Tuesday 2 September 2014

TUHUMA ZA KIFO CHA MAHABUSU


NA WAANDISHI WETU
JESHI la Polisi limeunda timu kwa ajili ya kuchunguza tukio la askari wake kudaiwa kumshambulia na kusababisha kifo cha mtuhumiwa aliyekuwa mahabusu.
Jopo hilo ambalo majina na viongozi wake hawajawekwa hadharani, limeundwa wakati ndugu wa marehemu wakiweka ngumu kuchukua mwili kwa ajili ya mazishi, wakitaka uchunguzi wa tume huru.
Mtuhumiwa huyo, Liberatus Damian, anadaiwa kushambuliwa wakati akiwa kwenye mahabusu ya Kituo cha Polisi Stakishari, Dar es Salaam, kabla ya hali yake kuwa mbaya na kukimbizwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).
Damian, alitiwa mbaroni Agosti 22, mwaka huu, kwa tuhuma za kumjeruhi Juma Magoma, ambaye walikuwa na mgogoro naye baada ya kutofautiana walipokuwa kwenye baa ya Meku Pub.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, mke wa marehemu, Naomi Liberatus, alisema taarifa ya madaktari inaonyesha mumewe alishambuliwa na kitu kizito kichwani.
Hata hivyo, Naomi alisema katika hali isiyokuwa ya kawaida, Materu alifikishwa katika Hospitali ya Amana akiwa hajitambui huku akiwa uchi, ambapo askari waliomfikisha walidai ni kibaka na wamemuokota hivyo kuomba apatiwe matibabu.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema Damian kabla ya kupelekwa Muhimbili, alikuwa na majeraha yaliyosababishwa na kipigo kutoka kwa wananchi wenye hasira baada ya kumshambulia Magoma kwa mapanga.
Kamanda Kova alisema aliona ni vema ukafanyika uchunguzi wa kina kwa lengo la kuondoa utata wa tukio hilo ili kupata taarifa kamili kuhusiana na ugomvi uliosababisha Damian na Magoma kushambuliana mara kwa mara kila wanapokutana.
Alisema lengo linguine la kuundwa kamati hiyo ni kuchunguza jinsi Damian alivyokamatwa, alivyokaa mahabusu na hadi alivyopelekwa MNH, ambapo watahusisha madaktari bingwa wanaohusika na uchunguzi wa watu waliokufa katika mazingira yenye utata.
“Endapo itagundulika kwamba kuna mkono wa mtu katika kifo cha Damian, polisi haitasita kuchukua hatua ili sheria ichukue mkondo wake.
Kama kuna mtu yeyote anazo taarifa za ziada kuhusiana na shauri hili, aziwasilishe kwa mkuu wa upelelezi ambaye ndiye kiongozi wa jopo hilo,” alisema.
Akizungumza juzi na waandishi wa habari, Naomi alisema baada ya Damian kukamatwa, siku iliyofuata walianza harakati za kufuatilia dhamana ambapo, waliambiwa wasubiri kuangalia hali ya afya ya Magoma.
Alisema Agosti 29, mwaka huu, akiwa katika harakati za kufuatilia barua za dhamana, alipigiwa simu ya kumtaka asiende tena kituoni bali awahi Amana kwa sababu mumewe alipelekwa kwa ajili ya matibabu.
“Nikiwa katika hali ya mshangao baada ya kuambiwa kuwa mume wangu anaumwa na ana hali mbaya wakati jana yake nilikwenda kituoni na nikaongea naye na hakuwa na jeraha au hali yoyote ya kuonyesha kuwa ni mgonjwa.
“Nilimpigia simu shemeji yake ambaye anamiliki gereje iliyoko Amana, ambapo alifika kabla ya gari la polisi lililompakia halijafika, lakini hakuweza kumuona.
“Baada ya muda aliona gari la polisi likiwa limempakia marehemu mume wangu, ambaye alikuwa amevimba uso na macho yakiwa yamevilia damu na majeraha mikononi huku akiwa uchi ndipo, akanieleza kinachoendelea,” alisema Naomi.
Mke huyo wa marehemu aliongeza kuwa baada ya askari kumfikisha hospitalini hapo, walidai ni kibaka na alikuwa amepigwa na wananchi wenye hasira, ndipo baadhi ya ndugu walipokuja juu na kuwaeleza ukweli madaktari kuwa ndugu yao si kibaka bali ni mahabusu.
Alisema baada ya hapo madaktari walishauri akimbizwe Muhimbili kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi, ambapo baada ya kufika huko alifanyiwa kipimo cha CT Scan ya kifua na kugundulika kuwa alikuwa amepigwa na kitu kizito upande wa kushoto na damu nyingi zilikuwa zinavuja na kuchanganyika na ubongo.
Mke huyo wa marehemu alisema baada ya taarifa hiyo, waliambiwa anatakiwa kufanyiwa upasuaji wa kichwa haraka, ndipo walipoanza kuchangishana na Ijumaa usiku alifanyiwa upasuaji huku akiwa chini ya ulinzi.
Alisema siku iliyofuata walipeleka taarifa kituo cha Sitakishari kuhusu hali ya ndugu yao na kuwaomba wafike hospitali kwa ajili ya kufuatilia matibabu yake.
Kutokana na mazingira ya kifo hicho, msemaji wa familia hiyo, Jimy Sanga, alisema leo mwili wa Damian unatarajia kufanyiwa uchunguzi ili kubaini sababu za kifo chake na hawatauzika hadi watakapoelezwa sababu za ndugu yao kushambuliwa hadi kufa huku akiwa chini ya ulinzi wa polisi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru