Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Friday 28 February 2014

GAZETI LAKO HILI LIKO MTAANI -PATA NAKALA YAKO



CCM moto Kalenga


NA MWANDISHI WETU, KALENGA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), jana kilizindua kwa kishindo kampeni zake za ubunge katika Jimbo la Kalenda, Iringa,  kwa kumnadi mgombea wake, Godfrey Mgimwa, ambapo maelfu ya wananchi walihudhuria.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM (Bara), Mwigulu Nchemba, akimnadi mgombea wa CCM katika uchaguzi mdogo wa ubunge jimbo la Kalenga, Godfrey Mgimwa, wakati wa uzinduzi wa kampeni za CCM, uliofanyika jana, uwanja wa Chuo cha Ifunda, Iringa . (Picha na Bashir Nkoromo). 

Katika uzinduzi huo ambao ulitawaliwa na shangwe, nderemo na vifijo huku wananchi wakieleza bayana kuwa watampigia kura Mgimwa siku ya upigaji kura kwa kuwa sera zake zimekuwa na matumiani makubwa.
Naibu Katibu wa CCM (Bara), Mwigulu Nchemba, aliwaeleza kamwe wasidanganywe na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, kwa kuwa ana mapepo.
Mwigulu ambaye alikonga nyoyo za wananchi wa Kalenga, alisema baada ya Dk. Slaa kuacha kumtumikia Mungu, kwa sasa mawazo na mtazamo wake vimejikita katika kusema uongo na uzushi licha ya kuwa mtu mzima.
Akizungumza katika kijiji cha Ifunda,  wakati akizindua kampeni hizo, alisema CCM imemsimamisha mgombea makini na kijana mwenye uwezo wa kuwaletea wananchi maendeleo.
“Kwa sasa Dk. Slaa ana miaka 70, lakini ana mchumba na kichwa chake kimekuwa kikisema mambo ya uongo na kuhamasisha maandamano,’’ alisema Mwigulu huku akishangiliwa.
Pia alisema iwapo atatakiwa kumtaja mtu mmoja kati ya ambao hawaheshimu basi atamtaja Dk. Slaa na hilo linatokana na tabia zake za kusema uongo kwenye majukwaa ya kisiasa.
Alisema kuhangaika huko kwa Dk. Slaa, kunatokana na kulipwa mamilioni ya shilingi ambazo CHADEMA wanapewa kama sehemu ya ruzuku hivyo, ni lazima apige domo.
Aliwaasa wananchi wa Kalenga kumchagua Mgimwa kwa kuwa CCM ndiyo yenye Ilani inayotekelezwa tofauti na wapinzani ambao kazi kubwa ni kuhamasisha vurugu.
“Tunahitaji maendeleo ya wananchi wa Kalenga. Tumchague Mgimwa na tuachane na hawa wapiga kelele wakiongozwa na babu (Dk. Slaa), ambaye anahangaika kutafuta kula yake,’’ alisema.
Alisema kuwa ilani ya inayotekelezwa sasa ni ya CCM na upinzani hauna wanachotekeleza na hata kusimamia mgombea wao ni ushamba wa siasa.
“Kinachoendelea sasa ni kutekeleza maendeleo kupitia Ilani ya CCM ambayo wanayoimiliki ni wa CCM,” alisema.
Alisema umefika wakati kwa wananchi kumtuma kijana wao Mgimwa ili akafanye kazi ya kuleta maendeleo yao na si kuchagua mbunge kwa sababu tu ya kuchagua.
Mwigulu aliwaomba, wananchi kuacha ushabiki katika mambo ya maendeleo, hivyo hawatakiwi kufanya kosa kwa kumchagua mtu ambaye anatoka nje ya CCM.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Njombe, Pindi Chana, alisema wananchi wanahitaji maendeleo na si maandamano.
Alisema anashangazwa na CHADEMA kushindwa kutatua matatizo ya wananchi na badala yake wanazunguka hewani kwa helkopta wakati wananchi wako chini.
Akizungumza katika mkutano huo, Chifu wa Kabila la Wahehe, Abdul Mkwawa, alisema kuwa kamwe hawezi kuwa CHADEMA na wanaozusha kuwa amemkaribisha Dk. Slaa wanajisumbua.
Alisema kuwa yeye ni kada wa CCM na ataendelea hovyo na kwamba damu yake ni CCM.
“Siwezi kuwa CHADEMA, wamezusha hadi kwenye mitandao eti nimemkaribisha Dk. Slaa Kalenga na wanadai mimi ni CHADEMA. Si kweli kwanza huyo Dk. Slaa wa kazi gani huku kwetu,” alisema.
Nape acharuka, atoa
angalizo kwa Mangu
SIKU mbili baada ya kutangaza kujiunga na CCM, waliokuwa madiwani wawili wa CHADEMA katika Manispaa ya Shinyanga, wameanza kutishiwa maisha.
Hatua hiyo imetokana na kile kilichoelezwa hasira za baadhi ya viongozi kuchukizwa na uamuzi wa madiwani hao, Sebastian Peter (Ngokolo) na Zacharia Mfuko (Masekelo), ambao walijiuzulu nyadhifa hizo kutokana na chama hicho kukosa mwelekeo na dhamira ya dhati ya kuwatumikia watanzania.
Wakizungunza juzi wakati wakitambulishwa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Mahakama mjini Shinyanga, walisema wamekuwa wakipokea simu na kauli za vitisho kutokana kwa baadhi ya viongozi na wafuasi wa CHADEMA.
Walisema uamuzi wa kujiondoa CHADEMA na kujiunga na CCM umelenga kupata fursa ya kuwatumia wananchi na kamwe hawatakaa wajutie.
Kutokana na vitisho hivyo, Katibu wa NEC ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, ambaye aliwatambulisha rasmi kwenye mkutano huo, amemtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Ernest Mangu, kuchukua hatua kwa wahusika wote.
Pia alisema vitisho wanavyopewa makada wake hao ni ishara kuwa CHADEMA kimezoea kutesa wanachama wanaokihama hivyo, hatua za haraka zinapaswa kuchukuliwa ili kuwalinda.
Akizungumza kwenye mkutano huo uliohudhuriwa na umati mkubwa, Nape alilitaka jeshi la polisi kuwapa ulinzi na kufuatilia viongozi wa chama hicho wanaowatishia maisha.
‘’Wametoka CHADEMA kwenye mavurugu wamerejea nyumbani kwa ajili ya kuungana na viongozi makini ndani ya CCM na serikali yake ili kuwatumikia watanzania. Sasa wameanza kutishiwa maisha, naomuomba IGP Mangu afanyie kazi taarifa hizo na kuwapa ulinzi hawa makada wetu. Hii ni tahadhari na kamwe hatukubali iwapo watadhurika kwa namna yoyote ile. Tutaanza na polisi kisha tutamaliza na waliowadhuru,’’ alisema Nape huku akishangiliwa na umati wa wananchi.
Alisema limekuwa jambo la kawaida kwa wanachama wa CHADEMA wanaopenda mabadiliko kuitwa majina ya wasaliti au wahaini pamoja na kuwasukia mizengwe kutokana na kutokuwepo kwa demokrasia.
Alisema kuna wanasiasa waliojaribu kutaka kufanya mabadiliko ya kuigeuza CHADEMA kutoka kuwa taasisi ya kifamilia na kuwa chama cha siasa, lakini wamekwama kutokana na mizengwe na wengine wamefukuzwa.
“Chama halisi na makini kwa maslahi ya watanzania ni CCM, ndio sababu hawa wenzetu wamerudi nyumbani. Milango iko wazi kwa wengine kurejea CCM kwa sababu wenzetu wana taasisi ya kifamilia si chama cha siasa,’’ alisema Nape.

Kampuni za simu mtegoni

NA MOHAMMED ISSA
RAIS Jakaya Kikwete amezindua mtambo utakaodhibiti mapato ya kampuni za simu nchini hivyo kuiwezesha serikali kukusanya mapato yake kwa ufanisi.
Pia ameiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuhakikisha wanadhibiti mawasiliano ya ndani na sehemu zingine za serikali.
RAIS Jakaya Kikwete

Amesema kuanzia sasa ni lazima kuwepo kwa sheria maalumu za mitandao zitakazowezesha nchi kuwa salama kupitia mitandao hiyo.
Rais Kikwete alisema hayo jana Dar es Salaam, alipozindua mtambo huo, ambao pia utahakiki mawasiliano ya simu za nje ya nchi.
 Alisema mtambo huo utaiwezesha serikali kupata mapato yake kwa uhalali na kwamba katika mwaka itakusanya wastani wa sh. bilioni 20.
“Kabla ya mtambo huu, kampuni za simu zilikuwa zinakadiria mapato na kuleta serikalini lakini sasa tutaweza kukusanya fedha nyingi zaidi. Mtambo huu utawezesha kufahamu kila kampuni inapiga simu ngapi na wanapata kiasi gani hivyo itakuwa rahisi kwa serikali nayo kupata mapato yake kwa utaratibu unaostahili,” alisema.
Alisema serikali imeamua kuwekeza kwenye sekta ya mawasiliano kwa sababu ni kichecheo muhimu cha uchumi wa nchi.
Rais Kikwete alisema kwenye sekta ya mawasiliano TCRA inafanya vizuri na kwamba serikali inaridhishwa na namna inavyofanya kazi zake.
“Kufanya kazi na watu kama ninyi inaleta raha sana, mko tofauti na wenzenu ambao unatoa maagizo wanasema tuko kwenye mchakato au tuko mbioni,” alisema.
Rais alisema gharama za upigaji simu zimepungua kwa asilimia 57 na huduma za intaneti zimepungua kwa asilimia 75.
Kiongozi huyo mkuu wa nchi, alisema gharama za upigaji simu zimepungua kwa asilimia 99 na kwamba zimechangiwa na kuwepo kwa mkongo wa taifa wa mawasiliano.
“Ni jambo la kujivunia kuona Tanzania inafanya vizuri kwenye sekta ya mawasiliano kwa Afrika ni ya tatu,” alisema.
Kwa upande wake, Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, alisema watumiaji wa simu wameongezeka kutoka milioni tatu mwaka 2005 hadi milioni 27 mwaka jana.
Alisema mtambo huo una faida kuu tano ikiwemo ya kufahamu mapato yatokanayo na simu za kimataifa, kuzuia matumizi ya simu bila ya leseni na kudhibiti matumizi ya simu zisizo halali.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma, alisema sekta ya mawasiliano nchini inaendelea kukua kwa haraka na kwamba hivi sasa kuna laini za simu milioni 28, vituo vya radio 84 na televisheni 27.
Alisema mtambo huo unauwezo wa kuzuia matumizi ya simu kwa kampuni zisizo na leseni.
Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TCRA, Mhandisi Salmin Salmin, alisema mtambo huo unaboreshwa na kuendeleza huduma za watumiaji.

Kiama cha majangili


NA MWANDISHI WETU
SERIKALI imeendelea na dhamira yake ya kutokomeza ujangili wa wanyama na nyara zao, baada ya ‘kushusha’ bunduku 500 aina ya AK 47, imeelezwa.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, akizindua moja ya magari yatakayotumika kukabiliana na vitendo vya 
ujangili katika mbuga za wanyama, mjini Dar es Salaam, jana.


Pia imeligawanya pori la akiba la Selous lenye ukubwa wa kilomita za mraba 55,000 kwa kuzipandisha hadhi kanda nane ili ziweze kujitegemea kiuendeshaji.
Hayo yalisema jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, wakati akikabidhi magari maalumu yatakayosaidia kukabiliana na ujangili kwenye hifadhi na mapori ya akiba nchini.
Nyalandu alisema katika kutekeleza maazimio ya Bunge na ahadi zake  kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maliasili, Ardhi na Mazingira, serikali imekamilisha utaratibu wa kuzitoa bunduki zilizokuwa chini ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) tangu Novemba 2012.
Bunduki hizo zilikuwa zinashikiliwa na TRA kutokana na kutolipiwa kodi na kuwa tayari wizara imetoa sh. milioni 212 kwa ajili ya kodi na ushuru. Bunduki hizo zimegharimu sh. milioni 427.
Waziri Nyalandu ambaye tangu kuteuliwa kwake kushika wadhifa huo hivi karibuni na kuanza kufanya mabadiliko ya kuimarisha wizara hiyo, alisema bunduki hizo zitagawiwa kwa wapiganaji katika hifadhi za taifa, Mamlaka ya Ngorongoro, mapori yote ya akiba kwa lengo la kupambana na ujangili.
Katika hatua nyingine, Nyalandu alisema amezipandisha hadhi kanda nane zilizopo katika Pori la Akiba la Selou ili ziweze kujitegemea kiuendeshaji.
Alisema kanda hizo zitakuwa chini ya Meneja wa Poli lote la Selou, Benson Kibonde, ambaye atasaidiwa na wakuu wa kanda na kanda zao kwenye mabano ambao ni Msafiri Mashiku (Matambwe), Asterius Ndunguru (Msolwa), Adili Zella (Liwale), Bigilamungu Kagoma (Kingupira), William Mallya (Kalulu), Munhu Ndunguru (Miguruwe), Ramadhani Mkhofoy (Ilonga) na Msiba Kombo (Likuyu-Sekamaganga).
Mbali na wakuu hao, Nyalandu alisema wameimarisha Kikosi Dhidi ya Ujangili (KDU) kitakachotekeleza majukumu yake kwenye kanda nane kuu na kuwataja wakuu na kanda zao kwenye mabano kuwa ni: Paschal  Mrina (Kaskazini-Arusha), Faustine Masalu (Mashariki - Dar es Salaam), John Mbwilizi (Serengeti - Bunda), Benjamin Kijija (Ziwa - Mwanza), Charles Msilanga (Magharibi - Tabora), Keneth Sanga (Kati - Manyoni), Majid Lalu (Juu Kusini - Iringa) na Abeid Mmari (Kusini- Songea).
Katika hatua nyingine, Nyalandu alisema kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa tembo na mapambano dhidi ya ujangili wamepokea magari matano aina ya Land Rover ambayo yamegawiwa kwenye kanda za Matambawe, Msolwa, Kiwale, Kingupira na Kalulu.
Mbali na magari hayo yaliyotolewa na washirika, Mfuko wa Wanyamapori umenunua magari 14 aina ya Toyota yenye thamani ya sh. bilioni 1.6 ambayo yamegawanywa katika maeneo mbalimbali.
Mgawanyo wa magari hayo ni mawili katika Pori la Akiba la Rungwa na mengine ni moja moja katika mapori ya akiba ya  Selous kanda ya Sekamaganga, Uwanda, Lukwati - PITI, Kijereshi, Rukwa - LWAFI, Burigi-Biharamulo-Kimisi, Lukwika-Lumesule -Msanjesi, Moyowosi-Kigosi, Maswa, Mkungunero, Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori ya Pasiansi na Mfuko wa Kuhifadhi Wanyamapori (TWPF),
Mabadiliko mengine yaliyofanywa na Nyalandu ni kumteua Nurdin Chamuya kuwa msemaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii kuchuku anafasi ya Chikambi Rumisha, ambaye anarudi katika Idara ya Sera na Mipango.
Kuhusu mapambano dhidi ya ujangili na hatua ambazo serikali inazichukua, Nyalandu alisema vita dhidi ya vitendo hivyo, inahitaji ushirikiano wa Watanzania wote na kwamba serikali itaendelea kuwa mstari wa mbele kuhakikisha maliasili za taifa zinakuwa salama.
Pia alitumia fursa hiyo kuwaeleza watumishi na watendaji wa wizara yake kuwa wanapaswa kushiriki kikamilifu na kuwa waadilifu katika kutekeleza majukumu yao na kwamba, mabadiliko yanayoendelea kufanyika kwa sasa yanalenga kuongeza ufanisi.
‘’Watanzania wanatuangalia sisi watendaji tuliopewa jukumu kubwa la kulinda maliasili za taifa tunafanya nini, tunapaswa kuwa waadilifu ili kujenga imani na kuwahamasisha kuwa walinzi wa maliasili. Kama mtu tutamuona hayuko pamoja nasi tutambadili mara moja ili tuweze kusonga mbele,’’ alisema Nyalandu.

Thursday 20 February 2014

Nyongeza ya posho yazusha mjadala mkali

  • Bunge launda kamati kuivaa serikali
  • Wananchi wawajia juu, wadai ni walafi
  • Zitto: JK wapuuze wanaodai nyongeza

Na waandishi wetu, Dodoma na Dar

SAKATA la wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kudai nyongeza ya posho limeingia hatua mpya baada ya kuundwa kamati ili kufuatilia suala hilo.
Mwenyekiti wa Muda wa Bunge hilo, Pandu Ameir Kificho, ameunda kamati ya watu sita kufuatilia posho hizo.
Kificho, ambaye pia ni Spika wa Baraza la Wawakilishi, alitangaza kamati hiyo jana asubuhi kabla ya kuanza semina maalumu ya wajumbe kuhusu Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Alisema ameunda kamati hiyo baada ya kupata mawazo ya wajumbe kadhaa kuhusu namna nzuri ya kuishi mjini Dodoma kutokana na ugumu wa kazi.

“Wajumbe, mawazo mliyoyatoa kuhusu jinsi gani tutaweza kuishi hapa na kuifanya kazi hii nimeyachukua lakini bado sijawa na jibu.
“Ili kuwa na majibu, nimeona ni vyema nikaunda kamati ya watu sita ili kwa pamoja tuone ni namna gani nzuri ya kuishauri serikali tuweze kufanya kazi kwa ufasaha tukiwa hapa Dodoma,’’ alisema.
Kificho aliwataja wajumbe wa kamati kuwa, William Lukuvi, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge).
Baada ya kutajwa jina la Lukuvi, baadhi ya wajumbe walizomea wakiashiria kutoridhika na uteuzi wake.
Hata hivyo, Kificho alisema Lukuvi hatafanya kazi peke yake na kwamba, ipo siku wajumbe hao watapiga kofi juu ya uteuzi wa mjumbe huyo.
Wajumbe wengine ni Mohammed Aboud Mohammed, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar na Freeman Mbowe, ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani katika Bunge la Jamhuri ya Muungano na Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA.
Wamo pia mwanasiasa mkongwe nchini, ambaye amewahi kuwa mbunge na waziri, Paul Kimiti, Asha Bakar Makame na Jenista Mhagama, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
Mwenyekiti aliwataka wajumbe wa kamati baada ya kumaliza kazi jana wakutane naye ili kujipanga katika timu hiyo itakayowashirikisha pia makatibu wa Bunge la Muungano na Baraza la Wawakilishi.
Kificho alisema anaamini watapata jibu litakalosaidia kupata suluhu.

Jukwaa la Katiba lawaponda
Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA), limelaani madai hayo yaliyotolewa na baadhi ya wabunge ya kutaka nyongeza na kusema sh. 300,000 wanazolipwa zinakidhi mahitaji.
Kaimu Mwenyekiti wa JUKUTA, Hebron Mwakagenda, alisema jana kuwa wabunge wanapaswa kuweka mbele maslahi ya taifa badala ya kujali matumbo.
Pia, alionya wabunge kuacha kulitumia Bunge la Katiba kama sehemu ya kujitajirisha kwa kutumia kodi za wananchi ambazo zinahitaji pia kutumika kwenye maendeleo ya taifa.
“Madai ya nyongeza ya posho yanaonyesha jinsi baadhi ya wabunge hawako makini na kazi waliyopewa na umma. Hawana uzalendo na nia ya dhati ya kuwapatia
Watanzania Katiba bora na yenye tija,’’ alisema.

Zitto: JK awapuuze wabunge

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, amemuomba Rais Jakaya Kikwete kuwapuuza wabunge kwa kukataa maombi ya kuongezewa posho kwani kilichopangwa na serikali kinatosha.
Pia, aliwataka wabunge wenzake kuacha kutanguliza mbele maslahi binafsi na badala yake waweke utaifa mbele ili kutimiza malengo ya wananchi.

“Namuomba rais asikubali kuongeza posho kama ilivyoombwa na baadhi ya wabunge. Binafsi sitapokea ongezeko lolote la posho licha ya kwamba uamuzi huu usisaidie kuzuia walafi wengine kupata posho kubwa,” alisema Zitto.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga, Mrisho Gambo, aliwashangaa wabunge wanaodai ongezeko la posho.
Alisema wabunge hao wamekuwa wakilipwa posho ya chini ya sh. 300,000 katika vikao vya Bunge la Jamhuri ya Muungano iweje kwenye Bunge la Katiba isitoshe.

“Haya madai ya ajabu kabisa, miaka yote Bunge linafanyika Dodoma na wabunge wanalipwa posho ya chini ya sh. 300,000 na inawatosha, iweje bunge hilo ambalo ni nyeti na la kihistoria watake malipo makubwa,’’ alihoji Gambo.
Mkazi wa Dar es Salaam, John Shayo alisema iwapo wabunge hao wanaona posho wanayolipwa ni ndogo ni vyema wakajiondoa na kutoa fursa kwa wazalendo kwenda kufanya kazi ya kutayarisha katiba.
Alisema walioomba kushiriki kwenye bunge hilo ni wengi, wengine wameachwa kutokana na ufinyu wa nafasi, waliokwenda kwa ajili ya matumbo yao wanaweza kutangaza kujiondoa.

“Serikali ya Rais Kikwete imetoa fursa kwa Watanzania kupata katiba mpya ambayo kwa kiasi fulani itakuwa suluhisho la kero na matatizo, lakini bado itaendelea kutoa huduma za kijamii na maendeleo kwa wananchi.
“Hawa wanataka posho kubwa fedha hizo zitatoka wapi, kama wamekwenda kushibisha matumbo yao wajiondoe,’’ alisema Subira Juma, mkazi wa Kiwalani.
Juzi, baadhi ya wajumbe walizua zogo kuhusu posho, wakidai ni ndogo ikilinganishwa na waliyolipwa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Richard Ndassa, ambaye ni mbunge wa Sumve, alisema posho ya sh. 300,000 wanayolipwa hailingani na hadhi ya kazi wanayoifanya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.
Alisema inashangaza kuona wakilipwa posho ya sh. 220,000, ambayo ni ndogo ikilinganishwa na waliyolipwa madereva wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Wajumbe pia wanalipwa posho ya kujikimu ya sh. 80,000 kwa siku.
Pia, ili kupata posho hiyo, alisema ni lazima mjumbe ahudhurie vikao siku nzima na kwa Jumamosi na Jumapili hawalipwi zaidi ya posho ya kujikimu ya sh. 80,000, huku akilazimika kuwalipa wasaidizi wake, akiwemo dereva.

“Hebu tuangalie wajumbe wa Tume ya Katiba walikuwa wakilipwa sh. 500,000 kwa siku, dereva analipwa sh. 220,000, ambayo ndiyo posho ya siku. Mimi ninahangaika hivi nami nalipwa sh. 220,000,” alisema.
Ndassa pia alidai kuwa wajumbe kutoka Zanzibar wameongezwa posho ya vikao kutoka kwao, hivyo kutengeneza makundi.
Hata hivyo, mjumbe wa bunge hilo, ambaye ni mwakilishi wa Kwahani, Ali Salum Haji, akizungumzia hilo alisema si kweli kuwa wamelipwa ziada.
Kwa upande wake, Seleman Nchambi, alisema posho zinazolipwa kwa wajumbe ni sawa na mishahara ya vibarua wa mashambani.
Nchambi pia alitoa ombi maalumu kwa Mwenyekiti wa Muda Kificho, kuwanunulia wajumbe kitendea kazi cha mawasiliano cha ipadi (IPAD) ili kupunguza matumizi ya karatasi na gharama kwa bunge.
Kificho akijibu hilo, alisema ununuzi wa IPAD pia ni gharama, hivyo Bunge litaendelea kutumia karatasi katika kutoa nyaraka mbalimbali.

CHADEMA yaumbuka Kalenga

  • Mkakati mchafu waliopanga wagonga mwamba, Mgimwa apeta Kalenga
 
Na Tumaini Msowoya Iringa, IRINGA

MCHEZO mchafu na fitina zilizoanza kufanywa na uongozi wa CHADEMA kuihujumu CCM zimegonga mwamba baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kutupilia mbali pingamizi lao.
Walikuwa wakidai kuwa mgombea ubunge katika Jimbo la Kalenga, Godfrey Mgimwa si raia na waliomdhamini si wakazi wa Kalenga.
Harakati hizo ambazo wachunguzi wa masuala ya kisiasa wanadai kuwa ni mwanzo wa chama hicho kuanza kutafuta visingizio, zilisukwa na baadhi ya viongozi kwa kushirikianana na mgombea wa ubunge wa CHADEMA, Grace Tendeka.
Hata hivyo, CHADEMA na mgombea wake wameshindwa kuwasilisha vielelezo kuthibitisha madai hayo, hivyo NEC kuamua kulitupilia mbali pingamizi hilo kwa kuwa halina mashiko.
Akizungumza na Uhuru jana, Msimamizi wa uchaguzi wa jimbo la Kalenga, Pudensiana Kisaka, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, alisema NEC ilitumia muda uliopangwa kisheria kutaka pande zote mbili, kupeleka vielelezo vyake ili kujiridhisha na pingamizi hilo.
“CHADEMA walishindwa kuleta uthibitisho wa pingamizi lao kwa muda uliopangwa, badala yake walipeleka barua ya kusisitiza pingamizi hilo.
“Kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, barua hiyo haikutosha kuthibitisha pingamizi lao la kwamba, Mgimwa sio raia wa Tanzania,” alisema.
Alisema mgombea wa CHADEMA, aliwasilisha pingamizi lake likiwa na vipengele vingi, hivyo ikatumika sheria ya uchaguzi kuwataka mlalamikiwa kuwasilisha utetezi wake haraka iwezekanavyo na mlalamikaji kuwasilisha ushahidi wao ili tume ijiridhishe.
Pingamizi liliwasilishwa ofisini kwake juzi (Jumatano) na upande wa mlalamikiwa ulileta utetezi wao kama walivyoagizwa, huku CHADEMA wakiwasilisha barua. Mpaka jana mchana, hakukuwa na ushahidi kutoka kwa walalamikaji, hivyo Tume ikatoa ruksa ya kampeni kuanza kama ilivyopangwa.
“Hatuwezi kufanyia kazi vitu ambavyo havina ushahidi wa kutosha,” alisema Pudenciana.
Katibu wa CCM wilaya ya Iringa, Amina Imbo, alisema Mgimwa ni raia wa kuzaliwa wa Tanzania na kwamba, pingamizi hilo halina maana na kamwe halitaweza kuvuruga kampeni za Chama hicho.
Amina alisema CCM ilisimamia kikamilifu kuhakikisha fomu za mgombea zinadhaminiwa na wananchi wa jimbo husika ambao waliambatanisha shahada za kupigia kura kutoka jimboni na si vinginevyo.
Alisema kilichofanyika ni kuwapotezea muda wao wa kampeni, kwa kuwa  malalamiko hayo hayana ukweli wowote na kamwe hayataweza kuvuruga jambo lolote.
“Hatutaogopa hata kidogo, CCM ipo makini na mgombea wetu yupo makini, Mgimwa ni mzaliwa wa Tanzania na raia mwenye haki ndani ya nchi yake, ikiwemo haki ya kuchagua na kuchaguliwa kuwa kiongozi,” alisema Amina.
Uhuru iliamua kuwatafuta ndugu wa karibu wa Mgimwa ili kupata ukweli wa maisha ya  Godfrey ambao walidai kushangazwa na madai hayo ambayo hawakuyatarajia.
Baba mdogo wa Godfrey, Joachim Mgimwa, alisema mwanaye ni raia wa Tanzania wa kuzaliwa na sio kuomba.
“Jambo hili ni la ajabu, mwanagu alizaliwa katika hospitali ya Mkoa wa Iringa, baba yake ni mzaliwa wa kijiji cha Magunga wilaya ya Iringa vijijini, mama yake ni mzaliwa wa kijiji cha Kinyanambo ‘B’, wilayani Mufindi, uraia wake sio wa kuomba ni wa kuzaliwa,” alisema.
Alisema baada ya Godfrey kuzaliwa, alipata elimu ya msingi katika shule ya msingi Wilolesi, iliyopo katika Manispaa ya Iringa, baadaye alijiunga na shule ya sekondari ya Njombe (NJOSS) ambako alisoma kwa muda mfupi kabla ya kuhamia Dar es Salaam.
Alisema Godfrey alienda nchini Uingereza kwa ajili ya masomo ya juu na mara zote amekuwa akitumia hati yake ya kusafiria inayoonyesha  yeye ni raia wa Tanzania.
Pia alisema Godfrey anacheti cha kuzaliwa kinachoonyesha kuwa ni raia wa Tanzania.
“Hivi mtu asiye raia anaweza kuwa na cheti cha kuzaliwa? Jambo hili lisiwachanganye wapiga kura wa Kalenga, huyu ni mtoto wa nyumbani mwenye sifa na uwezo wa kuwa mbunge,” alisema Joachim.
Alisema hati yake ya kusafiria ameitumia mpaka mwezi Desemba, mwaka jana wakati akienda nchini Afrika Kusini.
Akizungumza na Uhuru, Godfrey alikiri kuwepo kwa pingamizi dhidi, hata hivyo alisema anashangazwa na jambo hilo kwa kuwa tangu azaliwe hajawahi kuukana uraia wa Tanzania, nchi aliyozaliwa na ambayo anaipenda kwa moyo wake wote.
Alisema ataendelea kusimamia ukweli na kuwataka CHADEMA kutumia muda wao kwa ajili ya kuhangaikia mambo yao badala ya kuchokonoa masuala ambayo hayana msingi.

Membe: Uraia wa nchi mbili uzingatiwe katika Katiba Mpya

Na MUSSA YUSUPH

WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, amesema uraia wa nchi mbili kwenye katiba mpya ni suala muhimu linalohitaji kuwepo kwa manufaa ya Watanzania wote.
Alisema wao kama Wizara, wamejipanga kuhakikisha wanaitetea hoja hiyo pindi itakapojadiliwa kwenye bunge la Katiba linaloendelea na vikao vyake mjini Dodoma.
Membe alisema Watanzania wengi waliopo nje ya nchi wanashindwa kushiriki katika fursa za kimaendeleo nchini kutokana na kuwa na uraia wa nchi zingine, baada ya kuomba huko na kupewa.
Alisema watanzania hao hukataliwa pia kupata huduma za kiupendeleo kama mikopo ya nyumba, fedha na hata huduma za afya kutokana na kukosa uraia kamili wa nchi hizo.

“Tuwasaidie kupata Uraia wa Tanzania na tutapigania, ikiwa mgeni anayeishi nchini kwa muda wa miaka 10 anapewa uraia wa Tanzania. Je kuna tatizo gani Mtanzania mwenye uraia wa nje nayea akapewa uraia,” alihoji Membe.
Alisema wamejipanga kutetea hoja hiyo, ili watanzania wenye uraia wa nchi za nje nao wapate uraia wa Tanzania ili waweze kushiriki katika fursa muhimu za kimaendeleo ndani na nje ya nchi.
Hivyo, alisema kuna umuhimu wa kuandaa utaratibu wa sheria na kanuni za kila mtanzania kupata haki hiyo pasipo kuasili usalama na maendeleo ya nchi.

Pandu, Kamati ya ushauri wakutana

Na Theodos Mgomba, Dodoma

KAMATI iliyoundwa kumshauri Mwenyekiti wa Muda wa Bunge Maalumu la Katiba, Pandu Ameir Kificho, inakutana leo kupitia Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalumu, iliyowasilishwa bungeni jana.
Kificho alisema hayo jana bungeni mjini hapa, alipoahirisha kikao.
Alisema kazi hiyo itafanyika hadi  Jumapili wiki hii.
Mwenyekiti huyo alisema atajiunga na kamati hiyo ili kuangalia ilipofikia katika utendaji na kwamba, itafanya kazi pamoja na makatibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Dk. Thomas Kashililah na wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad.
Kificho alisema lengo la kukutana na kamati hiyo ni kupitia vifungu vya kanuni na kuangalia kama kuna jambo la kuongeza au la.
Alisema Jumatatu kabla ya kuanza  majadiliano kuhusu rasimu ya kanuni hizo, kamati itatoa taarifa kwa wajumbe kuhusu kazi iliyofanyika.

“Kamati itaanza kazi kesho (leo) saa tatu asubuhi, itafanya kazi hadi Jumapili nami nitaungana nao kuona walichofanya.
“Jumatatu kabla ya kuanza majadiliano, mjumbe mmoja wa kamati au wawili watapewa nafasi ya kutuambia nini kimefanyika, na nini kimeongezwa ili tuwe katika njia sahihi wakati tunajadili,’’ alisema.
Mwenyekiti Kificho aliwaasa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuwa waungwana wakati wa kujadili kanuni hizo na pia kuvumiliana wakati mjumbe akitoa  hoja.
Alisema majadiliano yatakayoanza Jumatatu ni mwanzo wa kuelekea katika majadiliano ya kina kuhusu Rasimu ya Katiba.

“Watanzania wanasubiri tuwasaidie kufanya kazi hii, hivyo ili tuweze kuwatendea haki ni muhimu kufanya kazi kwa weledi na urafiki mkubwa,’’ alisema. 
Kificho, juzi aliwateua wajumbe 20 watakaomshauri ili kuleta ufanisi wa utendaji.
Wengi kati ya walioteuliwa ni wataalamu wa sheria, wakiwemo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Kairuki na Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA Tundu Lissu.
Pia wamo Profesa Costa Mahalu na Magdalena Rwebangira, ambao Jumanne wiki hii waligombea nafasi ya mwenyekiti wa muda wa bunge hilo.
Wengine ni Abubakar Khamis Bakari, Mgeni Hassan Juma, Usi Jecha Simae, Ismail Jusa Ladu, Profesa Abdul Shariff, Agila Hila Vuai, Dk. Tulia Ackson, Amon Mpanju, Elizabeth Minde, Evord Mmanda, George Simbachawene, Nakazaeli Tenga, Peter Mziray, Honoratha Chitanda na Othman Masoud Othman.

Wabunge waonywa kuacha rushwa

Na Peter Orwa, Dodoma

MWANASHERIA Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, amewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kujiepusha na rushwa wakati wa uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa bunge hilo ili haki itendeke.
Uchaguzi huo utafanyika baada ya wajumbe kujadili na kupitisha Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalumu la Katiba, ambayo itaanza kujadiliwa Jumatatu.
Jaji Werema alitoa kauli hiyo jana alipowasilisha mada kwenye semina ya wajumbe wa Bunge Maalumu kuhusu Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Alisema ni vyema wajumbe wakaweka kando suala la itikadi, badala yake watende haki kwa kumchagua mtu atakayewanufaisha kwa kutenda haki, huku wakiweka kando rushwa.

“Nawaomba mtumie haki ya uchaguzi kwa busara. Naomba msianze mambo ya rushwa, tukianza hivyo tutaanza vibaya. Chagua mtu atakayetenda jukumu kwa haki,” alisema.
Jaji Werema pia aliwaomba wajumbe kuheshimu utaratibu na miongozo iliyowekwa, ikiwemo kuzungumza kwa zamu wanaporuhusiwa na kujenga utamaduni wa kuvumiliana wakati wa kuwasilisha hoja.
“Acheni tabia ya kila mmoja kuzungumza bila kupata ruhusa ya mwenyekiti, au kuwasha mic (vipaza sauti) kabla ya kuruhusiwa kuzungumza. Tusizungumze kama bata,” alisema.
Hata hivyo, tangu vikao vianze Jumanne wiki hii, baadhi ya wajumbe wamekuwa wakikiuka utaratibu kwa kuzungumza bila ruhusa, licha ya kupewa mwongozo wa namna ya kuzungumza ndani ya ukumbi.
Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, mwenyekiti na makamu wake, mmoja akitoka Tanzania Bara mwingine atatoka Zanzibar.
Wakati muda wa uchaguzi ukiwa bado, baadhi ya wajumbe wamekuwa wakitajwa kutaka kuwania nafasi hizo, huku wakihusishwa na kampeni za chini kwa chini.
Katika hatua nyingine, akiwasilisha mada, Jaji Werema alisema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, katika kifungu cha Tunu za Taifa inazuia wajumbe kufanyia marekebisho suala la Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hivyo hoja ya serikali moja ni suala gumu.
Hilo linafanya ajenda ya serikali moja inayodaiwa na baadhi wajumbe, akiwemo Rais wa TADEA, John Chipaka, kutojadilika.
Kuhusu hoja iliyoibuliwa na wajumbe wakihoji sababu za katiba kuwa katika lugha ya Kiswahili pekee, Jaji Werema alisema itaendelea kuwa katika lugha hiyo kwa kuwa hilo linatokana na uamuzi wa Mahakama ya Rufani Tanzania.
Jaji Werema alisema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba iko katika lugha za Kiingereza na Kiswahili, lakini mwongozo unaotumika ni kuwa, iwapo kutakuwepo mgongano wa tafsiri, ya Kiingereza ndiyo itatumika.Alisema kigezo hicho kimetumika kutokana na sababu za kihistoria ambazo hakuzifafanua.

Wednesday 19 February 2014

Mzee Makamba awapasha Lowassa, Membe

  • Awataka watumikie adhabu kwa uadilifu
  • Adai angekuwa yeye angekata rufani
  • Wasomi: CCM ni makini na imekomaa

Na Khadija Mussa

Yusuph Makamba - Katibu mkuu mstaafu wa CCM
ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa CCM, Yusuph Makamba, amewataka makada sita waliopewa onyo kwa kukiuka utaratibu wa Chama kutumikia kwa uaminifu na uadilifu.
Pia, alisema adhabu iliyotolewa kwa makada hao haikupaswa kulingana na kwamba, kila mmoja angepewa adhabu kwa kuzingatia makosa aliyokutwa nayo.
Makada hao ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu Fredrick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na wabunge Edward Lowassa (Monduli) na William Ngeleja (Sengerema), walitiwa hatiani kwa kukiuka utaratibu wa CCM.
Walituhumiwa kuanza kampeni za urais katika uchaguzi mkuu ujao kinyume cha utaratibu hivyo, kuvuruga utaratibu wa Chama, ambapo Kamati Ndogo ya Maadili iliwaita kuwahoji.
Juzi, Katibu wa NEC ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alitangaza kuwa makada hao wamepewa onyo kali na Chama kinaendelea kuchunguzwa mienendo yao kwa miezi 12 pamoja na kuzuiwa kugombea nafasi yoyote ya uongozi ndani ya Chama.
Hata hivyo, akizungumza na Uhuru jana kuhusiana na hatua zilizochukuliwa dhidi ya makada hayo, Makamba, alisema wanatakiwa kutumikia adhabu hiyo kwa uaminifu na uadilifu kama Nabii Ayoub.

“Nawaomba wawe wavumilivu kama Nabii Ayoub, na watumike adhabu hiyo kwa uaminifu na uadilifu.
“Wakifanya hivyo, watamaliza adhabu zao na watapata fursa ya kugombea tena nafasi za uongozi ndani ya Chama,’’ alisema Makamba.
Hata hivyo, alisema iwapo angekuwa yeye angekata rufani kwa kuwa adhabu hiyo imetolewa kwa ujumla huku makosa yaliyowatia hatiani makada hao yakitofautiana.
Alisema adhabu zilipaswa kuwa tofauti kulingana na makosa, kwani anasikia wapo waliotoa fedha kwa wanachama huku mafungu yanayotajwa yakitofautiana.
Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana, alisema hatua zilizochukuliwa na CCM dhidi ya makada hao inaonyesha namna kinavyo jipambanua kuwa ni makini na hakikurupuki.
Alisema CCM imekuwa ikisimamia nidhamu na misingi iliyojiwekea jambo ambalo litaendelea kukifanya kiimarike zaidi tofauti na vyama vingine.

“Nidhamu ni jambo zuri, hatua zilizochukuliwa dhidi ya makada wake ambao ni maarufu na wameshika nyadhifa kubwa serikalini, itasaidia kukiimarisha Chama,” alisema Dk. Bana.
Pia, alisema kilichofanywa na CCM ni funzo kwa vyama vingine vya siasa nchini katika kusimamia kanuni badala ya kukurupuka na kufukuza wanachama ama viongozi bila utaratibu.
Kwa upande wake Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Mohammed Bakari, alisema suala la kufuata utaratibu na sheria ndani ya chama ni zuri na muhimu.
Pia, aliipongeza CCM kwa kutoa onyo kali kwa makada wake ambao wamethibitika kwenda kinyume na kuvuruga utaratibu.

“Napongeza hatua zilizochukuliwa, mwenendo waliokuwa wakienda nao makada hawa haukuwa sahihi kwa mustakabali wa kanuni, hivyo CCM ipo sahihi katika hili,” alisema.
Alisema ni lazima CCM iendelea kuimarisha na kusisitiza matumizi ya kanuni zake inazotumia katika kuwapata viongozi kwani mambo yalivyokuwa yalianza kuwavuruga wanachama.
“Chama kibaki na kanuni na utaratibu wake katika kuwapata viongozi, mambo yalivyokuwa yakipelekwa si sahihi na ingeachwa ingewavuruga wanachama na kusababisha mpasuko mkubwa,’’ alisema.
Akitangaza adhabu hizo mbele ya waandishi wa habari juzi, Nape alisema Kamati Kuu ya CCM, imeiagiza Kamati Ndogo ya Udhibiti kuendelea kuwachunguza na kuchukua hatua kali kwa makada hao iwapo watakiuka onyo hilo.
Pia, imeagiza mawakala na wapambe wa makada hao walioshiriki kukivuruga Chama nao wachunguzwe na kuchukuliwa hatua kali.
Kwa mujibu wa Nape, waliohojiwa walithibitika kuanza kampeni za kutafuta kuteuliwa kugombea urais kabla ya wakati kinyume na kanuni za uongozi na maadili za CCM toleo la Februari 2010, ibara 6 (7) (i).
Pia, walithibitika kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya Chama na baadhi yao kukiuka maadili ndani ya jamii, jambo ambalo ni kinyume.
Kosa hilo ni kwa mujibu wa kanuni za uongozi na maadili za CCM toleo la Februari 2010, ibara kadhaa za kanuni.

Ikulu: Hatukuwa na nia ya kuwabagua Wapentekoste

Na Mohammed Issa

OFISI ya Rais, Ikulu, imesema uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, haukuwa na nia ya kulibagua Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.
Imesema kuna kila sababu ya kuamini kuwa mapendekezo ya wajumbe kutoka baraza hilo hayakuwasilishwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi kama sheria ilivyohitaji.
Pia, imesema pamoja na baraza hilo kutowasilisha mapendekezo yao kama ilivyotakiwa, litawakilishwa vyema na wajumbe walioteuliwa ambao wanajumuisha mjumbe aliyeteuliwa kutoka moja ya madhehebu yanayounda baraza hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ikulu mjini Dar es Salaam, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk. Florence Turuka, alisema tamko la Baraza la Maaskofu kuwa linabaguliwa na serikali halina ukweli wowote.
Dk. Turuka alitoa ufafanuzi huo kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, na kuongeza kuwa kama mapendekezo ya baraza hilo yengewasilishwa kwa mujibu wa sheria, yasingeachwa.
Alisema uchunguzi uliofanywa na Ikulu, haujathibitisha kuwa baraza hilo liliwasilisha mapendekezo yake na kwamba ni vyema baraza likajiuliza kwanini kama kulikuwa na mapendekezo hayakufikishwa kwa wakati kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi, Zanzibar.
Dk. Turuka, alisema iwapo mapendekezo ya baraza hilo yangefikishwa kwa makatibu wakuu hao, Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Alli Mohammed Sheni, wangechagua mwakilishi kutokana na mapendekezo hayo.
Alisema uchambuzi wa majina ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba umebaini kati ya wajumbe 13 kutoka taasisi za kidini wa Tanzania Bara walioteuliwa, Respa Adam, ameteuliwa kutoka Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT), Patmos Vission, Kigamboni, ni moja ya madhehebu ambayo maaskofu wake wakuu wanaunda baraza hilo.
Kwa mujibu wa Dk. Turuka, Februari 11, mwaka huu, baraza hilo lilitoa taarifa kwa vyombo vya habari kuwa limebaguliwa na serikali wanayoiheshimu, kuiombea na kuipenda katika uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.
Alisema anawahakikishia Watanzania hususan waliolengwa na taarifa ya baraza hilo kwamba serikali haikupuuzia kundi lolote lililoanishwa kwa mujibu wa sheria ya mabadiliko ya katiba.
Dk. Turuka alisema serikali inaliheshimu baraza na inalishukuru katika juhudi inazozifanya kwa kushirikina na serikali katika kuwaendeleza Watanzania.
Alisema makundi 850 yaliwasilisha mapendekezo ya majina 3,636, ambapo makundi ya kidini yalipendekeza majina 429.
Katibu Mkuu huyo, alisema uchambuzi wa mapendekezo 52 yaliyowasilishwa nje ya muda, haukubaini kuwepo kwa mapendekezo kutoka baraza la maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.
Katika hatua nyingine, Dk. Turuka alisema hana uhakika kuwa wajumbe waliochaguliwa kutoka Chama cha NLD ni mtu na mke wake.

Chipaka: Ni serikali mbili

Na Peter Orwa, Dodoma

WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza msimamo wa muundo wa serikali mbili, Rais wa TADEA, John Chipaka, amesema ataunga mkono iwapo hoja ya chama hicho ya serikali moja haitakubalika.
Chipaka, mmoja wa magwiji wa harakati za siasa za vyama vingi nchini, alisema hayo wakati wajumbe wa vyama vya upinzani katika Bunge Maalumu la Katiba mjini hapa wakiweka mkakati wa kuungana kutetea hoja ya serikali tatu.
Akizungumza katika viwanja vya Bunge mjini hapa jana, Chipaka alisema hoja ya serikali tatu haikubaliki, kwa sababu zitakuwa mzigo kwa wananchi.
Kwa mujibu wa Chipaka, hoja hiyo pia inapingana na waasisi wa taifa waliounda Muungano wa serikali mbili, wakilenga kuelekea serikali moja.
“Nakubaliana na wanaosema serikali tatu zitaongeza mzigo,” alisema na kuongeza kuwa, mizigo hiyo ni kuwa na marais wengi na jeshi zaidi ya moja. 
Habari zilizopatikana mjini hapa zinasema vyama vya upinzani vimekuwa vikikutana ndani ya majengo ya bunge vikipanga mikakati ya kushirikiana, ikiwemo kuhusu hoja ya Muungano.
Chipaka alikataa kushiriki vikao hivyo vinavyodaiwa kuratibiwa na CHADEMA chini ya Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Taarifa zinasema katika kikao cha juzi, washiriki walitofautiana huku wale wa vyama vidogo wakidai wamekuwa wakitengwa lakini linapotokea jambo kama hilo ndipo wanapoombwa ushirikiano. Katika hatua nyingine; CHADEMA imekuwa ikifanya ushawishi ikitaka kuungwa mkono kuhusu uraia wa serikali mbili.
Baadhi ya wabunge wa chama hicho wanadaiwa kupita kuwashawishi wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuwaunga mkono.

Kingunge awafunda wajumbe bunge la katiba

Na Theodos Mgomba, Dodoma

MJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba, Kingunge Ngombale –Mwiru, amewataka wajumbe wenzake kutanguliza mbele uzalendo wakati wa kupitia Rasimu ya Pili ya Katiba badala ya kuendekeza ubinafsi.
Kwa mujibu wa Kingunge, lengo la bunge hilo ni kupata katiba bora itakayolifikisha taifa katika miaka mingine 50 na si ya chama au mtu fulani. 
Alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa bunge baada ya kikao kuahirishwa.
Kwa mujibu wa Kingunge, ni muhimu kwa wajumbe kuthamini nafasi waliyoipata kwa kufanya uamuzi sahihi kuhusu hatima ya nchi na vizazi vijavyo.
Alisema katiba inayoandikwa si ya CCM, CHADEMA au CUF, bali ni ya Watanzania wote.

“Kama wataweka uzalendo mbele bila kujali itikadi za vyama, tutapata katiba bora ambayo itawasaidia wananchi  kwa vizazi vingi vijavyo,” alisema.
Alisema bunge hilo ni chombo kikubwa katika historia ya nchi.

Naye Peter Orwa, mwandishi mwingine aliyeko Dodoma ametaarifu kuwa:

MWENYEKITI wa Muda wa vikao vya Bunge Maalumu la Katiba, Pandu Ameir Kificho, amewateua wajumbe 20 watakaomshauri ili kuleta ufanisi wa utendaji.
Wengi kati ya walioteuliwa ni wataalamu wa sheria, wakiwemo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angelah Kairuki na Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA Tundu Lissu.
Wateule hao wanatoka pande zote mbili za Muungano.
Kificho alisema amefanya uteuzi huo kwa mujibu wa mamlaka aliyopewa kisheria. Alisema wajumbe hao watakuwa wakifuatilia vikao kwa kuchukua dodoso muhimu za kufanyia kazi na watakutana naye kujadili na kufanya uamuzi.
Wamo pia Profesa Costa Mahalu na Magdalena Rwebangira, ambao juzi waligombea nafasi ya mwenyekiti wa muda wa bunge hilo.
Wengine ni Abubakar Khamis Bakari, Mgeni Hassan Juma, Usi Jecha Simae, Ismail Jusa Ladu, Profesa Abdul Shariff,  Agila Hila Vuai, Dk.Tulia Akson, Amon Mpanju, Elizabeth Minde, Evord Mmanda, George Simbachawene, Nakazaeli Tenga, Peter Mziray, Honoratha Chitanda na Othman Masoud Othman.
Kificho alisema Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Werema, leo atatoa semina kwa wajumbe kuhusu Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalumu la Katiba ambayo iliwasilishwa bungeni jana na wajumbe kugawiwa nakala.
Alisema wajumbe watapewa nafasi ya kuzipitia kabla ya kuzipitisha Jumatatu ijayo ili kuwezesha mjadala wa Rasimu ya Katiba kuanza.

Tuesday 18 February 2014

URAIS 2015 - Vigogo sita CCM hatiani

Katibu wa NEC -  CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.
Na Mohammed Issa

MAKADA sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), waliotuhumiwa kuvuruga utaratibu na kanuni kwa kujihusisha na kampeni za urais kabla ya wakati wametiwa hatiani.
Makada hao ambao ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu Fredrick Sumaye, Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira, wamepewa onyo kali.
Pia, Chama kimewataka wajiepushe na vitendo vinavyokiuka maadili na iwapo wataendelea kitawachukulia hatua kali zaidi. Mbali na kupewa onyo kali, pia wametakiwa kutogombea uongozi wa aina yoyote ndani ya Chama kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Pia, Kamati Kuu ya CCM imeiagiza kamati ndogo ya udhibiti kuwachunguza na kuchukua hatua kwa mawakala na wapambe wa makada hao walioshiriki kufanya vitendo hivyo.
Katibu wa NEC ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema hayo jana katika Ofisi Ndogo za Chama, Lumumba, Dar es Salaam.
Nape, alisema makada hao wataendelea kuchunguzwa mwenendo wao ili kuwasaidia waweze kujirekebisha.
Alisema kati ya Februari 13 na 18, mwaka huu, Chama kimekuwa na mfululizo wa vikao kadhaa vilivyoshughulikia maadili, ambapo makada hao waliitwa kuhojiwa na Kamati Ndogo ya Maadili.
Alisema vikao hivyo ni pamoja na kamati ndogo ya udhibiti iliyokutana Februari 13 na 14, mwaka huu, pamoja na tume ya udhibiti na nidhamu na kamati kuu, iliyokutana juzi.
Nape alisema baada ya kuwahoji, ilithibitika kuwa baadhi ya tuhuma dhidi yao zilikuwa za ukweli ikiwemo kujihusisha na kampeni za urais kabla ya wakati na kupendekeza adhabu.
Alisema mapendekezo hayo yalipelekwa kwenye tume ya udhibiti na nidhamu na kamati kuu ambayo ilitoa adhabu kwa wahusika.
Kwa mujibu wa Nape, waliohojiwa walithibitika kuanza kampeni za kutafuta kuteuliwa kugombea urais kabla ya wakati kinyume na kanuni za uongozi na maadili za CCM toleo la Februari 2010, ibara 6 (7) (i).
Alisema pia wamethibitika kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya Chama na baadhi yao kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya jamii.
Nape alisema kosa hilo ni kwa mujibu wa kanuni za uongozi na maadili za CCM toleo la Februari 2010, ibara kadhaa za kanuni.
Alisema kamati kuu imewaonya viongozi na watendaji wa Chama na imewataka kutojihusisha na matendo ya kuwania urais, ambayo yanavunja na kukiuka maadili ya Chama na wanatakiwa kuzingatia kanuni na utaratibu.


CHADEMA iwe na adabu kwa Kikwete
 

Katika hatua nyingine; Nape aliitaka CHADEMA kuwa na nidhamu kwa Rais Jakaya Kikwete na kuacha kuweweseka.
Alisema kamwe Rais Kikwete hawezi kufuta kauli yake na kwamba, itakuwa kali zaidi ili kukomesha vitendo vya vurugu vinavyofanywa na wafuasi wa CHADEMA.
Juzi, viongozi wa CHADEMA walimtaka Rais Kikwete kufuta kauli yake aliyoitoa kwenye mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, akiwataka wanachama na mashabiki wa Chama hicho kuacha unyonge.
Katika mkutano huo, Rais Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, alisema kwa muda mrefu wana-CCM wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya vurugu na unyanyasaji na wafuasi wa CHADEMA,  wanapaswa kuwa ngangari.

“Mwenyekiti wetu hawezi kufuta kauli yake, CHADEMA wametufanyia unyama…tunawasubiri Kalenga waje wafanye hayo mambo yao tena.
“Kama wao ni jeshi la angani basi na sisi ni jeshi la nchi kavu na dawa ya moto ni moto, nina maanisha kuwa kama wao watatumia helkopta kufanya kampeni sisi tutatumia magari,” alisema Nape.
Hata hivyo, Nape alisema mchezo mchafu wa CHADEMA kuanza kuzitumia taasisi zisizo za kiserikali na wanaharakati kutoa matamko hayo umebainika.
“Tayari kuna taasisi ilishatoa taarifa, huu ni mpango endelevu, lakini ni mambo ambayo yanapaswa kutazamwa kwa umakini,” alisema mmoja wa viongozi wa Chama hicho makao makuu.
Utekelezaji wa matamko hayo yanafanywa na taasisi moja inayomilikiwa na chama hicho (jina linahifadhiwa), ambapo jana chama hicho pia kilitoa tamko la kumtaka Rais Kikwete aombe ardhi.

Mgimwa atikisa Kalenga

Na Tumaini Msowoya, Iringa

MAMIA ya wakazi wa Jimbo la Kalenga mkoani Iringa, jana walisimamisha shughuli za uzalishaji kwa muda, kwa ajili ya kumsindikiza mgombea ubunge wa CCM, Godfrey Mgimwa alipokuwa akirejesha fomu ya kuomba kuteuliwa na Tume ya Taifa ya uchaguzi (NEC).
Mgimwa alirejesha fomu hiyo baada ya kushinda kura za maoni ndani ya CCM na baadaye kupata baraka za vikao vyote vya Chama.
Akizungumza baada ya kurejesha fomu, Mgimwa alisema ana imani kuwa CCM itashinda kwa kishindo katika uchaguzi huo kutokana na mshikamano uliopo.
Aliwataka wakazi wa Kalenga kutobabaishwa na kelele za vyama vya upinzani ambavyo haviwezi kuwaletea maendeleo kama vitapata nafasi ya kuingia madarakani.
Alisema jimbo hilo linapaswa kubaki mikononi mwa CCM ili yale yaliyoanza kufanywa tangu mwaka 2010, yamaliziwe.

“Sikutarajia kuona watu wengi namna hii, nashukuru kwa kunisindikiza naamini safari ndiyo imeanza, utu huu mlionifanyia nitaulipa kwenu nawaomba sana mtulie wala msibabaishwe na vyama vya upinzani ambavyo haviwezi kutuletea maendeleo wana-Kalenga,” alisema.
Aliiponda CHADEMA kwa matumizi mabaya ya fedha kwa ajili ya kampeni ikiwemo kutumia magari ya kifahari na helkopta.
Alisema ufujaji huo hauwasaidii wananchi, bali unazidi kuwakandamiza kwani fedha hizo zingiweza kutumiwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo jimboni humo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Iringa, Delfina Mtavilalo, aliwataka wakazi hao kutokuwa wanyonge kama alivyotoa wito Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete, badala yake wahakikishe wanajibu hoja kwa hekima na busara.

Godfrey Mgimwa - Mgombea Ubunge CCM Jimbo la Kalenga
“Ili tuendelee kudumisha amani iliyopo tusiwe wanyonge, tujibu hoja kwa busara kama alivyotuasa Rais Kikwete, kwa kufanya hivyo, tutapata ushindi wa kishindo na tutajihakikishia usalama,” alisema.
Awali, Katibu wa CCM wa wilaya ya Iringa vijijini, Amina Imbo, alisema tayari maandalizi ya kampeni za ubunge kwenye jimbo hilo yamekamilika kinachosubiriwa ni kipenga cha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Aliwataka watu wote kuiunga mkoani CCM katika uchaguzi wa jimbo hilo kwa madai kuwa ndicho chama pekee chenye uwezo wa kuwasaidia wananchi wake.

“Maandalizi ya kampeni yamekamilika, nawaombeni sana tuiunge mkono CCM ili ituletee maendeleo,” alisema Imbo.
Alisema CCM ni chama makini ambacho kimeweza kuwaletea maendeleo Watanzania kwa utekelezaji wake mzuri wa ilani ya Uchaguzi.
Alisema iwapo itaendelea kuongoza jimbo hilo, utekelezaji wa Ilani ambao ulikuwa ukiendelea utakamilika.
Naye msimamizi mkuu wa uchaguzi wa Jimbo la Kalenga, Pudensiana Kisaka, alimpongeza mgombea wa CCM kwa kuwahi kurejesha fomu.
Alisema baada ya masaa 24 kupita lisipotokea pingamizi, atatangazwa rasmi kuwa mgombea.

“Hongereni kwa kufuata kanuni na sheria za uchaguzi, tumepokea fomu hii, tunaibandika hapo nje na baada ya masaa 24, kusipokuwa na pingamizi, atatangazwa rasmi kuwa mgombea,” alisema.
Alisitiza vyama vyote kuhakikisha vinafuata sheria na utaratibu wa uchaguzi ili kuepusha migongano isiyo ya lazima.

Ulinzi waimarishwa Bunge la Katiba,

Na Theodos Mgomba, Dodoma

ULINZI katika mkutano wa Bunge Maalumu la Katiba umeimarishwa ikiwa ni pamoja na kuongezwa vituo vya ukaguzi.
Katika vituo hivyo, watu wote wanaoingia na kutoka ndani ya ukumbi wa Bunge wanakaguliwa kwa kutumia mashine maalumu.
Ulinzi katika maeneo ya nje ya ukumbi pia umeimarishwa kwa kuwapo askari wenye silaha na kunafanyika doria ya askari wa kikosi cha farasi.
Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, jana wakati wa mkutano wa maelekezo ya ukaaji na jiografia ya ukumbi wa bunge, alisema kila mjumbe ataonekana alipo awapo ndani ya ukumbi au nje.
Alisema hilo linatokana na vifaa vya ulinzi vilivyoko katika jengo hilo kuwa vya kisasa zaidi.

“Nawaomba ndugu zangu wajumbe mtambue kuwa ulinzi umeimarishwa, hivyo hata ukiegesha gari nje, jicho letu linaweza kufika huko,” alisema.
Awali, akitoa taarifa, Mratibu wa Ulinzi wa Bunge, Peter Magati, alisema ulinzi umeongezwa, hivyo wajumbe na wengine wote wanaoingia na kutoka ndani ya ukumbi na jengo la bunge watatakiwa kukaguliwa mara mbili.
Magati alisema sababu ya kuongezwa ulinzi ni kutaka kuhakikisha usalama wa wajumbe unakuwa wa kutosha.

“Nawaomba wajumbe mridhie hali hiyo. Tumejipanga vizuri,” alisema na kuwataka wajumbe kuvaa vitambulisho wawapo ndani ya ukumbi na maeneo ya bunge ili kuwaepushia usumbufu.
Kuhusu mavazi, aliwataka kuvaa yenye staha, vinginevyo watarejeshwa wakabadilishe.

Wakati huo huo, Peter Orwa ameripoti kuwa

KATIBU wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, amesema wasaidizi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wenye watoto wachanga watalipwa posho.
Bila kutaja kiwango cha posho hiyo na ni lini itaanza kutolewa, Dk. Kashililah alisema italipwa pia kwa wasaidizi wa wajumbe wenye mahitaji maalumu.
Dk. Kashililah alisema hayo jana asubuhi wakati wa mkutano wa maelekezo ya ukaaji na jiografia ya ukumbi wa bunge.
Alisema kwa kuzingatia haki ya kunyoyesha, kitatengwa chumba maalumu kwa ajili ya wajumbe hao.
Wajumbe hao wanalipwa posho ya kujikimu ya sh. 80,000 na sh. 220,000 ni kwa ajili ya kuhuhudhuria vikao na kuwalipa madereva.
Dk. Kashililah alisema wajumbe wote watapata huduma ya matibabu bure katika zahanati iliyo ndani ya viunga vya ukumbi wa bunge na katika hospitali za serikali na kwa watakaolazimika kutibiwa katika hospitali binafsi watarejeshewa fedha zao.
Kwa wajumbe wanaovuta sigara, wametengewa eneo maalumu katika mgahawa ulio ndani ya viunga vya Bunge.

Wasomi washauri serikali mbili

NA Khadija Mussa

WASOMI wamesema mfumo wa serikali tatu ni changamoto na mzigo mkubwa kwa Tanzania, hivyo ni vyema uliopo kwa sasa wa serikali mbili ukaendelea. 
Wameshauri kuwa mfumo wa serikali moja unaweza kuwa suluhisho na kuwaunganisha Watanzania, lakini kwa sasa utekelezaji wake ni mgumu.
Pia, wamesema ni vyema kukawekwa utaratibu maalumu wa kuwaenzi waasisi wa Muungano na kuendeleza misingi yao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Mpango wa Utafiti wa Vyuo Vikuu Kusini Mashariki mwa Afrika (ESAURP), Profesa Ted Maliyamkono, alisema kero za wananchi haziwezi kutatuliwa kwa kuwa na serikali tatu.
Aliyasema hayo wakati wa mkutano wa kujadili Katiba Bora ya Tanzania uliojumuisha wasomi takribani 100 kutoka Angola, Botswana, Tanzania, Kenya, Lesotho, Malawi, Msumbiji, Swazland, Uganda, Zambia, Zimbabwe na Afrika Kusini.
Uifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Alisema kwa mujibu wa utafiti walioufanya, serikali moja ndiyo itakayoweza kuwaunganisha wananchi na kutatua kero zinazowakabili.
“Tathmini inaelekea katika serikali moja, lakini kabla ya kufika huko inabidi tuendelee na iliyopo kwa sasa (serikali mbili), kwani hatuwezi kuwa na serikali tatu au nne,” alisema.
Mhadhiri wa Sheria za Katiba na Haki za Binadamu, Dk. Charles Kitima, alisema suala la kuwa na serikali tatu ni jibu la kukata tama.
Alishauri waasisi wa taifa waenziwe kwa kuwa na serikali moja.
Alisema ni lazima watu wahakikishe ndoto za waasisi wa taifa zilizoasisiwa mwaka 1964 za kuwa na serikali moja zinatimizwa, kwani waliona ni vyema waanze na mbili ili lengo la kuwa na serikali moja lije baadaye.
Dk. Kitima, alisema taifa imara linapaswa kuwaenzi waasisi wake, hivyo misingi iliyowekwa inatakiwa kuendelezwa na watu wasianze kuunda taifa, badala yake warudi katika misingi iliyowekwa wakati waasisi hao walipoamua kuungana.
Naye Profesa Peter Kagwanja ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Chuo cha Africa Policy kilichopo Nairobi, Kenya, alisema suala la serikali tatu ni changamoto na kushauri wananchi wakubaliane na mfumo wa sasa.

MICHEZO - Watanzania waitwa Ujerumani kucheza Soka la kulipwa

Na Amina Athumani

WATANZANIA watatu wanaocheza soka wameombewa Hati za Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa ajili ya kucheza mpira wa kulipwa katika nchi za Thailand na Ujerumani.
Wachezaji hao ni Khamis Jamal, Said Nassor na Samuel Chuonyo ambao wanacheza soka katika klabu mbalimbali nchini.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura, alisema Mroki wa timu ya Polisi Dar es Salaam, ameombewa ITC Thailand (FAT) kujiunga na Kabinburi ya nchini humo.
Alisema Nassor na Chuonyo wanaocheza FC Turkey ya Zanzibar wameombewa ITC na Chama cha Mpira wa Miguu Ujerumani (DFB) kwa ajili ya kujiunga na klabu ya VfB Eichstatt.
Alisema TFF inafanyia kazi maombi hayo na baada ya utaratibu kukamilika ikiwemo ridhaa kutoka kwa klabu zao shirikisho hilo litatoa ITC hizo.
Wakati huo huo, timu ya Stand United ya Shinyanga imekata rufani TFF kupinga Kanembwa JKT ya Kigoma kuchezesha wachezaji waliosajiliwa katika dirisha dogo katika mchezo wao wa kiporo.
Mchezo huo namba 22 wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL) ulichezwa juzi kwenye Uwanja wa Ali Hassani Mwinyi mjini Tabora ambapo Kanembwa JKT iliibuka na ushindi wa bao 1-0.
Boniface Wambura alisema Stand United inadai Kanembwa JKT iliwatumia wachezaji wanane kinyume na maelekezo kutoka TFF.
Wachezaji wanaodaiwa kusajiliwa katika dirisha dogo ni Hamidu Juma, Ibrahim Issa, Joseph Mlary, Lucas Karanga, Raji Ismail, Salvatory Raphael, Seif Zaidi na Yonathan Sabugowiga.
Alisema dirisha dogo lilifunguliwa Novemba 15 na kufungwa Desemba 15, mwaka jana, hivyo Stand United katika rufani yake inaombwa ipewe pointi tatu na mabao matatu.
Awali, mchezo huo ulichezwa Novemba 2, mwaka jana Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga kabla ya kuvunjwa na mwamuzi dakika ya 87 baada ya Kanembwa JKT kugomea mkwaju wa penalti.

Meno ya tembo yanaswa Singida

Na Nathaniel Limu, Singida

JESHI Polisi mkoani hapa, limekamata vipande 16  vya meno ya tembo vyenye thamani ya sh. milioni 17.
Vipande hivyo ni sawa na tembo wakubwa wanne na tembo watano wadogo waliouawa na majangili.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Cordula Lyimo, alisema meno hayo yalikamatwa Jumapili iliyopita, saa tano usiku katika kizuizi cha mazao kilichoko kijiji cha Ukimbu, Itigi wilayani Manyoni.
Alisema askari wakiwa katika kizuizi hicho, walifanya ukaguzi kwenye gari  lenye namba za usajili T.288 AJF aina ya Scania, mali ya Kampuni ya Super Service likiendeshwa na Ally Hamadi akitokea Makogolosi, Chunya kwenda Itigi.
"Baada ya upekuzi huo, walikuta meno hayo yakiwa yamehifadhiwa ndani ya begi la nguo na kuwekwa kwenye keria za ndani ya basi. Mtuhumiwa aliweza kupatikana wakati akiwa katika juhudi za kutaka kutoka ndani ya basi ili akimbie,” alisema.
Kaimu Kamanda huyo alisema uchuguzi zaidi unaendelea ili kubaini na kuupata mtandao kamili unaojihusisha na kuwinda na kununua nyara hizo.
Idadi hiyo inafanya kufikisha vipande 37 vilivyokamatwa ndani ya wiki moja kwenye kizuzi cha mazao cha Ukimbu, mkoani Singida.

TAMWA kuzindua ripoti utafiti wa kijinsia

Na Mwandishi wetu

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), leo wanatarajia kuzindua ripoti ya utafiti wa kijinsia uliofanyika Desemba, mwaka jana katika wilaya 20 za Tanzania.
Ripoti hiyo inatarajiwa kuzinduliwa katika ofisi za TAMWA zilizoko Sinza Mori, Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka, alisema jana kuwa uzinduzi huo unatokana na utafiti uliofanyika baada ya mafunzo kutolewa kwa waandishi wa habari  juu  ya habari za uchunguzi kuhusu a ukatili wa kijinsia, chini ya ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu UNFPA.
Alisema ripoti hiyo ya utafiti inaonyesha hali halisi ya unyanyasaji wa kijinsia katika jamii pamoja na mambo yanayokwamisha juhudi za vyombo vinavyotetea haki za wanawake na watoto hapa nchini.
Kwa mujibu wa Valerie, utafiti huo ulifanywa kwa kushirikiana na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali.
Mkurugenzi Mtendaji huyo alisema waandishi wa habari waliweza kuwahoji wanajamii mbalimbali kuanzia ngazi za familia na kupata ukweli wa hali halisi ya unyanyasaji wa kijinsia ikiwemo, ukeketaji, ubakaji, mauaji ya vikongwe, mimba katika umri mdogo na watoto wa kike kulazimishwa kuolewa.
Wilaya ziliyofanyiwa utafiti ni Kahama (Shinyanga), Tarime (Mara), Sengerema (Mwanza), Newala (Mtwara), Mbulu (Manyara), Singida Vijijini (Singida), Bariadi (Simiyu), Busega (Simiyu), Nkasi (Rukwa), Dodoma (Dodoma), Babati (Manyara), Chunya (Mbeya) na Bunda (Mara).
Kwa upande wa Zanzibar utafiti ulifanywa katika wilaya sita za mikoa ya Mjini Magharibi, Kusini Pemba, Kaskazini Pemba, Unguja Kusini na Kaskazini Unguja.

UWT yampongeza JK


Na Mwandishi Wetu

UMOJA wa Wanawake wa Tanzania (UWT) umempongeza Rais Jakaya Kikwete kwa uteuzi wake wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba lililoanza jana mjini Dodoma.
UWT imewataka wajumbe waliochaguliwa kuwepo katika bunge hilo kutambua dhamana waliopewa na Rais kwa kuhakikisha wanahakikisha wanawatetea wananchi ndani ya bunge hilo katika kupata Katiba Mpya.
Taarifa iliyotolewa jana na Naibu Katibu Mkuu (Bara) wa UWT, Eva Kihwele, ilisema wajumbe wanapaswa kuzingatia ueledi na uadilifu katika kutengeneza katiba ya Tanzania yenye kulinda kutetea na kusimamia maslahi ya taifa.
"Katibu Mkuu wa UWT, Amina Makilagi, anampongeza Rais Kikwete kwa uteuzi huo, kwa kuwa umezingatia uwakilishi wa makundi mbalimbali ya kijamii na hasa kutimiza 50/50 ya uwakilishi wa wajumbe,''alisema.
Hivyo, UWT ilisema inawatakia kazi njema katika kuhakikisha wanalijenga taifa moja na imara katika upatikanaji wa Katiba mpya.

Mkutano biashara Manyara kuanza leo

Na Mwandishi wetu, Manyara

MKUTANO wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Manyara ambao ulikuwa unasubiriwa kwa muda mrefu tangu kufanyika kwa Kongamano kubwa la Uwekezaji mwaka jana, unafanyika leo chini ya uenyekiti wa Mkuu wa Mkoa huo, Elaston Mbwilo.
Mbwilo aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa kwamba maandalizi yote ya mkutano huo muhimu yamekamilika na moja ya agenda kuu itakuwa matokeo ya kongamano la uwekezaji na utekelezaji wake.
“Wajumbe wote kutoka sekta za umma na ile binafsi wamethibitisha ushiriki wao hapo kesho (leo) na kila kuhusiana na mkutano wetu kipo safi,” alisema Mkuu wa Mkoa huyo.
Mbwilo alisema mkutano huo una maana kubwa sana ikizingatiwa kuwa mwaka jana uliandaa kongamano kubwa la uwekezaji ambalo lilivuta wawekezaji wengi wa ndani na wale wan je hivyo utatoa nafasi kubwa kwa wajumbe kujadili matokeo yake kwa kina.
“Wajumbe wa baraza watapata fursa ya kupitia utekelezaji wa mambo yote yaliyokubaliwa wakati wa kongamano ambalo lilihudhuriwa pia na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,” alisema.
Akifafanua zaidi umuhimu wa mkutano huo, Mbwilo alisema tangu kuanzishwa kwa baraza hilo la biashara mkoa, sekta za umma na binafsi zimekuwa zikifanya kazi kwa ukaribu mkubwa na hivyo kuibua fursa mbalimbali za kibiashara.
“Mkoa huu Manyara una utajiri mkubwa sana na sisi kama baraza la mkoa tunatumia mikutano kama huu kujadiliana kwa kina ni namna gani tunaweza kutumia fursa hizi kubadilisha maisha ya watu na kujenga kujenga uchumi imara.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), Mhandisi Raymond Mbilinyi, ambaye anahudhuria mkutano huo, amelisifu baraza la Mkoa wa Manyara kwa kuandaa mkutano na kuiomba mikoa mingine kufanya hivyo.

TANESCO yapokea mitambo ya Umeme

SERIKALI imepokea mitambo miwili ya kuzalisha umeme wa megawati 75 kwa ajili ya mradi wa Kinyerezi I ambao unatarajiwa kukamilika  Oktoba, mwaka huu.
Mitambo hiyo kutoka Marekani, ilipokewa jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, ambaye alikuwa ameambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mhandisi Felchesmi Mramba, katika bandari ya Dar es Salaam.
Maswi alisema mradi wa Kinyerezi I utazalisha megawati 150 na kwamba mitambo hiyo ni ya awamu ya kwanza ambayo itakuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 75.
"Serikali tunatekeleza ahadi tulizozitoa kwa wananchi katika kupunguza ghrama za uzalishaji umeme. Meli hii kubwa ina shehena ya mitambo ya kuzalisha megawati 75 ambayo tutaisimika Februari 28, mwaka huu," alisema.
Alisema mitambo hiyo haitakuwa na athari kwa kuwa ni ya kisasa na awamu ya pili itawasili nchini mwezi ujao. Mitambo hiyo imetengenezwa na kampuni ya General Electric.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Mramba, alisema kuwasili kwa mitambo hiyo ni hatua za msingi za kutatua tatizo la umeme nchini, ambapo tangu uhuru uwekezaji wake ulikuwa duni.
"Katika historia ya nchi tangu Uhuru hatujawahi kuwa na uwekezaji mkubwa kama huu. Mitambo  ya kuzalisha umeme itatatua suala la uzalishaji umeme hivyo bado usafirishaji na usambazaji. Watanzania tuna mipango mingi inayotekelezeka jitihada za leo (jana) ni sehemu ya mipango hiyo," alisema.
Mhandisi Mramba alisema katika eneo la Kinyerezi kuna miradi minne ambayo ni Kinyerezi I, II, III, IV ambayo itapunguza matatizo ya uzalishaji umeme.
Aliwaomba Watanzania kuwa na subira kwa kuwa matatizo ya umeme yatafika mwisho kutokana na miradi mikubwa iliyopo ambayo utekelezaji wake ni wa makini na madhubuti.
Kwa upande wake, Meneja wa Miradi ya Uzalishaji Umeme TANESCO, Mhandisi Simon Jirima, alisema mitambo hiyo itahifadhiwa katika eneo la mradi na baada ya uzalishaji, umeme utaingizwa kwenye gridi ya taifa.
Mhandisi Jirima alisema mradi huo utagharimu dola za Marekani milioni 183 (zaidi ya sh. bilioni 250).

Sunday 16 February 2014

Wabunge kulamba 300,000 kwa siku

Na Mwandishi wetu

KITENDAWILI cha posho za wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba sasa kimeteguliwa, ambapo imeelezwa itakuwa sh. 300,000 kwa siku.
Tayari wabunge wameanza kuwasili tangu Jumamosi na leo watapewa mafunzo maalumu ya namna ya kutumia ukumbi na miundombiu mingine ndani ya Ukumbi wa Bunge.
Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, alisema jana kuwa malipo hayo yatahusisha posho ya kikao sh. 80,000 huku posho zingine ikiwemo usafiri, madereva zitakuwa sh. 220,000 kwa siku.
Pia, alisema ukarabati wa jingo pamoja na miundombinu miengine ya ukumbi kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya wabunge zaidi ya 650, yamegharimu kiasi cha sh. Bilioni 8.2.
Dk. Kashillilah alisema mkutano wa Bunge hilo maalum utazinduliwa rasmi Februari 26, mwaka huu, kesho utafanyika mkutano wa maelekezo ya ukaaji na jiografia ya ukumbi.
Alisema wabunge wameanza kusajili jana na kazi hiyo itaendelea tena leo na kwamba, kesho asubuhi mkutano wa maelekezo utaanza hadi mchana utafanyika uchaguzi wa Mwenyekiti wa muda, kuandaa na kupitisha Kanuni za Bunge.
“Mwenyekiti wa muda atachaguliwa kwa utaratibu maalumu uliowekwa na Katibu wa Bunge la Muungano na wa Baraza la Wawakilishi. Mwenyekiti wa muda atasimamia kuchaguliwa kwa Mwenyekiti na Makamu wake kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba,” alisema Dk Kashillilah.
Alisema Mwenyekiti wa muda pia atasimamia kuandaliwa kwa kanuni na baada ya kupatikana kwa viongozi hao, ndipo Katibu wa Bunge na Naibu wake watateuliwa kwa Sheria.
Pia, alisema kabla ya viongozi hao kuanza kutekeleza majukumu hayo mazito kwa taifa, watendaji hao wataapishwa na Rais Jakaya Kikwete.
Rais Jakaya Kikwete atazindua rasmi Bunge hilo Jumatatu saa 10 jioni na kwamba, wabunge wote wataapishwa siku hiyo saa 4 asubuhi na baadaye kuunda Kamati za Bunge Maalumu.
Uwasilishaji wa Rasimu ya Katiba katika Bunge Maalumu hilo utafanyika Februari 26 na kwamba, mjadala wa kupitisha Rasimu ya Katiba na utahitimishwa Aprili 30, mwaka huu.
Kwa mujibu wa kifungu cha 25 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Bunge Maalumu litakuwa na mamlaka ya kujadili na kupitisha masharti ya
Katiba inayopendekezwa na kutunga masharti ya Mpito na masharti yatokanayo kama Bunge Maalumu litakavyoona inafaa.
Ili Katiba inayopendekezwa iweze kupitishwa katika Bunge Maalumu la Katiba, itahitaji kuungwa mkono kwa wingi wa theluthi mbili ya idadi
ya wajumbe wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili kutoka Zanzibar.
Bunge Maalumu la Katiba litakuwa na wabunge 629 ikiwa ni wa Bunge la Muungano na Baraza la Wawakilishi pamoja na wale wa kuteuliwa.