wanaweza kufukuzwa.
Mmanda alisema sheria ipo wazi kuwa, iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ilishamaliza kazi yake na waliokuwa wajumbe wake wanazungumza kwa utashi wao.

Kazi imeanza



  • Sitta acharuka, arusha makombora UKAWA
  • Aonya hawana uhalali mbele ya Watanzania
  • Dk.Kigwangalah naye amtolea uvivu Warioba

Na Waandishi Wetu
MWENYEKITI wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, amewapasha wajumbe wa kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kuwa, hawana uhalali wala hadhi kuliko wajumbe wengine.
Amesema jambo la kutofautiana katika kujadili Rasimu ya Katiba Mpya ni la kawaida na kwamba, kamwe vikao vya bunge hilo havitasitishwa kwa sababu ya wachache kususa.
Amesema masuala na matakwa ya kisheria yatazingatiwa katika kufikia hatma ya upatikanaji wa Katiba mpya, ambayo imekuwa ikijenga imani na matumaini mapya kwa Watanzania.
Alitoa msimamo huo jana wakati akifungua kikao cha bunge hilo, ambapo alisema hoja za uzushi na upotoshaji zinazozungumzwa nje, haziwezi kukwamisha shughuli za bunge hilo.
Alisema kutokana na tofauti ya kimtazamo na maoni, ndio sababu umewekwa utaratibu wa kupiga kura pamoja na ule wa maridhiano.
Sitta alisema utaratibu mpya ulioanza kujengwa na baadhi ya viongozi kususia mijadala halali ya Bunge na kwenda nje kuelezea hoja za upande mmoja, hauna nafasi katika jamii inayojali amani na upendo.
‘’Kuna mengi yanazungumzwa kujadili mchakato wa Katiba Mpya nje ya bunge hili, ni muhimu wahusika wapunguze jazba, chuki na upotoshaji na Bunge Maalumu lisaidiwe kwa mawazo chanya ili limalize kazi yake,’’ alisema Sitta.
Kuhusu tuhuma zinazotolewa kuwa bunge hilo linajadili mambo nje ya Rasimu ya Katiba, Sitta alisema hazina ukweli wowote na kuwa msingi wa majadiliano hayo ni kuipitia Rasimu hiyo.
Hata hivyo, alisema kiutaratibu wajumbe wana haki ya kurekebisha baadhi ya maeneo iwapo wataona inafaa na kuwa si kosa kufanya hivyo.
Sitta alisema kwa kaida Rasimu ni andiko ambalo halijajitosheleza bila kupata ithibati ya taasisi ya juu zaidi, likiwemo Bunge Maalumu la Katiba.
“Anayekabidhiwa Rasimu anayo haki na mamlaka ya kuirekebisha, vinginevyo hakuna sababu ya kuijadili,’’ alisema Sitta.
Rasimu ni mali ya Bunge
Mjumbe wa bunge hilo, Hamad Rashid Mohamed, alisema jambo lolote likishakabidhiwa kwa Bunge, ni mali ya Bunge, hivyo wanaweza kulifanyia lolote katika kuliboresha.
Hamad, ambaye ni Mbunge wa Wawi (CUF), alisema kwa mujibu wa taratibu zote duniani, jambo hilo linakuwa ni mali ya Bunge, ambalo pia ni chombo kinachowawakilisha wananchi, kwa hiyo hakuna kosa lolote kufanya baadhi ya marekebisho au maboresho ya rasimu .
Kigwangala na Jaji Warioba
Dk. Hamis Kigwangalah, akichangia bungeni jana, alimtaka aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, kuacha kuingilia mchakato huo.
Alisema kazi ya Jaji Warioba na Tume yake ilishamalizika na kwamba, kilichobaki kwa sasa ni nafasi ya wajumbe wa bunge hilo kutimiza wajibu wa kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.
Alisema amekuwa akishangazwa na baadhi ya wajumbe wa Tume hiyo kuendelea kutetea maoni yao huku wakitoa kauli zenye kuudhi dhidi ya wajumbe wa bunge hilo.
“Inashangaza, wakati wao walipokuwa wakifanya kazi sisi tulinyamaza, lakini sasa tunafanya kazi wao wanaingilia, kila siku kazi ni kuliponda Bunge, ni vyema Mwenyekiti ukae chini na wazee wenzako na kuzungumza nao ili waache bunge lifanye kazi. Kila kukicha kwenye midahalo kutetea maoni yao na kuzungumza maneno ya kejeli, hii si sawa kabisa, kaa na wazee wenzako mzungumze,’’ alisema.
Aidha, aliiomba Kamati ya Kanuni kuweka kanuni itakayomshauri Rais Jakaya Kikwete kufuta uteuzi wa wajumbe watakaosusa kuhudhuria vikao vya Bunge hilo.
Watoto wa vigogo kusoma nje
Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), umesema kuna mambo mengi ya kujadiliwa katika mchakato wa Katiba Mpya kuhusiana na elimu.
Pia umependekeza kuwepo kwa sheria katika Katiba Mpya ijayo, inayokataza watoto wa vigogo kwenda kusoma nje ya nchi kama chachu ya kuboresha elimu nchini.
Mtandao huo umesema kushuka kwa elimu nchini ni matokeo ya mambo mengi, ikiwemo watoto wa wakubwa kupelekwa kusoma nje huku wale wa masikini wakiendelea kupambana na changamoto zilizopo kwenye elimu nchini.
Katibu Mkuu wa TSNP, Alphonce Lusako, alisema mjini Dar es Salaam, jana, kuwa wamependekeza kuongezwa kwa ibara ya 21, katika sura ya 3 (a), itakayohusu maadili ya viongozi .
“Tunapendekeza iwepo sheria itakayowabana viongozi kuwasomesha watoto wao katika shule na vyuo vya ndani badala ya kuwakimbiza nje ya nchi. Wakiwepo hapa, watajenga uzalendo na hata kuwa wepesi kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazoukabili mfumo wa elimu nchini,” alisema.
Pia aliwataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, kuweka kando itikadi na misimamo ya vyama vyao, badala yake waungane kutengeneza Katiba ya Watanzania.
“Tunawaomba CCM, UKAWA, Tanzania Kwanza na wajumbe wengine kufahamu kuwa, kushindwa kwa mchakato huu sio kushindwa kwa chama chochote cha siasa bali ni Watanzania ndio watakuwa wameshindwa,” alisema.
Mwigulu na posho
Kwa upande wake, Mwigulu Nchemba, alishauri bunge hilo kuendeshwa kwa mujibu wa bajeti na wabunge wasiowajibika wabanwe kikamilifu.
Alisema ni muhimu kwa uongozi wa Bunge kujiridhisha katika kuhakikisha wajumbe wanaolipwa posho ni wale waliohudhuria vikao na pia kuorodhesha wajumbe ili kufahamu idadi.
Pia alieleza umuhimu wa kupatikana kwa theluthi mbili kwa ajili ya kuendesha shughuli za Bunge hilo ili kuokoa muda na fedha za umma.
“Tuwabane wale wote wasiohudhuria ili wasilipwe posho kwa sababu hata vitabu vya dini vimesema asiyefanya kazi na asile,” alisema Mwigulu.
Naye Goodluck Ole Medeye, alisema anaomba mjumbe ambaye hakushiriki mjadala, asishiriki kupiga kura na ikiwezekana afutwe ujumbe wake.
Naye, Fahmi Dovutwa, alisema ni kebehi na dharau kwa vyama vya upinzani kudai kuwa Rais Jakaya Kikwete alipozindua bunge hilo, alilenga kuharibu mchakato.
“Jamani tukubali Rais wetu ni smart, hawa walikuwa wanamtega, walitaka wamwambie andika hiki, futa hiki ili baadaye waje kusimama kusema rais amewaingilia. Hila na mchezo mchafu waliotaka kuufanya sasa umekwama,” alisema.
Wajumbe waapishwa
Katika bunge hilo, wajumbe watatu Ridhiwani Kikwete, Godfrey Mgimwa na Haroun Ali Seleman, waliapishwa kabla ya kuanza kwa bunge hilo. Wajumbe hao waliapishwa na Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta.

Taaluma vyuo vikuu sasa kwa mtandao


NA WILLIAM SHECHAMBO
HATIMAYE serikali imezindua mradi wa ujenzi wa mtandao wa Internet kwa vyuo vya elimu ya juu na taasisi za utafiti nchini, ambao utaziunganisha na kuziwezesha kushirikiana katika masuala ya kitaaluma.
Mradi huo uliofadhiliwa na Benki ya Dunia, mara utakapokamilika, unatarajiwa kuziunganisha taasisi 28 huku zingine zikipewa fursa ya kujiunga na mradi huo kwa kadri inavyowezekana.
Serikali ya awamu ya nne imekuwa ikiweka mkazo mkubwa katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA).
Katika uzinduzi huo uliofanyika Dar es Salaam jana kwenye Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, alisema hayo ni mafanikio makubwa kitaaluma.
Hata hivyo, alisema mradi huo ambao ulianza ujenzi wake mwaka 2008, umechelewa kukamilika hivyo alitumia nafasi hiyo kuwaomba radhi Watanzania.
Alisema zipo sababu kadhaa zilizosababisha hali hiyo, ikiwemo matatizo ya makandarasi, ambao walisababisha kuwepo ufinyu wa fedha, ambazo kadri muda unavyosogea, ndivyo thamani yake inabadilika.
“Fedha (Dola) tulizopewa na WB zinabadilika thamani kadri muda unavyokwenda, mkandarasi alikuwa hajakamilisha ujenzi wa mtandao, hivyo alitafutwa mwingine ambaye mpaka anaanza kazi, muda ulishapotea,” alifafanua.
Mbarawa alisema hatua hiyo ilisababisha Benki ya Dunia kutaka kujitoa kwenye mradi huo, hali iliyomlazimu kuwasiliana na wakuu wa vyuo kadhaa ili kutoa msaada kifedha kwa ajili ya kupatiwa huduma ya mtandao kupitia mkongo wa taifa.
Hata hivyo, alisema utaratibu huo uliofanikiwa mpaka sasa, unadhihirisha nia ya serikali ya kuwekeza kwenye Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA), kupitia mkongo wa taifa wenye huduma bora na nafuu, ambapo elimu ya juu nchini itapata fursa za kushirikiana kwa rasilimali zilizopo kwenye taasisi husika na jirani.
Aidha, katika kuhakikisha kuwa matumizi ya TEKNOHAMA nchini yanakuwa kama yalivyokusudiwa kwa kupambana na usalama wa matumizi katika mtandao, Waziri Mbarawa alisema wizara yake imeandaa sera tatu 
zitakazosimamia utumiaji sahihi wa mtandao, ambazo zitawasilishwa bungeni kwa ajili ya kupitishwa huku pia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikifanya kila jitihada kulisimamia hilo.
Naye Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini, Kaboko Kahiga, alisema Watanzania wanatakiwa kutumia vizuri teknolojia hiyo katika malengo yaliyokusudiwa na kwamba taasisi zote za elimu zihakikishe zinajiunga  ili kuliletea maendeleo taifa kupitia teknolojia hiyo, ambayo itawapa soko kimataifa kutokana na maendeleo ya utandawazi.

Kikwete awapa somo Wamarekani


Na mwandishi wetu
RAIS Jakaya Kikwete ameitaka sekta binafsi na wafanyabiashara wa Marekani kujifunza kutoka kwa wenzao wa Bara la Asia, ambao wameongeza uwekezaji barani Afrika.
Amesema hatua hiyo inatokana na kuwa wawekezaji hao wanapata taarifa sahihi na za ukweli kupitia vyombo mbalimbali.
Aidha, Rais Kikwete amesema pingamizi kubwa la kufanya biashara kati ya Marekani na Afrika sio tena Bahari ya Atlantic ama umbali, bali ni maono hasi yanayojengwa na vyombo vya habari vya Marekani kuhusu Bara la Afrika.
Rais Kikwete aliyasema hayo juzi wakati wa sherehe ya kuwekwa kwa Rais Kikwete katika Jumba la Mashujaa wa Uongozi wa Afrika la Jarida la African Leadership– African Leadership Hall of Fame – kwenye Jengo la National Press Club mjini Washington D.C., Marekani ambako Rais anafanya ziara ya siku tisa.
Rais Kikwete anakuwa kiongozi wa tatu wa Afrika kutunukiwa heshima hiyo kubwa. Marais waliotangulia kupewa heshima hiyo ni Rais wa Sierra Leone na Rais wa Namibia.
Akizungumza kabla ya kukabidhiwa medali na cheti cha kutunukiwa heshima hiyo, Rais Kikwete alisema ni jambo la kusikitisha kuwa vyombo vya habari havijali sana maendeleo mazuri ya Bara la Afrika. 
“Matokeo yake ni kwamba sekta binafsi ya Marekani imefanywa kuamini kuwa Bara la Afrika ni bara hatari sana kuwekeza,”alisema na kuongeza:
 “Mara nyingi Afrika inaonekana kama nchi moja badala ya Bara moja, na hivyo tatizo katika nchi moja kwa urahisi sana linafanywa tatizo la nchi zote na kwa namna hasi. Hii ni tofauti na Bara la Asia, ambako vyombo vya habari huelezea picha nzuri za matukio ya Afrika. Hii ndiyo maana kuna ongezeko la uwekezaji wa sekta binafsi ya Asia katika Afrika leo kuliko ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.”
Rais Kikwete ameongeza: “Hivyo, pingamizi kubwa la kufanya biashara kati ya Afrika na Marekani siyo Bahari ya Atlantic wala umbali kati ya maeneo hayo. Pingamizi ni maono hasi. Tunayo kila sababu ya kumshukuru Rais Obama kwa uongozi wake na dhamira yake katika kubadilisha gurudumu hili la historia.”
 “Uamuzi wake wa kuitisha Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika na kuiwekea Sekta Binafsi ya Marekani ushiriki muhimu katika mkutano huu ni uamuzi wa kimapinduzi. Afrika imekuwa inasubiri fursa hii ya kufanya biashara na Marekani kwa muda mrefu. Na tumedhamiria kutumia fursa hii kwa kadri inavyowezekana,”alisisitiza.
Rais Kikwete amelishukuru Jarida la The African Leadership kwa mchango wake mkubwa wa kujenga uhusiano kati ya Afrika na Marekani.
Aidha, Rais Kikwete amelishukuru Jarida hilo kwa kumtunuku tuzo ya Kiongozi Bora wa Kusukuma Maendeleo Mwaka 2013 (The Most Impactful African Leader of the Year Award 2013), tuzo ambayo Rais Kikwete alipewa Aprili 9, 2014. Tuzo hiyo ilipokelewa kwa niaba ya Rais Kikwete na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.