Thursday 28 August 2014

CCM yatoa mifuko 100 ujenzi sekondari Nduli


NA ANITA BOMA, IRINGA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa kimetoa msaada wa mifuko 100 ya saruji kukamilisha ujenzi wa shule ya sekondari ya kata ya Nduli.
Ujenzi huo ulisimama kutokana na wananchi kuhamasishwa kutochangia ujenzi wake na kusababisha wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata shule.
Akipokea msaada huo kutoka kwa Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa,  Hassan Mtenga, Katibu wa Kata wa Nduli, Petro Mpogole, alisema utafanikisha kukamilisha ujenzi wa sekondari hiyo ambao ulianza mwaka 2010.
“Agosti 23 Katika sherehe za kumsimika Kamanda wa UVCCM Mkoa Salim Abri, Katibu wa CCM Mkoa aliahaidi kutoa mifuko 100 ya saruji ili kukamilisha ujenzi wa shule ya sekondari ya Nduli na leo ametimiza ahadi yake,” alisema.
Kwa mujibu wa katibu huyo, wanafunzi wamekuwa wakilazimika kwenda Kihesa, Lugalo na hata shule ya sekondari Miyomboni.
Naye Diwani wa kata hiyo, Bashiri Mtove, alisema ujenzi wa shule hiyo ulikwama kutokana na mambo ya kisiasa ambapo baadhi ya wanasiasa walikuwa wakiwahamasisha wananchi kutochangia.
Mtove alisema msaada huo ni moja ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kwamba  utafanikisha ujenzi huo kwa kiwango kikubwa.
Kwa upande wake, Meya wa Manispaa ya Iringa, Amani Mwamwindi, aliwashukuru Katibu na Diwani kwa jitihada walizofanya katika kukwamua ujenzi huo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru