Tuesday 10 March 2015

Zitto yametimia


NA WAANDISHI WETU

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, imetupilia mbali kesi ya msingi iliyokuwa imefunguliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), dhidi ya chama hicho.
Kutokana na kutupiliwa mbali kwa kesi hiyo, uongozi wa CHADEMA, ulitangaza jana kumtimua  uanachama Zitto na kumvua nyadhifa zake zote za kichama.
Uamuzi wa mahakama ulitolewa jana na Jaji Richard Mziray, baada ya kukubaliana na moja ya mapingamizi ya awali yaliyowasilishwa na mawakili wa CHADEMA, kupinga kesi hiyo.
Zitto alifungua kesi hiyo namba moja ya mwaka jana, dhidi ya bodi ya wadhamini ya chama hicho na Katibu Mkuu wa CHADEMA.
Katika shauri hilo, alikuwa anaiomba mahakama iamuru Kamati Kuu ya CHADEMA na chombo chochote cha chama hicho, kutojadili na kuchukua uamuzi kuhusu uanachama wake hadi rufani yake itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi na baraza kuu la chama hicho.
Pia alikuwa anaiomba mahakama imwamuru katibu mkuu huyo, ampatie mwenendo wa kikao cha Novemba 22, mwaka jana, cha baraza kuu ambacho kilifikia uamuzi wa kumvua nyadhifa zake zote za kichama.
Akitoa uamuzi huo, Jaji Mziray alikubaliana na mapingamizi yaliyowasilishwa na mawakili wa CHADEMA na kuitupilia mbali kesi hiyo, kwa kuwa ilifunguliwa bila ya kufuata utaratibu wa kisheria.
Jopo la mawakili wa CHADEMA, likiongozwa na Tundu Lissu, akishirikiana na Peter Kibatala na John Mallya, waliwaslisha mapingamizi ya awali matano kupinga shauri hilo.
Moja ya mapingamizi hayo, yalikuwa ni kwamba kesi kufunguliwa Mahakama Kuu haikuwa jambo sahihi kwa kuwa ingepaswa kufunguliwa mahakama ya wilaya au hakimu mkazi kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Kesi za Madai.
Pia, walidai kesi hiyo ilikosewa kufunguliwa Mahakama Kuu, Masijala Kuu badala ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam.
Katika uamuzi wake, Jaji Mziray alikubaliana na mawakili wa CHADEMA na kutupilia mbali kesi hiyo na kuamuru chama hicho kulipwa gharama zote za kuendeshea shauri hilo.
Wakizungumza baada ya kutolewa kwa uamuzi huo, Kibatala alisema akiwa wakili, alitumwa mahakamani hapo na CHADEMA, hivyo amemaliza kazi yake na atakabidhi nakala ya hukumu kwa chama.
Kwa upande wake, Lissu alisema kwa mujibu wa katiba ya CHADEMA, ni marufuku kupeleka mambo ya chama mahakamani kwa kuwa unajifukuzisha uanachama mwenyewe.
Atangazwa kutemwa rasmi
Baada ya mahakama kutoa uamuzi huo, CHADEMA ilifanya mkutano na waandishi wa habari katika makao makuu ya chama hicho, Kinondoni, Dar es Salaam, ambapo Mwanasheria wa chama hicho, Lissu alitangaza kumfukuza uanachama Zitto.
Lissu, ambaye ni Mbunge wa Singida Mashariki,  alisema katika kufungua kesi hiyo, Zitto alikiuka utaratibu kwa kuwa hakupaswa kufungua Mahakama Kuu ya Tanzania bali katika Mahakama ya Hakimu Mkazi au Masijala ya Wilaya ya Mahakama Kuu.

“Katiba ya CHADEMA inatamka wazi hatua  anazochukuliwa mwanachama baada ya kuikiuka, ambazo ni kwamba haruhusiwi kuchukua hatua za kukishitaki chama mahakamani.

“Zitto alikishitaki chama mahakamani, hivyo alipuuza katiba ya chama. Kutokana na hatua hiyo,  CHADEMA imemfukuza rasmi uanachama kuanzia leo hii (jana),” alisema  Lissu.

Alisema  chama hicho kilikwishamfukuza uanachama Zitto muda mrefu, lakini uamuzi ule ulikuwa wa kisiasa.
Alisema baada ya Zitto kukimbilia mahakamani na mahakama kufutilia mbali pingamizi lake, chama kimemfukuza na kumvua nyadhifa zake zote.

“Kuanzia leo (jana) Zitto si mwanachama wa CHADEMA na tutawasilisha taarifa Tume ya Taifa ya Uchaguzi  ili kuieleza kuwa yule aliyekuwa mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa dhamana ya CHADEMA, Zitto Kabwe, si mwanachama  tena wa chama hicho,” alibainisha mwanasheria huyo.

Alisema Zitto alitabiri mwenyewe kupitia vyombo vya habari, ambapo  CHADEMA ilimnukuu akisema kuwa hatima yake ndani ya chama itakuwa ni Machi, mwaka huu.

“Alitabiri mwenyewe kuwa hatima yake itakuwa mwezi Machi, mwaka huu. Hatimaye imetimia leo (jana). Kesi hamna na uanachama hamna. Umekoma rasmi,” alisema.

Akizungumzia juu ya nguvu ya Zitto na umuhimu wake  ndani ya CHADEMA, hususan kutokana na kujizolea umaarufu zaidi kupitia sakata la akaunti ya Tegeta Escrow, Lissu alidai sauti ya Zitto katika sakata hilo ilitokana na uamuzi uliokuwa unachukuliwa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) anayoiongoza na si vinginevyo.

“Itakumbwa kuwa, wakati sakata la Escrow linajadiliwa bungeni, lilipingwa vikali kiasi cha Zitto kutaka kubwaga manyanga ili lisijadiliwe.

Lakini sauti yetu kama Ukawa ndiyo ilichochea suala hilo kujadiliwa na watuhumuwa kuchukuliwa hatua. Yeye mwenyewe alikuwa na tuhuma za kuchota fedha. Hivyo alikuwa hana sauti. Sifa ile ya Escrow haiwezi kumfanya Zitto aonekane maarufu kama Zitto bali ni kwa kamati nzima ya PAC,” alisema Lissu.

Lissu alimshambulia Zitto kwa kudai kwamba kama anategemea kupata sifa kwa wananchi kupitia sakata la Escrow,  imekula kwake.

“Isitoshe katika uongozi wake, CHADEMA ilipoteza nguvu Kigoma Kaskazini, lakini baada ya uongozi kuchukua uamuzi wa kuwaondoa wale wote waliokuwa wanakisaliti chama, akiwemo yeye CHADEMA Kigoma imeanza kuimarika,” alisema.

Mwigamba: CHADEMA ni dhaifu
Katibu Mkuu wa Chama cha ATC, Samson Mwigamba, alisema maamuzi yaliyochukuliwa na CHADEMA yanaonyesha udhaifu mkubwa kisiasa.
Alisema viongozi wa chama hicho si waelewa na kwamba uamuzi wa kumfukuza ulikuwa uchukuliwe na Kamati Kuu ya CHADEMA na sio Lissu.
Hata hivyo, alisema hakuna haja kwa Zitto kung’ang’ania CHADEMA, badala yake alimtaka ajiunge na ATC.
Zitto: Sivurugiki ng’o
Jitihada za kumtafuta Zitto kuzungumzia uamuzi huo, hazikuweza kuzaa matunda hata alipotafutwa kupitia simu yake ya kiganjani, ambayo muda mwingi ilikuwa imezimwa.
Hata hivyo, kupitia mtandao wake wa kijamii, Zitto aliandika kuwa ameshangazwa kama suala la kashfa ya Escrow lingepita kimya kimya.
Amesema kwa namna kazi hiyo ilivyofanyika, waathirika wa kashfa hiyo wasingeweza kukaa kimya bila kujaribu kumvuruga, lakini kwa bahati mbaya havurugiki.
Aliongeza kuwa kwa sasa anaendelea na kazi zake za Kamati ya PAC kama kawaida na jana, walikutana na maofisa wa EWURA kujadili masuala mbalimbali.

“Ningeshangaa kama Escrow ingepita kimya kimya bila waathirika kujaribu kunivuruga. Bahati mbaya sana sivurugiki, leo (jana) tumekutana na EWURA kukagua hesabu zao, kesho (leo) tutakutana na TANESCO kisha tutamalizia na mabilioni ya Uswisi,” alisema.

Hata hivyo, kuhusiana na kufukuzwa uanachama na uamuzi wa mahakama, alisema hafahamu lolote kwa kuwa hakuwa na wito wa mahakama.
Pia, alisema jaji anayesikiliza kesi hiyo, Jaji John Utamwa, amehamishiwa mkoani Tabora na hakuna taarifa ya kuwepo kwa jaji mpya mpaka sasa.
Aliongeza kuwa mwanasheria wake anafuatilia suala hilo na baadaye watatoa tamko rasmi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru