Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Tuesday, 25 June 2013

Wafanyakazi 15 TRA wachunguzwa

Na Epson Luhwago, Dodoma
BUNGE limepitisha bajeti ya serikali kwa mwaka 2013/2014, ambayo itatumia sh. trilioni 18.2 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo. 
Bajeti hiyo ilipitishwa jana kwa wabunge kupiga kura kukubali au kuikataa. Jumla ya wabunge 270 walikuwepo wakati wa kupiga kura, ambapo kura za NDIYO zilikuwa 235 na za HAPANA 35.
Wabunge wote wa CCM waliokuwepo waliikubali, huku wapinzani wakiikataa. CHADEMA hawakupiga kura kwa madai hawakushiriki kuijadili.
Hata hivyo, mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP), kama ilivyo ada, aliikubali. Alisema anaiunga mkono tangu alipokuwa akiijadili. Kila mwaka amekuwa akiunga mkono bajeti ya serikali.
Licha ya upigaji kura ambao ni hatua ya mwisho, wabunge walijadili kwa siku nne mfululizo na kutoa hoja mbalimbali. Wabunge 119 walichangia kwa kusema na wengine 36 kwa maandishi.
Awali, akijibu hoja za wabunge waliochangia, Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, alisema bajeti iliyopitishwa imekidhi vigezo na kujibu maswali muhimu ambayo wataalamu wa bajeti wanataka yazingatiwe.  Vigezo hivyo, kwa mujibu wa Waziri Mgimwa ni kuleta unafuu kwa wananchi, kiwango cha upunguzaji umasikini, kutambua umuhimu wa makundi yaliyosetwa kama wanawake na vijana, na kutambua vipaumbele muhimu.
“Bajeti hii imekidhi mambo hayo muhimu kwa sababu imetoa majibu kwa kuweka kipaumbele kwenye uwekezaji wa mambo muhimu ya kiuchumi. Mfano ni kutengwa kwa sh. trilioni 1.2 kwa ajili ya miundombinu ya barabara, umeme na usafirishaji ili kuchochea uzalishaji nchini,” alisema.
Katika kudhihirisha bajeti inajali maisha ya wananchi, Dk. Mgimwa alisema serikali imejikita katika kutatua kero za maji, umeme, pembejeo za kilimo na umeme vijijini.
Alisema umeme vijijini pekee umetengewa sh. bilioni 186 ili kuwawezesha wananchi wa maeneo hayo yapate nishati hiyo na maji yametengewa sh. bilioni 184.5.
Maeneo mengine yaliyopewa kipaumbele kwa kuongezewa bajeti na kiasi katika mabano ni uwekezaji maeneo maalumu -EPZ (sh. bilioni 30), usafirishaji (sh. bilioni 30), mifugo (sh. bilioni 20) na mfuko wa mbolea (sh. bilioni 21.5).
Kuhusu hoja ya kukusanya kodi kutoka kampuni za madini, alisema zimekuwa zikikusanywa na juhudi zinafanywa ili kuzibana ziweze kulipa kodi zaidi kutokana na fedha zinazopata.
Alisema kampuni hizo zimekuwa zikilipa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), kampuni, maendeleo ya elimu, ushuru wa stempu na kodi za mapato.
Dk. Mgimwa alitoa takwimu za kodi zinazolipwa kwa miaka mitano katika mabano kuwa, 2007/08 (sh. bilioni 69.5), mwaka 2009/10 (sh. bilioni 66.6), 2010/11 (sh. bilioni 85.5), 2011/11 (sh. bilioni 119), 2011/2012 (sh. bilioni 274.8) na kwa mwaka 2012/13 hadi kufikia Machi mwaka huu zilikusanywa sh. bilioni 251.8.
“Kwa miaka yote hiyo mitano, serikali imekusanya sh. bilioni 867.38 kutoka kwa kampuni za Bulyanhulu, North Mara, Pangea, Resolute, Tanzanite One na Williamson Diamond,” alisema. 
Kwa kampuni zinazofanya utafiti na utafutaji wa mafuta na gesi, alisema haziwezi kutozwa kodi kwa kuwa hazijaingizwa katika utaratibu huo, kwani hazijaanza kuzalisha.
Hata  hivyo, Dk. Mgimwa aliwaondoa hofu juu ya kasi ya kupungua kwa mfumuko wa bei kutoka asilimia 19.8 hadi asilimia 8.4 kwa kusema ni takwimu ni za kweli.
Alisema hatua hiyo imetokana na kudhibiti uhaba wa chakula na mafuta, ambavyo ndivyo chanzo kikuu cha kupanda kwa mfumuko wa bei. Pia alisema hatua hiyo ilitokana na kupunguzwa kwa ushuru wa bidhaa za mafuta na kuwabana waliokuwa wakichakachua.
Waziri alisema kodi ya mapato kwa wafanyakazi iliyopendekezwa kupunguzwa hadi asilimia 10 kutoka asilimia 13 iliyopendekezwa na serikali itabaki kama ilivyo. Aliahidi kuwa kodi hiyo itapunguzwa mwaka hadi mwaka.
Katika harakati za kupunguza matumizi makubwa yasiyo na tija,  alisema serikali imekubali hoja za wabunge na kwamba kuanzia mwaka ujao wa fedha magari yatanunuliwa kwa mfumo wa jumla. Pia alisema serikali itapunguza misamaha ya kodi kwa maeneo yasiyo na tija.
Alisema serikali inakusudia kubadilisha sheria ya ununuzi wa umma ili kuwabana wanaonufaika na mfumo wa sasa na kuigharimu serikali fedha nyingi katika eneo hilo.

WAFUTWA KAZI TRA
Katika hatua nyingine, wafanyakazi 15 wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wamefukuzwa kazi katika miaka mitatu iliyopita kwa kujihusisha na njama za kuikosesha serikali mapato.
Naibu Waziri wa Fedha, Janet Mbene, alisema hayo bungeni jana, alipojibu hoja za wabunge waliochangia hotuba ya bajeti ya serikali ya mwaka 2013/2014.
Alisema wafanyakazi hao walifukuzwa kazi kutokana na  kushirikiana na wafanyabiashara kukwepa kodi, hivyo kuifanya serikali kukosa mapato yanayostahili.
Kwa mujibu wa Janet, wafanyakazi hao wamefukuzwa kazi kati ya mwaka 2010 na Mei, mwaka huu, katika sehemu mbalimbali ikiwemo, Dar es Salaam.
Kuhusu kuhamishwa kwa maofisa waliotuhumiwa kuhusika na wizi wa makontena bandarini, alisema hatua hiyo imefanyika ili kutoa nafasi kwa uchunguzi unaoendelea.
“Huo ni utaratibu wa kawaida wa TRA kwa kuwa huwezi kumwacha mtuhumiwa katika kituo chake cha kazi wakati uchunguzi unafanyika. Baada ya kukamilika uchunguzi hatua zinazostahili kwa mujibu wa sheria zitachukuliwa,” alisema.
Naibu waziri alisema utoroshaji wa makontena bandarini, ulifanywa na maofisa wa mamlaka hiyo kwa kushirikiana na mawakala wa forodha wasio waaminifu. Alisema mawakala hao watachukuliwa hatua kulingana na ripoti ya uchunguzi itakayotolewa.
Alikiri rushwa imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa serikali kukosa mapato ndani ya TRA na kutokana na hilo, mamlaka imeanzisha mkakati wa kupambana na rushwa, ambao umesaidia kubaini wahusika na kuwachukulia hatua.
Ili kuhakikisha wafanyakazi wanaoajiriwa wanakuwa waadilifu, alisema hivi sasa TRA imekuwa ikiwafanyia uchunguzi kupitia vyombo mbalimbali vya usalama ndani na nje ya mamlaka. 
MADUKA YAFUTIWA LESENI
Wakati huo huo, maduka 17 ya kubadilishia fedha yamefutiwa leseni kutokana na kukiuka sheria na masharti ya uendeshaji wa shughuli, imefahamika.
Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, alisema bungeni jana kuwa, maduka hayo yamechukuliwa hatua baada ya kubainika yalikuwa yakiendesha shughuli kinyume cha utaratibu.
Alisema maduka mengine matano yamefungiwa kwa muda, 33 yametozwa faini na mengine 103 yamepewa onyo kali kutokana na makosa yaliyofanywa kutokuwa makubwa.
Saada alisema hatua hiyo iliyochukuliwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambayo ndiyo msimamizi wa maduka hayo, kwa mujibu wa Sheria ya Kubadilisha Fedha.
Alisema moja ya makosa yaliyofanywa na maduka hayo ni kutokufanya biashara inayozidi dola 10,000 (zaidi ya sh. milioni 160) kwa siku kwa duka moja.
“Hiki ndicho kiwango cha juu kwa bureau de change (duka la kubadilisha fedha). Kiasi kinachozidi hapo ni lazima kiombewe kibali, vinginevyo hatua zinaweza kuchukuliwa,” alisema.
Alisema kwa sasa, ili maduka hayo yaweze kufanya kazi kwa mujibu wa sheria, masharti makali yamewekwa, ikiwemo ya kusajiliwa kama kampuni.
Sharti la pili kwa mujibu wa Saada ni wamiliki lazima wawe Watanzania na la tatu ni kutofanya biashara nyingine nje ya kubalisha fedha.

Gharama huduma za simu



Na waandishi wetu, Dar na Dodoma

SERIKALI imesema itaanza kuzibana kampuni za simu ili zilipe kodi na mapato stahili, pia kuwashirikisha Watanzania katika umiliki wake.

Katika kufanya hivyo, imesema itaweka mtambo maalumu wa kufuatilia miamala yote ya kampuni hizo na kuziingiza katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).
    
Serikali imesema kamwe gharama za huduma za simu hazitaongezwa, kwa kuwa kuziongeza ni kuwanyonya Watanzania, kwani gharama za uendeshaji zimeshuka kwa kiwango kikubwa.

Naibu Waziri wa Fedha, Janet Mbene, akijibu hoja za wabunge waliochangia hotuba ya bajeti ya serikali kwa mwaka 2013/2014, alisema suala la kampuni za simu kutokulipa kodi stahili limekuwa kilio cha muda mrefu.

Alisema ili kuhakikisha serikali inapata mapato hayo, kampuni hizo kuanzia mwaka ujao wa fedha zitawekewa mtambo maalumu utakaofuatilia miamala na viwango vyote vinavyotozwa na kampuni hizo. 

Kwa mujibu wa Janet, mtambo huo maalumu utakuwa ukisimamiwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

“Mtambo huu utasaidia kudhibiti wizi wa aina yoyote na kubaini miamala ya fedha ndani ya kampuni hizo, pia kutambua kama kuna udanganyifu wowote unaofanywa,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, alisema serikali imeanzisha vikosi kazi kwa ajili ya kuzifuatilia kampuni hizo ili kuhakikisha zinaingizwa kwenye orodha ya kampuni zilizoko DSE.

Saada alisema vikosi kazi hivyo vinatokana na sheria mpya inayolenga kuzidhibiti kampuni hizo na vitakuwa chini ya TCRA na Wizara ya Nishati na Madini kwa ajili ya kudhibiti kampuni za madini nazo kuingia katika soko la hisa. 

Alisema Kampuni ya Airtel imeorodheshwa kwenye soko hilo pamoja na zingine za sukari za Kilombero na Mtibwa, Saruji Mbeya, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Kampuni ya Mabati ya ALAF Limited na kampuni ya vyombo vya umeme ya TANELEC.

Kampuni hizo zinaungana na Benki ya NMB, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), TOL Gases Limited, Swissport, Saruji Tanga na CRDB.

“Kuingia kwa kampuni hizo katika soko la hisa, kutawawezesha Watanzania kupata fursa katika umiliki na kuendesha uchumi wa nchi.

Wabunge waliochangia bajeti walisema serikali imekuwa ikikosa mabilioni ya shilingi kwa mwaka kutokana na kampuni za simu kutokulipa fedha kupitia huduma mbalimbali zinazotoa kwa wateja.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, alisema kampuni hizo zinatumia gharama ndogo kujiendesha hivyo, gharama kwa watumiaji zinapaswa kupungua zaidi na si kuongezeka.

Alisema kwa sasa serikali ipo katika mchakato wa kuangalia gharama za uwekezaji katika kampuni hizo ili iweze kukusanya kodi inayostahili, kwa kuwa kuna udanganyifu mkubwa.

“Tusingependa wananchi waathirike wala kubebeshwa mzigo wa gharama, kampuni hizi zinatumia gharama ndogo kujiendesha kwa kutumia mkongo wa taifa wa mawasiliano,” alisema.

Alisema kampuni hizo zimevunja  sheria ya soko huria kwa kukutana na kupanga kupandisha gharama kinyume cha sheria.

“Hairuhusiwi kisheria kampuni zinazofanya biashara moja kukaa na kukubaliana kupandisha gharama, huo si ushindani na suala hili halikubaliki,” alisema.

Kampuni hizo kupitia Chama cha Wamiliki wa Simu za Mkononi Tanzania (MOAT), zimetangaza gharama za matumizi ya simu zitapanda kuanzia Julai Mosi, mwaka huu. 

Hatua hiyo imeelezwa huenda  inatokana na serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2014 kueleza itazitoza kodi kwa asilimia 14. 

LIKO MTAANI


Thursday, 20 June 2013

Mbowe, Lema wahojiwa kwa saa tano

MWENYEKITI wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbelss Lema, wamachiwa kwa dhamana baada ya kuhojiwa kwa saa tano katika Makao Makuu ya Polisi Jijini Arusha. Mbowe na Lema walihojiwa na maofisa wa polisi wakiongozwa na Mkuu wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi Nchini, Paul Chagonja.
Picha tofauti Mbowe na Lema na viongozi wengine wa chama hicho wakitoka nje ya makao makuu ya polisi. ZAIDI SOMA UHURU KESHO

Pinda avipa rungu vyombo vya dola


Na Theodos Mgomba, Dodoma
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, amesema serikali itatumia njia yoyote inayostahili ili
kuwadhibiti wote watakaojaribu kuvunja amani na utulivu nchini. ia amesema mtu yeyote
atakayefanya fujo na akakaidi amri ya vyombo vya dola, atapigwa kwa kuwa hamna namna
nyingine.
Waziri mkuu alisema hayo bungeni jana, alipojibu maswali ya papo kwa hapo.

Mbowe, Lema wajisalimisha Polisi Arusha


MWENYEKITI wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, wamejisalimisha kwa jeshi la polisi leo asubuhi. Wanasiasa hao walipewa onyo la kujisalimisha jana kwa ajili ya kutoa ushahidi kuhusu madai yao kuwa wanawafahamu polisi waliolipua bomu kwenye mkutano wa hadhara.
Hata hivyo, habari kutoka ndani ya jeshi hilo zinasema kuwa, Mbowe amekanusha kusema kuwa ana ushahidi kuhusu polisi waliolipua bomu hilo wakati akihojiwa na maofisa wa polisi. Lakini baadaye baada ya kuachiwa kwa dhamana na kuzungumza na waandishi wa habari, alidai tena ana ushahidi na atauwasilisha kwenye tume maalumu itakayoundwa kuchunguza tukio hilo.
Habari zaidi, soma gazeti la Uhuru kesho Ijumaa.

Wednesday, 19 June 2013

Simba huru kesi ya UDA


Na mwandishi wetu
MKURUGENZI wa Mashitaka (DPP), Dk. Eliezer Feleshi, amewasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea
kuwashitaki Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la UDA, Idd Simba na wenzake.
Simba, aliyewahi kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mkurugenzi wa shirika hilo, Salim Mwaking'inda,
Meneja Mkuu wa UDA, Victor Milanzi na Mkurugenzi wa Kampuni ya Simon Group Ltd, Simon Kisena, walikuwa wakishitakiwa kwa shitaka la uhujumu uchumi.
Kutokana na hatua hiyo ya DPP, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Ilvin Mugeta,
aliifuta kesi ya uhujumu uchumi namba 3/2013, iliyokuwa ikiwakabili washitakiwa hao.
Awali, Wakili wa Serikali Awamu Mbagwa, alidai kesi hiyo ilipagwa jana ili upande wa Jamhuri uwasomee
maelezo ya awali washitakiwa, lakini kutokana na hati ya DPP ya kutokuwa tayari kuendelea na
kesi dhidi ya washitakiwa hawawezi kufanya hivyo.
Wakili Alex Mgongolwa, anayemtetea Simba, alidai upande wa utetezi hauna pingamizi kuhusu hati hiyo,
lakini upande wa Jamhuri usiwasumbue tena wateja wao.
Hakimu Mugeta alisema kwa kuwa kesi hiyo ni ya jinai iliyofunguliwa na Jamhuri na imewasilisha hati ya
kutokuendelea kuwashitaki washitakiwa, mahakama haina mamlaka ya kupingana na hati hiyo.
“Kutokana na hilo, nawafutia kesi hiyo ya uhujumu uchumi  washitakiwa wote,” alisema.
Upande wa Jamhuri Aprili 30, mwaka huu, uliifuta kesi ya awali, ambayo walishitakiwa kwa matumizi
mabaya ya madaraka.
Kesi hiyo ilikuwa ikimkabili Simba, Mwaking'inda na Milanzi. 
Baadaye ilifungua kesi mpya, washitakiwa wakikabiliwa na mashitaka sita, yakiwemo ya rushwa na
uhujumu uchumi, ambapo Kisena aliunganishwa.
Katika shitaka la kwanza la kula njama, Simba, Milanzi na Kisena walikuwa wakidaiwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, jijini Dar es Salaam, walikula njama za kutenda kosa la vitendo vya rushwa.
Kisena katika shitaka la pili alidaiwa kujihusisha na vitendo vya rushwa. Hata hivyo, halikusomwa
kutokana na mshitakiwa kutokuwepo mahakamani.
Shitaka la tatu liliwahusu Simba na Milanzi waliodaiwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, walipokea sh. milioni 320 kutoka kwa Kisena, zikiwa ni ushawishi wa kuiuzia Simon Group hisa za UDA, ambazo zilikuwa hazijagawiwa.
Simba, Mwaking’inda na Milanzi katika shitaka la nne, walishitakiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka.

Mbowe, Lema wasakwa na polisi

SHAABAN MDOE NA LILIAN JOEL, ARUSHA
JESHI la Polisi limemwamuru Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe na mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, kujisalimisha kutokana na vurugu zilizotokea juzi jijini Arusha.
Pia limewaonya watu waliowapa hifadhi kuwa wakiendelea kuwaficha na wakibainika watachukuliwa hatua za kisheria.
Onyo hilo lilitolewa jana na Mkuu wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Kamishna Paul Chagonja.
Alisema ni lazima wajisalimishe polisi ili watoa ushahidi kuwa, askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) ndio waliolipua bomu kwenye mkutano wa hadhara wa CHADEMA Jumamosi iliyopita, eneo la Soweto, jijini Arusha.
Chagonja anayeongoza timu ya wapepelezi kutoka Makao Makuu ya Polisi, alisema iwapo Mbowe anaona hatatendewa haki, anapaswa kuwasilisha ushahidi huo kwa viongozi wa dini au kwa Rais Jakaya Kikwete, ili kurahisisha kazi ya kuwatia mbaroni wahusika.
Mbowe na Lema wamejificha tangu juzi walipotimua mbio wakati wabunge wenzao wakitiwa mbaroni kwa kosa la kukusanyika bila kibali.
Wabunge waliokamatwa ni Tundu Lissu (Singida Mashariki), Mustapha Akonaay (Mbulu), Saidi Arfi (Mpanda Mjini) na Joyce Mukya (Viti Maalumu), ambao jana walishindwa kupandishwa kizimbani kutokana na kutokamilika kwa jalada la kesi.
Watuhumiwa hao na wafuasi 67 wa CHADEMA walitiwa mbaroni juzi na jana waliachiwa kwa dhamana, ambapo huenda wakapanda kizimbani leo.
Katika tukio la juzi, polisi walitumia mabomu ya machozi kuwatawanya wafuasi na viongozi wa chama hicho waliokusanyika viwanja vya Soweto. Pia baiskeli 16, pikipiki 106 na magari sita, likiwemo linalotumiwa na Mbowe yanashikiliwa polisi.
Kamishna Chagonja alisema ni vyema wakatii sheria kwa kujisalimisha mikononi mwa polisi, badala ya kusubiri jeshi litumie nguvu kuwakamata.
Alisema hali ya amani imerejea jijini Arusha, ambapo wananchi wanaendelea na shughuli za uzalishajimali.
Kamishna Chagonja aliwataka wananchi kupuuza vitisho vinavyotolewa na wafuasi wa chama hicho, kwani polisi wapo kwa ajili ya kulinda raia na mali zao.

WABUNGE KUADHIBIWA
Katika hatua nyingine, wabunge wa CHADEMA wameendelea kutohudhuria vikao vya Bunge bila taarifa au kupewa ruhusa.
Wabunge hao wakiongozwa na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mbowe, hadi jana hawajahudhuria vikao vitatu, huku wenzao wakiendelea kujadili hotuba ya bajeti ya serikali.
Spika wa Bunge, Anne Makinda, amesema hana taarifa za kutokuwepo kwa wabunge hao bungeni.
Mkurugenzi wa Idara za Shughuli za Bunge, John Joel, alisema jana kuwa, hakuna taarifa kuhusu kutokuwepo kwa wabunge hao na kwamba, kwa mujibu wa kanuni ni kosa.
Alisema kutokuwepo kwao kunahesabiwa kuwa utoro na kwamba, licha ya kuwa ni kinyume cha kanuni, lakini kunaathiri mwenendo wa Bunge.
“Kikanuni mbunge akitaka kuondoka ni lazima atoe taarifa kwa spika, ambaye ataangalia iwapo hakutakuwa na athari kwa shughuli za Bunge. Bunge halina taarifa kuhusu kutokuwepo kwao,” alisema.
Hata hivyo, alisema Bunge linaendelea kuweka sawa kanuni ili kuwabana zaidi wabunge na kwamba, watoro wote hawatalipwa posho za vikao.
“Wabunge ambao hawako bungeni bila ruhusa hawatalipwa posho, kwa sababu tunatoa kwa wanaohudhuria vikao,” alisema.

WALIPULIWA KWA UCHOCHEZI
Mbunge wa Nzega, Dk. Khamis Kigwangallah, ameitaka CHADEMA kuacha kufanya siasa za vurugu.
Akichangia hotuba ya bajeti ya serikali bungeni jana, alisema kauli za baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa, wakiwemo CHADEMA, zinaathiri amani na utulivu.
Dk. Kigwangallah alisema siasa ni uchumi na kwamba, kuendelea kuhamasisha vurugu kamwe hakuwezi kuliondoa taifa kwenye umasikini.
“Kauli aliyotoa Mbowe kuwa ana ushahidi kuhusu aliyehusika na tukio la kurusha bomu katika mkutano wake ni tata na inaacha maswali mengi,” alisema.
Alisema ni vyema Mbowe kama ana ushahidi akaupeleka polisi ili ufanyiwe kazi na wahusika wakamatwe, lakini hatua yake ya kukimbia inatia shaka.
“Anapodai ana ushaidi wa video kuhusu tukio hilo, nani alipiga na yeye alikuwa wapi hadi aone uhalifu ukitendeka na akae kimya. Aseme ametumia chombo gani kuwabaini wahusika,” alisema.

WASOMI WAPONDA
Katika hatua nyingine, wasomi nchini wamewashukia wanasiasa na kuwataka kuacha siasa za kiharakati, kwa kuwa mara nyingi zinasababisha vurugu.
Pia wametakiwa kujifunza kuendesha vyama kwa ustaarabu, kuhamasishana kutii sheria na kuviacha vyombo vya usalama kutekeleza wajibu wake bila ya kuingiliwa.
Hata hivyo, serikali kupitia vyombo vya dola imetakiwa ichuke hatua madhubuti ili kudhibiti uvunjifu wa amani.
Mhadhiri wa Skuli ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Mzumbe, Mohammed Bakari, alisema nchi iliamua kufuata siasa ya vyama vingi, hivyo ina wajibu wa kufuata sheria kwa sababu vyama vililetwa na sheria.
"Baadhi ya watu wanaendesha siasa za harakati, ambazo zinaleta vurugu. Kama tumeamua kufuata vyama vingi tuna wajibu wa kufuata sheria kwa sababu vyama vingi viliruhusiwa kwa mujibu wa sheria," alisema.
Bakari alisema demokrasia inatakiwa iambatane na wajibu wa kufuata sheria, hivyo kisitokee kikundi cha watu au mtu yeyote akasababisha uvunjifu wa amani kwa madai ya demokrasia, kwani demokrasia bila sheria ni vurugu.
Naye Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana, alisema matukio yaliyotokea Arusha yanapaswa kuangaliwa kwa upana zaidi.
Alisema jamii inatakiwa kujiuliza kwa nini matukio kama hayo yanajirudia mkoani humo.
Dk. Bana alisema vyama vya siasa vinatakiwa vijifunze kuendesha shughuli kwa njia za kistaarabu na kutii sheria.
Alisema hakuna chama chenye uwezo wa kuchunguza matukio ya kihalifu, ukiwemo wa jinai, hivyo alishauri suala hilo liachwe kwa vyombo husika.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TLP, Dk. Augustine Mrema, aliwataka wanasiasa kuwa makini kwa kauli na matendo yao, kwani yanaweza kulisambaratisha taifa.
Alisema wanasiasa nchini wanatakiwa kuwa makini na baadhi ya vitendo vyao, ambavyo havina tija kwa maendeleo ya taifa.

Ulinzi ziara Obama waimarishwa

 

Na Mwandishi Wetu
ZIKIWA zimebaki wiki mbili kabla ya kuwasili kwa Rais wa Marekani, Barrack Obama, jiji la Dar es Salaam limeanza operesheni kubwa ya usafi ambayo imewakumba wasafisha viatu na wafanyabiashara ndogo ndogo katika maeneo ya Posta Mpya.
Kutokana na operesheni hiyo, zaidi ya watu 20 wamekamatwa baada ya kukutwa wakifanya shughuli zao katika maeneo yasiyoruhusiwa, huku ulinzi ukiimarishwa kwenye maeneo mbalimbali ya jiji hilo.
Kwa upande wa Manispaa ya Ilala, hususan maeneo yanayozunguka eneo la Ikulu, Posta Mpya na Posta ya Zamani na mitaa mbalimbali ya Kata ya Kivukoni, operesheni hiyo ilifanyika jana.
Mgambo wa manispaa, polisi jamii na askari polisi walishirikiana kuwaondoa watu hao hali iliyozua gumzo na manung’uniko miongoni mwa watu.
Rais Obama anatarajiwa kuwasili nchini Julai Mosi, mwaka huu, ikiwa ni ziara yake kwanza Barani Afrika baada ya kuchaguliwa kwa mara ya pili kuwa Rais wa Marekani.
Mbali ya Tanzania, Ras huyo atazitembelea pia nchi za Afrika Kusini na Nigeria.
Wakizungumza na Uhuru jana, baadhi ya wakazi wa Dar es Salaam, walisema wanaamini operesheni hiyo inafanyika kwa ajili ya ujio wa Rais Obama.
Msemaji wa Manispaa ya Ilala Dar es Salaam, Tabu Shaibu, alisema manispaa hiyo iliamua kufanya usafi kwa kuwa suala la uchafu wa mazingira limekuwa kero ya muda mrefu.
Tabu alisema wameona ni muda muafaka wa kuhakikisha wanaimaliza hali hiyo kwa kufanya oparesheni hiyo.
Hata hivyo, alisema ujio wa Rais huyo pia inaweza kuwa moja ya sababu kati ya nyingi.
“Lakini kikubwa tunataka kuiweka Manispaa yetu katika hali ya usafi na usalama,” alisema Tabu.
Alisema usafi kwa mkoa wa Dar es Salaam ni moja ya mambo ambayo Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadiki, aliliagiza kwa watendaji wote kulisimamia.
Alisema mkuu huyo wa Mkoa aliagiza oparesheni hiyo ianzie Manispaa ya Ilala,  kata ya Kivukoni.
Akijibu madai ya baadhi ya wananchi waliodai kuwa oparesheni hiyo inatokana na ujio wa Rais Obama, Tabu alisema si kweli.
Bali alitoa wito kwa wafanya biashara hao kutambua kuwa licha ya kutafuta riziki, wanatakiwa kufanya biashara kwa kufuata utaratibu.
Akizungumzia baadhi ya watu wanaofanya kazi ya kusafisha viatu, alisema wamekuwa na tabia ya kufanya zaidi ya kazi hiyo.
Alisema wapo ambao huuza pombe na biashara nyingine haramu. Alitoa wito kwa wakazi wa jiji hilo badala ya kutoa visingizio.

Vurugu zaathiri utalii Arusha
Na Waandishi Wetu, Arusha
SERIKALI imesema vurugu zilizofanywa mapema wiki hii zikihusisha viongozi na wafuasi wa CHADEMA mkoani hapa, zimeathiri taswira ya utalii nchini na kuyumbisha biashara kwa ujumla.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu, aliyasema hayo jana jijini hapa alipozungumza na waandishi wa habari na kutoa msimamo wa wizara hiyo, kuhusiana na vurugu hizo pamoja na zile za Mei 5, mwaka huu, katika Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasiti.
“Nchi hivi sasa imeyumbishwa na matukio mawili, jambo ambalo linawafanya watalii pamoja na wafanya biashara kushindwa kufanya shughuli zao kama kawaida,” alisema Nyalandu.
Kufuatia matukio hayo, Nyalandu alisema serikali itawachukulia hatua kali za kisheria wale wote walioshiriki katika tukio la ulipuaji wa bomu ambao inadaiwa wamenunuliwa ili wawaue na kuwajeruhi watu wasio na hatia.
“Sote tunajua kuwa tukio la Mei 5, mwaka huu katika Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasiti, lilisababisha pia kuyumba kwa biashara na uingiaji wa watalii nchini.
“Lakini tukiwa tunaendelea kulitafakari hilo, hili nalo linatokea. Sasa hali hii inachangia kuathiri uingiaji wa watalii nchini na kusababisha wafanyabiashara nao kushindwa kuendelea na shughuli zao kama ilivyokuwa imezoeleka,”alisema Nyalandu.

Alisema endapo hali ya utulivu haitatengamaa, wafanyabiashara watashindwa kufanya kazi kwa uhuru pamoja na watalii kushindwa kutembelea mbuga za wanyama na vivutio vingine vya utalii.
Kwa mujibu wa Nyalandu, Tanzania kwa mara ya kwanza imefanikiwa kupokea watalii milioni moja kwa kipindi cha mwaka jana, Kenya wakiwa wanaongoza kwa kuwapokea milioni mbili hadi tatu.
Hata hivyo, alisema matukio kama hayo yanafifisha juhudi za serikali za kuendelea kuutangaza utalii.
Alisema tayari nchi ya Italia imeshaahirisha safari za kitalii ambapo watalii wengi toka nchini humo hutembela kwa wingi visiwa vya Zanzibar.
Aidha, alisema mwaka jana zaidi ya watalii milioni 2.4 walitembelea katika hifadhi za taifa.
Nyalandu alihadharisha kuwa, endapo matukio yenye sura ya kigaidi yataendelea kutokea nchini, mapto ya utalii yatashuka kwa asilimia kubwa na hivyo, kuathiri uchumi wa nchi.
Wakati huo huo, Naibu waziri huyo alisema  ziara ya Rais Barrack Obama ipo pale pale na atatembelea moja ya hifadhi za taifa ambayo hakuitaja.

Mji wa Biharamulo kuwa halmashauri
MCHAKATO wa kuufanya mji wa Biharamulo, mkoani Kagera,  kuwa halmashauri ya mji mdogo unatarajiwa kukamilika Novemba, mwaka huu.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Aggrey Mwanri, alisema hayo alipojibu swali la Dk. Anthony Mbassa (Biharamulo -CHADEMA), aliyetaka kujua ni lini mchakato wa kuufanya mji huo kuwa halmashauri utakamilika.
Mwanri alisema mchakato huo utakamilika baada ya Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) wa Kagera kufanya kikao cha mwishoni mwa mwaka huu.
Kwa mujibu wa Mwanri, RCC itakutana kujadili masuala mbalimbali, ambapo moja ya ajenda ni suala la Halmashauri ya Mji wa Biharamulo. 
Alisema mchakato huo ulianza mwaka 2010, kwa kuanza kupima upya eneo la kiutawala, ikiwa ni pamoja na kuanzisha kata mpya mbili ili kufanya idadi kufikia tano kama sheria inavyotaka.
Mwanri alisema suala hilo limechukua muda kutokana na wilaya ya Biharamulo kugawanywa na kuwa wilaya mbili za Biharamulo na Chato.
Naibu waziri alisema kisheria ili mji uweze kuwa na halmashauri unapaswa kuwa na watu 10,000 lakini Biharamulo imevuka kigezo hicho, kwani ina watu takriban 101,000.

Vijiji Mikumi kupata umeme
VIJIJI saba vya jimbo la Mikumi, mkoani Morogoro, vinatarajiwa kupatiwa umeme wa gridi ya taifa katika mwaka ujao wa fedha.
Akijibu swali la Abdulsalaam Ameir (Mikumi -CCM), Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene, alisema katika kuhakikisha azma hiyo inafikiwa, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), linafanya tathmini ili kubaini gharama halisi.

Simbachawene alivitaja vijiji hivyo kuwa, Zoumbe, Lumbe, Kipekenya, Ulaya Mbuyuni, Ulaya Kibaoni, Nakala na Mhenda.
Ameir alitaka kujua ni lini serikali itapeleka umeme katika vijiji hivyo, ili viweze kutumia nishati hiyo kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Kwa mujibu wa Simbachawene, baada ya tathmini serikali itatafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza mradi huo, ikiwemo Mfuko wa Nishati Vijijini.
Hata hivyo, katika swali la nyongeza la Yussuf Nasir (Korogwe Mjini -CCM), aliyetaka kujua kama azma hiyo itatimizwa kwa kuwa vijiji hivyo haviko kwenye awamu ya pili ya Wakala wa Umeme Vijijini (REA), naibu waziri alisema vitaingizwa katika awamu ya tatu.
Alisema baada ya awamu ya pili, REA inatarajiwa kuanzisha awamu ya tatu, ambayo itajumuisha vijiji vingine, vikiwemo vilivyotajwa na Malolo na Malolo Wasaganza katika jimbo hilo.

Wafanyabiashara walanguzi kukiona

SULUHU ya kudumu juu ya ulanguzi wa wafanyabiashara wanaonunua mazao ya wakulima kwa ujazo uliozidi kipimo (lumbesa), itapatikana hivi karibuni baada ya serikali kuanzisha sheria ili kuwadhibiti.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Gregory Teu, alisema jana kuwa, chini ya sheria itakayowasilishwa katika mkutano ujao wa Bunge, watakaoendelea na tabia hiyo watapata adhabu kali.
Teu alisema hayo alipojibu swali la Mchungaji Luckson Mwanjale (Mbeya Vijijini -CCM), aliyehoji serikali inatoa tamko gani juu ya wizi huo, unaofanywa na wafanyabiashara.
Alisema wananchi wamekuwa wakiendelea kuwa masikini kutokana na kuuza mazao kwa mtindo wa lumbesa, hivyo serikali imeamua kutunga sheria kali itakayowabana wafanyabiashara.
“Naomba niwaeleze wakulima na wafanyabiashara kuwa, hakuna sheria inayowataka wakulima kupima mazao kwenye lumbesa. Nawaagiza wafanyabiashara kuacha mara moja mtindo huo wa kuwashurutisha wakulima kutumia lumbesa,” alisema.
Kuhusu kukithiri tabia hiyo, Teu alisema kunatokana na adhabu ndogo wanayopewa wafanyabiashara hao ya faini ya sh. 10,000 wanapobainika kufanya hivyo.
Alisema chini ya sheria mpya, serikali imeazimia wanaoendekeza tabia hiyo watatozwa faini ya sh. milioni 100 ama kifungo cha miaka mitatu jela au vyote kwa pamoja.
“Kwa atakayefanya hivyo kwa mara ya pili atatozwa faini ya sh. milioni 200 ama kifungo cha miaka saba jela au vyote kwa pamoja,” alisema.
Alisisitiza wakulima ni lazima waendelee kupima mazao kwa uzito wa kilo 100 kwa gunia,  ambao unatakiwa kisheria na kwamba, anayefanya kinyume cha hapo ajue ni makosa.

Serikali yazionya NGO

SERIKALI imeyaonya mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO), kuacha kueneza propaganda za uchochezi kuhusu utafiti wa madini ya urani katika Wilaya ya Manyoni, mkoani Singida.
Onyo hilo lilitolewa jana,  bungeni mjini hapa, na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele, alipojibu swali la nyongeza la Kapteni John Chiligati (Manyoni Mashariki - CCM).
Chiligati alitaka kujua kauli ya serikali kuhusu NGO zinazopita kueneza ujumbe kwa wananchi kupinga mradi wa uchimbaji urani katika vijiji vya Manyoni na Bahi, mkoani Dodoma.
Masele alisema serikali ina taarifa kuhusu asasi hizo, ambazo zimekuwa zikieneza ujumbe wa chuki kwa wananchi kuwa, watafukuzwa iwapo itagundulika kuna madini katika maeneo hayo.     
Naibu waziri alisema NGO hizo zinafanya propaganda kupitia ufadhili wa baadhi ya mataifa ya nje, ambayo yamekuwa yakiwania uchimbaji wa madini hayo adhimu duniani.
“NGO hizi zinacheza ngoma ambayo inapigwa na mataifa ya nje, ambayo yanawania kupata nafasi ya kupata madini haya yanayogombewa duniani. Hii yote inatokana na ukweli kwamba, urani ni madini ya kimkakati,” alisema.
Kuhusu maendeleo ya utafiti wa madini hayo unaofanywa na kampuni ya URANEX, Masele alisema unaonyesha wilayani Manyoni kuna kiasi kikubwa cha urani kinachofikia ratili milioni 29.
Alisema licha ya kiwango hicho kutosha kuanza shughuli ya uchimbaji, kampuni hiyo inaendelea kufanya utafiti wa kimaabara ili kutenganisha urani katika udongo wa mfinyanzi.
Masele aliwaasa wananchi wa Manyoni kutokuwa na hofu kuwa watafukuzwa kwenye maeneo yao uchimbaji utakapoanza.

KUTOKA BUNGENI DODOMA

Mgogoro wa ardhi Mpendae kutatuliwa

MGOGORO wa ardhi kati ya wananchi wa Mpendae na kambi ya jeshi ya Bavuai, Zanzibar,   unatarajiwa kupatiwa ufumbuzi baada ya serikali kuamua kupima maeneo hayo katika mwaka ujao wa fedha.
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha, alisema jana kuwa, mgogoro huo utamalizwa baada ya kupimwa kwa maeneo ya kambi hiyo ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Nahodha alisema katika upimaji, iwapo itabainika jeshi limechukua eneo la wananchi, wahusika watalipwa fidia na kwa upande mwingine ikijulikana wananchi ndio waliovamia, watalazimika kuondoka.
“Kimsingi serikali haina sababu ya kuwa na mgogoro na wananchi, ndiyo maana imeamua kupima maeneo ya kambi hii ili kuweka wazi mipaka na hatimaye kumaliza tatizo hili,” alisema.
Katika hatua nyingine, Nahodha alisema nchini kuna zaidi ya migogoro 80 inayohusisha wananchi na kambi za jeshi.
Akijibu swali la nyongeza la Ester Bulaya, aliyetaka kujua kuna mpango gani wa kutatua migogoro hiyo, ukiwemo wa kambi ya Kunduchi, Dar es Salaam, waziri alisema serikali imeanza kuipatia ufumbuzi.
Kwa mujibu wa Nahodha, mgogoro wa ardhi wa Kunduchi uko katika hatua nzuri ya kupatiwa ufumbuzi na kwamba, baada ya mkutano wa bunge, atatembelea eneo hilo pamoja na mbunge wa Kawe, Halima Mdee (CHADEMA), kuona namna ya kufikia suluhu.

 

Friday, 1 March 2013

Joketi kutua Tarime kesho

Kupamba uzinduzi wa
kampeni ya unyanyasaji
na mwandishi wetu
MWANAMITINDO nyota nchini, Joketi Mwegelo, anatarajiwa kunogesha uzinduzi wa kampeni ya kupinga unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto kike, unaotarajiwa kufanyika keshokutwa, ambapo shughuli mbalimbali na mada zitatolewa.
Joketi, ambaye anawika katika tasnia mbalimbali nchini ikiwemo urembo, mitindo, muziki na filamu, atashiriki kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo ijulikanayo kama Okoa Mtoto wa Kike Tanzania utakaofanyika katika Kata ya Nyamongo wilayani Tarime, Mara.
Taarifa ya Mkurugenzi wa Kampuni ya Nyumbani Kwanza Media Group iliyoandaa kampeni hiyo, Mossy Magere, imesema kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika na Joketi atawasili wilayani Tarime kesho tayari kwa kushiriki na atatoa mada ya masuala ya ujasiriamali kwa washiriki wa tamasha hilo linalosubiriwa kwa hamu kubwa.
Mossy alisema kuwa mbali na Joketi, wasanii mbalimbali watashiriki kutoa burudani wakiwemo wasanii nyota wa bongo fleva na wale wa asili wanaotamba mkoani Mara.
"Maandalizi yote ya msingi yamekamilika na kinachosubiriwa ni muda wa uzinduzi ufike, Joketi anatarajiwa kuwasili hapa kesho tayari kwa kushiriki nasi. Atapata fursa ya kutoa mafunzo na mbinu za kimaisha kwa washiriki ambao wengi ni wanafunzi wa shule mbalimbali wilayani hapa," alisema Mossy.
Kampeni hiyo ambayo itadumu kwa kipindi cha miezi sita, itazinduliwa rasmi keshokutwa na Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudentia Kabaka, ambaye ameshirikishwa kwa karibu na Kampuni ya Nyumbani Kwanza.
Alisema mchakato wa uundwaji wa klabu za wapinga unyanyasaji katika shule mbalimbali za sekondari wilayani Tarime ambapo kampeni hiyo inaanzia umekamilika na wanafunzi wamevutiwa na kujiunga kwa wingi kwenye klabu hizo ambazo zitakuwa kichocheo cha kuendeleza kampeni hiyo.
Mossy aliongeza kuwa, uundwaji wa klabu hizo unalenga kukiwezesha kizazi cha sasa na kijacho kuwa mstari wa mbele kukataa vitendo vya unyanyasaji.
“Kila jambo jema huanzia ngazi za chini, kwa sasa tunaendelea kuunda klabu za wapinga
unyanyasaji ambazo zitakuwa zikipewa mafunzo na mbinu mbalimbali ili kuwajenga kufahamu madhara wakiwa wangali wadogo shuleni.

Thursday, 6 September 2012

Nape awashukia CHADEMA


NA PETER KATULANDA, MWANZA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimewataka viongozi wa CHADEMA kuheshimu vyombo vya sheria na kuwajibika kisiasa, hasa kutokana na mfululizo wa matukio ya mauaji na kujeruhi watu katika mikutano ya operesheni za chama hicho.
Pia, imevitaka vyama vya siasa na wanasiasa, kujenga utamaduni wa kuheshimu utawala wa sheria, kulinda amani na utulivu uliopo nchini ili tamaa na uchu wa madaraka usiendelee kupoteza maisha ya wananchi.
Wito huo ulitolewa jana na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi CCM Taifa, Nape Nnauye, alipozungumza na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali jijini hapa.
Nape alisema katika operesheni za chama hicho Septemba 2, mwaka huu, mkoani Iringa, zilijitokeza vurugu zilizosababisha kuuawa kwa mwanahabari wa kituo cha televisheni cha Channel Ten, Daudi Mwangosi na kujeruhiwa vibaya kwa askari watatu wa Kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU).
Alisema Chama kimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo hicho cha mwandishi huyo wa habari na kujeruhiwa kwa askari hao.
Nape alisema CCM inachukua nafasi hiyo kutoa pole kwa wafiwa, wanahabari nchini na wote walioguswa na msiba huo na kutoa wito kwa tume zilizoundwa kuchunguza suala hilo, akitaka zichunguze tukio hilo kwa umakini na weledi ili kubaini chanzo cha vurugu hizo na mazingira ya kifo cha Mwangosi.
Hata hivyo, aliomba uchunguzi huo ufanyike kwa muda mfupi ili ukweli uweze kubainika mapema na hatua zinazostahili zichukuliwe bila upendeleo kwa wahusika.

“Unaponyooshea wenzako kidole wawajibike, anza na wewe, matukio haya si mazuri kutokea mara kwa mara kwenye shughuli za chama cha siasa, ni aibu inayohitaji uwajibikaji hata kama ni ya kisiasa,” alisema Nape na kuongeza viongozi wa CHADEMA wana roho ngumu na ujasiri usio wa uwajibikaji.
“Hatutetei upande wowote, tunataka tamaa ya madaraka isipoteze maisha ya watu... CCM imesikitishwa mno na mfululizo wa watu kupoteza maisha au kujeruhiwa katika mikutano na operesheni mbalimbali zinazoendeshwa na CHADEMA nchini, hasa zilizofanyika kwa kukaidi amri halali ya vyombo vya ulinzi na usalama,” alisema.
Katibu huyo aliyataja matukio mengine ambayo CHADEMA imesababisha vurugu na mauaji kuwa pamoja na lile la kuuawa kwa kada wa CCM mkoani Singida na hivi karibuni mkoani Morogoro, ambapo Ally Hassan aliuawa.
“Matukio haya sio mazuri kwa chama cha siasa, kwa nini wanaopoteza maisha ni wengine na siyo wale wanaozianzisha?” alihoji Nape na kuongeza mstaarabu wa siasa angeachana na siasa za kupoteza maisha ya watu, kwani watu hao hawarudi.
Akifafanua, alisema vifo hivyo vimekuwa vikisababishwa na chama hicho kutotii amri halali zilizotolewa kwa mujibu wa sheria na Katiba ya nchi ambayo ni ile ile iliyovipa uhalali vyama vya siasa kuwepo na kuendesha shughuli zake kwa mujibu wa Katiba na si uroho na matakwa ya wanasiasa wake.
Alisema CHADEMA ingesubiri siku chache zilizobaki kabla ya mchakato wa sensa kumalizika ndipo kiendelee na mikutano yake, hivyo mauaji hayo yasingetokea, lakini kimekuwa kikikebehi na kukaidi amri za polisi kwa kauli za ‘tupo tayari kwa lolote’, jambo ambalo ni ishara ya kujiandaa kwa fujo hizo.
Katibu huyo alisema kwamba kwa kuwa CCM inatii amri halali za vyombo vya serikali, ndiyo maana iliahirisha mikutano yake ya hadhara iliyokuwa ifanyike katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo mkoani Kigoma.