Thursday 3 July 2014

Tangazeni vivutio vya utalii- Nyalandu


NA MWANDISHI WETU
KAMPUNI za utalii nchini, zimetakiwa kutangaza vivutio vya utalii, ndani na nje ya nchi.
Waziri  wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alisema hayo  jijini Arusha,  wakati akifungua mkutano mkuu wa Wamiliki wa Kampuni ya Kusafirisha Watalii (TATO).
Alisema kazi ya kutangaza utalii inapaswa kupewa kipaumbele katika kampuni hizo.
Alizitaka kampuni hizo kuhakikisa zinaongeza kiasi kikubwa cha watalii wanaoingia  nchini, ili kuiingizia serikali fedha nyingi za kigeni na kuachana na kasumba iliyozeeleka ya kupandisha ada ya kiingilio cha katika hifadhi  na vivutio.
Kuhusu kutunza  utalii wa utamaduni,  Nyalandu alizitaka kampuni hizo zinazohusika na kusafirisha watalii  mbugani, kuhakisha zinawapitisha pia katika maeneo ambapo mambo ya utamaduni yanafanyika.
“Msiwe mnawapeleka kwa wanyama pekee,  hao wanawaona kila siku, angalieni maeneo mengine ya kiutamaduni,” alisema.
Alisema kwa sasa wizara yake imejipanga katika kuendelea kuutangaza utalii ndani na nje ya nchi. Nyalandu alisisitiza kuwa mashirika makubwa ya utangazaji, likiwemo la Uingereza (BBC) na CNN yataingia mkataba na serikali katika kuutangaza utalii wa Tanzania duniani.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TATO, Willy Chambulo, alitoa malalamiko yake kwa serikali   kwa  kuwepo kwa mageti yasiyo rasmi katika baadhi ya hifadhi.
Sambamba  na hilo, alilalamikia pia ongezeko la kodi ambalo lilikuwa halikutolewa taarifa yoyote, hivyo kuleta usumbufu kwa watalii.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru