Thursday 28 August 2014

Waaswa kufuga nyuki kwa manufaa yao


WANANCHI mkoani Morogoro wametakiwa kufuga nyuki kwa njia ya kisasa ili kuongeza uzalishaji, kuinua kipato na kujitengenezea fursa za ajira.
Hayo yalibainishwa jana na mtaalamu wa ufugaji nyuki  kutoka asasi ambazo zinafuga nyuki kwa njia ya kisasa katika Tarafa ya Turiani wilaya ya Mvomero, Baiton Mshani, alipozungumza na waandishi wa habari mjini hapa.
Alisema ufugaji nyuki unaweza kutoa ajira kwa vijana wengi na kuondoa dhana potofu ya kusubiri ajira toka serikalini iliyojenga kwa Watanzania wengi hivi sasa.
Alisema iwapo mtu atakuwa na mzinga mmoja wa nyuki wanaofugwa kisasa anaweza kuingiza hadi sh.300,000 kila mwezi.
Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, wananchi wanapaswa kutambua faida zitokanazo na ufugaji nyuki ambazo ni pamoja na kupata asali, nta gundi.
Aidha, alisema nyuki pia wanasaidia kustawisha mimea  jambo ambalo husaidian kustawisha na kuongeza mazao ya kilimo.
Hata hivyo, alisema changamoto iliyopo sasa ni ukosefu wa vifungashio ambapo aliiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuusaidia kila mikoa ili iwe rahisi kutekeleza kazi hiyo.
Mshani alisema kwa sasa vifungashio hivyo hulazimika kufuatwa mkoani Arusha jambo ambalo huongeza gharama za uzalishaji asali.
Alisema serikali imekuwa ikitilia mkazo ufugaji nyuki kwa ajili ya kutunza mazingira mbalimbali na kuhamashisha wananchi kutumia asali kwenye maisha ya kila siku.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru