Tuesday 22 July 2014

Mabadiliko ya tabianchi kuathiri uzalishaji umeme


Na Greyson Mwase, Morogoro
MABADILIKO ya tabianchi yanachangia kwa kiwango kikubwa kupungua kwa uzalishaji wa umeme unaotokana na vyanzo vya maji, hivyo kukwamisha ukuaji wa uchumi wa nchi, imeelezwa.
Hayo yalisemwa  jana na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Ngosi Mwihava, alipofungua mafunzo  yanayowakutanisha wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Ofisi ya Makamu wa Rais– Mazingira na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam yanayoendelea mjini Morogoro.
Mhandisi Mwihava alisema awali Tanzania ilikuwa inategemea umeme unaozalishwa kwa maj ambao ulikuwa wa gharama nafuu.
Alisema kutokana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi yaliyosababisha kina cha maji kupungua katika mabwawa ya maji, uzalishaji huo umepungua.
Alisema kutokana na hali hiyo serikali imeingia katika gharama kubwa katika uzalishaji wa umeme kwa kutumia  vyanzo vingine, hususan matumizi ya mafuta mazito kuendesha mitambo.
Mhandisi Mwihawa alisema kutokana na mabadiliko hayo yaliyosababisha kupungua  kwa uzalishaji wa umeme, hivyo wananchi wamekuwa wakililalamikia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na serikali kwa ujumla.
Alisema serikali imeweka mikakati ya kubuni vyanzo mbadala ili kuweza kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa umeme wa kutosha.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru