Tuesday 3 March 2015

Mauaji ya albino yavuka mipaka

                                                                         


NA MWANDISHI MAALUM, BLANTYRE
WAKATI Rais Jakaya Kikwete akitangaza vita na mtandao hatari unaojihusisha na utekaji na mauaji ya walemavu wa ngozi (albino), matukio hayo kwa sasa yameshika kasi nchini Malawi.
Juzi, wakati akihutubia taifa katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, Rais Kikwete alisema serikali itahakikisha inasambaratisha mtandao huo na kuwataka watanzania wote kushiriki kwenye vita hiyo.
Hata hivyo, imebainika kuwa baada ya serikali kuunda kikosi maalumu cha kukabiliana na mtandao huo, matukio ya kuuawa kwa albino yamehamia nchini Malawi.
Habari za kuaminika zinasema tayari walemavu wa ngozi watatu wameuawa katika kipindi cha miezi mwili, hatua ambayo inatajwa kuwa ni mbaya na serikali imeanza kukabiliana na wimbi hilo.
Rais wa Chama cha Maalbino nchini Malawi (APAM), Boniface Massah, alisema hofu imetanda katika kila kona na watu wenye ulemavu wamekuwa wakiishi kwa hofu kuhofia maisha yao.
Alisema chama chake kinahofu kwamba kuongezeka kwa mauaji hayo, kunatokana na udhibiti na hatua kali zilizotangazwa na Tanzania dhidi ya mauaji ya albino.

"Hivi sasa hatuna amani, tunaishi kwa shaka kwa kuwa wakati wowote tunaweza kunaswa na kuuawa," alisema.

Akizungumzia moja ya matukio ya vifo vitatu vilivyotokea mwaka huu, Massah alisema mama mmoja ambaye hakumtaja jina, alikutwa ameuawa na kukatwa baadhi ya viungo vyake.
Baadhi ya viungo vilivyokatwa kutoka kwa mwanamke huyo ni kichwa, mikono na miguu ambavyo vinaaminika kutumika kwa imani za kishrikina.
Kasi hiyo inaonekana kuwa kali ikilinganishwa na miaka mitatu iliyopita ambapo, maalbino wawili waliripotiwa kuuawa.
Katika kipindi cha hivi karibuni, kumekuwepo na matukio ya kutekwa na kuuawa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, na kusababisha hofu kubwa.
Kwa mujibu wa Shirika la Kutetea Haki za Maalbino la Under The Same Sun (UTSS), watu 140 wenye ulemavu huo wameshauawa kati ya mwaka 1998 na 2015 kwenye nchi 25 za Afrika.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru