Monday 15 June 2015

 ‘Fanyeni uamuzi sahihi
 uchaguzi mkuu Oktoba’

WAKATI Taifa likielekea katika uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani, Watanzania wametakiwa kufanya uamuzi sahihi, ili kuwapata viongozi watakaowaletea maendeleo.
Pia  wametakiwa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika katika daftari la kudumu la wapigakura, ili watumie haki yao ya kikatiba kuwachagua viongozi wanaowataka.
Wito huo ulitolewa juzi na Askofu wa Jimbo la Shinyanga,  Liberatus Sangu, katika sherehe ya Jubilee ya miaka 55 ya Padri Paul Fagani, wa  Parokia ya Kanisa Katoliki la  Mt. Petro Songambele Nkololo, wilayani Bariadi, mkoani Simiyu, iliyofanyikia kanisani hapo.
Askofu Sangu alisema katika kipindi hiki, Watanzania hawana budi kuchunguza kwa makini na kufanya uamuzi sahihi, ili kuwapata viongozi watakaotumikia taifa kwa uadilifu na weledi.
Mbali na hilo, askofu huyo  aliwataka waumini wa dini hiyo kupiga vita mauji ya vikongwe pamoja na watu wenye ulemavu wa ngozi, huku akibainisha kuwa dini hiyo haikubalini na jambo la binadamu kumtoa roho mwenzake.

Katika Jubilee hiyo iliyohudhuriwa na mamia ya wakazi wa Wilaya ya Bariadi, Padri Paul Fagani, alihitimiza  miaka 55 ya upadri, tangu alipopata daraja hilo nchini Marekani, ambapo mwaka 1960 alikuja Tanzania na kuanzishwa  Parokia ya Buhangija Shinganya kama Paroko Msaidizi na mwaka 2007 alianzisha Parokia hiyo ya Mtakatifu. Petro Songambele Nkololo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru