Wednesday 16 July 2014

Kimbisa Mwenyekiti Bodi ya Uhuru Media


NA JUMANNE GUDE
KAMATI Kuu ya CCM, imemteua Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma, Alhaj Adam Kimbisa, kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Uhuru Media Group.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Siasa na Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nauye alisema kuwa Kimbisa anachukua nafasi hiyo  iliyoachwa na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahamani Kinana.


Kampuni ya Uhuru Media Group, inachapisha magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani. Pia inamiliki kituo cha redio cha Uhuru FM. 
Kimbisa ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania, ni mwanadiplomasia na mwanasiasa wa muda mrefu ambaye amewahi kushika nafasi mbalimbali kwenye medani hiyo.
Mwaka 2006 hadi 2010 aliwahi kuwa Diwani wa Kivukoni (CCM) na Meya wa Jiji la Dar es Salaa katika kipindi hicho. 
Pia aliwahi kuwa Mjumbe wa NEC kupitia mkoa wa Dodoma kuanzia mwaka 2002 hadi 2012 na mwaka juzi alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa huo. 
Kwa upande wa utumishi wa umma, Alhaji Kimbisa aliwahi kufanya kazi serikalini akiwa Ofisa Mambo ya Nje Mwandamizi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Kwa sasa ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) na Mwenyekiti wa Wabunge wa Bunge hilo kutoka Tanzania. 

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru