Tuesday 9 September 2014

Waliokufa, majeruhi ajali ya basi waanza kutambuliwa


NA LATIFA GANZEL, MOROGORO
MAITI mbili kati ya nne za ajali ya basi la kampuni ya Air Bus iliyotokea juzi wilayani Gairo, zimetambuliwa.
Basi hilo lilipata ajali likiwa safarini kutoka Dar es Salaam kwenda Tabora.
Aidha, majeruhi 30 wa ajali hiyo bado wamelazwa katika hospitali za Berega na ya rufani ya mkoa wa Morogoro, wakipatiwa matibabu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonard Paul,  alisema jana ofisini kwake mjini hapa kuwa waliotambuliwa ni Amina Rashid (50), mkulima na mkazi wa Tegeta, Dar es Salaam na Makoye Hamis (34) mkulima na mkazi wa Tabora.
Kamanda huyo alisema na tayari ndugu wamezichukua maiti hizo kwa ajili ya kusafirisha na kufanya utaratibu wa mazishi.
Kamanda Paul pia alitaja majina ya majeruhi hao 30 na kwamba majeruhi 16 wamelazwa Hospitali ya Berega na majeruhi 14 wamelazwa Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Morogoro.
Aliwataja majeruhi waliolazwa Morogoro kuwa ni Amood Said, Augustino Mbago, Novatus Patrick, Paulo Lucas, Single Salum, Jieleza Salum, Lazaro Clemence, Omary Amiri, Laurencia Deo na Neema Hamis wote watoto, Nasra Hassan, Hadija Yusuph, Asha Kobongo na Halima Adam.
Wengine waliolazwa katika hospitali ya Berega ni Rajabu Juma, Uweso Chamalupe, Emanuel Joel, Bakari Edmond, Fidelis Laurent, Mashala Shagembe, Magembe Salum, Isaya Clemence, Julieth Magomba, Joha Athumani, Esta Chagoma, Asha Musa, Lidya Claud, Helieth Kayaya, Daniel Lanford na Anjela Michael.
Kamanda huyo alisema kuwa hali za majeruhi zinaendelea vizuri na kuwataka wananchi kujitokeza kutambua maiti mbili zilizobaki ambazo ni za wanaume.
Pia alisema jeshi hilo mpaka sasa linamtafuta dereva wa basi ambaye alitoweka kusikojulikana baada ya kutokea kwa ajali.
Ajali hiyo ilitokea juzi saa 5.45 katika eneo la Berega, Gairo ambapo  basi la Airbus lilipinduka na kuacha njia na kutumbukia katika daraja la Mto Mkange na kusababisha vifo vya watu wanne na majeruhi 34.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru