Thursday 4 September 2014

Uenyekiti waipasua CHADEMA

  • Mikakati kumtosa mpinzani wa Mbowe yaiva
  • Wagombea wengine wageuzwa kiini macho 
  • Mtandao wa Zitto hatari, kuendelea kufyekwa 
NA MWANDISHI WETU
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetangaza majina ya makada wake wanaowania nafasi za uongozi ngazi ya taifa huku majina ya vigogo na wabunge yakisheheni.
Tayari uchaguzi huo umezidi kukiweka njiapanda chama hicho kutokana na makada wengi kuenguliwa kwenye ngazi za majimbo na mikoa, ikiwa ni mkakati wa kuwatosa wanachama wapenda mabadiliko.
Hata hivyo, katika orodha hiyo iliyotangazwa mjini Dar es Salaam jana, majina ya wagombea wanaowania nafasi ya Mwenyekiti Taifa haikuwekwa hadharani.
Freeman Mbowe
Nafasi hiyo inawaniwa na Mwenyekiti wa sasa, Freeman Mbowe, Daniel Luvanga, Gambaranyera Mongateo na Kansa Mbarouk, ambaye anatajwa kuwatia vigogo wa chama hicho matumbo joto.
Pia, anadaiwa alikuwa swahiba wa aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, ambaye mtandao wake ndani ya chama hicho umeendelea kusambaratishwa kutokana na kuwa na misimamo na kutokubali kuyumbishwa. 
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa Oganaizesheni, Mafunzo na Uratibu wa Kanda wa CHADEMA, Singo Kigaila, alisema majina ya wagombea nafasi ya mwenyekiti yanaendelea kuchambuliwa.
Alisema Kamati ya Uchaguzi inaendelea kuyapitia kwa umakini majina na taarifa za wagombea kabla ya kutoa maamuzi sahihi kulingana na vigezo.
Hata hivyo, habari za kuaminika kutoka ndani ya CHADEMA zimesema, kinachofanyika kwa sasa ni kuangalia mikakati ya kuwachinja baadhi ya wagombea ili kutoa fursa kwa Mbowe kupata ushindi wa kishindo.
Chanzo hicho kimesema kuwa, kazi ya kuchambua taarifa za wagombea wa nafasi hiyo haiwezi kuwa ngumu kwa kuwa idadi iliyojitokeza ni ndogo na wote ni makada wanaofahamika.
Kimesema nafasi ya Kamati Kuu ya CHADEMA ambayo, ndio nyeti katika chama cha siasa, ina wagombea 56 huku idadi inayotakiwa ni wajumbe wanane, ambao wote taarifa zao zimepitiwa na majina kutangazwa.
Miongoni mwa wanaowania ujumbe wa Kamati Kuu ni Profesa Mwesige Baregu, Bernad Saanane, Ansbert Ngurumo, Suzan Kiwanga, John Mwambigija, Methayo Torongey, Rose Kamili, Vicent Munghwai, Mwita Mwikabe Waitara, Alphonce Mawazo na Chiku Abwao.
Habari zaidi zimesema kuwa, hatua ya Mbarouk kuchukua fomu kupimana ubavu na Mbowe, imewashitua baadhi ya viongozi kwa kuwa hawakutarajia kada huyo kijana kuibuka.
Hatua hiyo inatokana na ushawishi mkubwa aliokuwa nao Mbarouk ndani ya CHADEMA huku kansa ya mpasuko iliyoikumba ikiendelea kukitafuna ndani kwa ndani.
“Hawawezi kutangaza majina ya wagombea wa uenyekiti hadi mikakati yao ya kumfyeka Mbarouk itakapokuwa imekaa vizuri. Wanafahamu uwezo na nguvu ya ushawishi aliyokuwa nayo huyu kijana, hivyo ni lazima wajipange. 
“Kinachofanyika ni kuhakikisha wanakata jina lake mapema ili wajihakikishie kutawala tena, hivyo wakifanya mambo kwa haraka, kuna wengine wanaweza kukimbilia mahakamani kusimamisha uchaguzi,” alisema na kuongeza: 
“Bado kuna makada hawafurahishwi na mwenendo wa CHADEMA na kwamba, wanaweza kupiga kura za maruhani na kusababisha fedheha iwapo Mbarouk atasimama mbele ya wajumbe kuomba kura.”
Dalili za kumdhibiti Mbarouk zilianza kuonekana siku aliyotangaza kuchukua fomu, ambapo aliwekewa mizengwe mbalimbali huku wafuasi na walinzi wake waliomsindikiza wakizuiwa kuingia ofisini.
Mbarouk alikuwa Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Tabora, ambapo kabla ya kukuchukua fomu kuwania nafasi hiyo, alijiuzulu nyadhifa zake zote na kuonya kuwa, amejitokeza kwa lengo la kumdondosha Mbowe.
Vigogo BAWACHA
Nafasi nyingine ambayo inatarajiwa kukipasua chama hicho ni ya Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake (BAWACHA), ambapo vigogo kadhaa wakiwemo wabunge wamejitosa kuipigania.
Waliojitosa kuwania nafasi hiyo ni Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Iringa, Chiku Abwao na Lilian Wassira. Wengine ni Janeth Rithe, Rebecca Magwisha na Sophia Mwakagenda.
Hata hivyo, habari za kuaminika zinasema Lilian ndiye alikuwa anapewa nafasi kubwa ya kuongoza baraza hilo, lakini kutokana na misimamo yake, amewekewa wapinzani.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha mwanasiasa huyo kijana na mwenye kukubalika, anapata wakati mgumu kwenye kusaka ushindi. Kwa sasa washindani wakubwa kwenye kundi hilo ni Chiku na Halima.
Chanzo chetu ndani ya CHADEMA kimesema kuwa, baadhi ya makada hao walichukua fomu za kuwania nafasi hiyo siku za lala salama na kwamba, walipata msukumo wa kufanya hivyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru