Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Pata mafanikio, tangaza hapa

Tangaza nasi hapa.

Wednesday 30 July 2014

Maafa makubwa



  • Ajali basi na lori yaua 17, yajeruhi 56
  • Waliokufa, waliojeruhiwa watambuliwa
  •  DC Kangoye aongoza shughuli ya ukoaji

Na Waandishi Wetu
WAKATI Waislamu wakiendelea kusherehekea Sikukuu ya Idd elFitri, vilio na simanzi vimetawala eneo la Pandambili wilayani Kongwa, Dodoma, kutokana na ajali mbaya iliyosababisha watu 17 kupoteza maisha.


Mbali na vifo hivyo, ajali hiyo iliyohusisha basi la Kampuni ya Moro Best na lori lililokuwa limebeba mabomba, pia imejeruhi watu wengine 56. Katika ajali hiyo madereva wote wa basi na lori pamoja na wasaidizi wao, wamepoteza maisha.
Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Christopher Kangoye, ambaye alifika eneo la tukio muda mfupi baada ya ajali, alisema ilihusisha basi hilo lenye namba T 258 AHV aina ya Scania, ambalo liligongana uso kwa uso na lori lenye namba T 820 CKU likiwa na tela lake.
Alisema lori hilo lililokuwa limepakia mabomba, liligongana uso kwa uso na basi na kwamba chanzo ni uzembe wa dereva wa lori.
Alisema dereva huyo alikuwa akijaribu kulipita gari bila kuchukua tahadhari. Kabla  ya kugongana uso kwa uso na basi, aligonga gari lingine.
Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alisema ajali hiyo ilitokea jana saa mbili asubuhi na kati ya waliopoteza maisha 12 ni wanaume na wanawake ni watano.
Alisema basi hilo lilikuwa likitoka Mpwapwa kwenda Dar es Salaam na lilikuwa likiendeshwa na Said Lusogo huku lori likiendeshwa na Gilbert Nemanya.
Kamanda Misime alisema mpaka jana jioni, miili ya watu 11 ilikuwa imetambuliwa na ndugu na jamaa.
Waliotambuliwa ni dereva wa lori Gilbert Nemanya na utingo wake Mikidadi Zuberi, dereva wa basi la Morobest, Saidi Lusogo na kondakta wake, Omary Mkubwa.
Wengine ni Merina Malikeli, Nasib Machenje, Wilson Suda, Gabriel Mejachiwipe, Justine Makasi na mwanamke aliyetambuliwa kwa jina la Christina.
Kamanda Misime alisema majeruhi 56 wa ajali hiyo wamelazwa Hospitali za Wilaya ya Kongwa na Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Dodoma, ambapo wamepata majeraha mbalimbali mwilini.
Mpaka jioni, majeruhi waliokuwa wamelazwa Dodoma walikuwa 23 wakiwemo Frank Raymond, Patricia Ngamwai, Amos Chiwaga, Mary Mateo, Safari Jonas, Suzan Charles, Gasper Shao, Felician Rite, Felister Mathias, Amos Jonas, Edina Lwande, Seleman Kaseni, Nazareth Kasua, Simon Msoloka, Juma Mtezi na Swalehe Bakari.
Wengine ni Naseria John, Getruba Kombo, George Njelewa, Manase Makuja, Chibago Mchiwa, Nicholous Roger na Michael Chibwela.
Kangoye aliwataka wananchi wenye ndugu na jamaa waliokuwa wakisafiri na basi hilo, kufika kwenye hospitali kwa ajili ya kuwatambua.
Eneo la Pandambili limekuwa maarufu kutokana na ajali za mara kwa mara zinazogharimu maisha ya watu. Ni eneo ambalo aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, alipata ajali mbaya na kufariki dunia papo hapo.

Mfanyakazi wa ndani atoweka na kichanga



  • Mwingine aiba mtoto wa miaka miwili

NA MWANDISHI WETU, MWANZA
WIMBI la wizi wa watoto sasa limeanza kushika kasi nchini, ambapo watumishi wawili wa ndani kwa nyakati na maeneo tofauti, wametoweka na watoto wa waajiri wao.
Miongoni mwa watoto walioibwa, yupo mwenye umri wa miezi tisa na mwingine miaka miwili na nusu. Kati ya hao, mmoja amepatikana akiwa ametelekezwa barabarani.
Watumishi hao walikuwa wakiwalea watoto hao, ambapo waliofanikiwa kuwaiba wazazi wao wakiwa kwenye shughuli za uzalishaji mali.
Matukio hayo yametokea jijini Mwanza, ambapo la kwanza limetokea Ibanda, mtaa wa Nyabulogoya wilayani Nyamagana. Katika tukio hilo, mtoto Patrick Mwendesha (2), aliibwa na Vestina Odilo, aliyekuwa akimlea.
Kwa mujibu wa mama mzazi wa Patrick, Rosemary Mutakyahwa,  Vestina baada ya kutoweka na mtoto huyo bila taarifa, juhudi za kumsaka zilianza katika maeneo mbalimbali.
Alisema mapema wiki hii, Vestina alitiwa mbaroni katika eneo la Pasiansi wilayani Ilemela, alikomtelekeza mtoto huyo. Alisema wananchi walimbana na hatimaye kukiri kuwa si wake bali ni wa bosi wake.
Alipobanwa zaidi, Vestina alidai kuwa aliondoka na mtoto huyo baada ya kumlilia hivyo aliingiwa na huruma na kuamua kuondoka naye kwa kuwa amekuwa akiishi naye siku zote, hivyo amemzoea.
“Huyo mfanyakazi nililetewa na rafiki yangu anisaidie kazi za ndani. Siku  anamwiba mtoto nilimwachia kwa sababu nilishamzoea, hivyo nikaenda kujipumzisha (kulala) kidogo. Nilipoamka sikumkuta yeye wala mwanangu,” alisema.
Alisema baada ya kubaini mtumishi huyo kutoweka na mtoto, alitoa taarifa kituo cha polisi pamoja na rafiki yake ili kumsaidia kumsaka. Alifanikiwa kutiwa mbaroni na wasamaria wema.
“Alipohojiwa, alidai alimlilia hivyo akaamua kuondoka naye. Namshukuru  Mungu mtoto kapatikana. Tunawapenda wadada wa kazi, lakini tunapaswa kuwa makini na tuchunguze mahali walikotoka,” alishauri mama huyo.
Tukio lingine limetokea Jumanne ya wiki iliyopita, ambapo kichanga cha mwezi mmoja na siku saba, Aida Nuru, kiliibwa na mwananmke aliyekuwa akiishi jirani kwa Mwenyekiti wa Mtaa wa Mbugani, Bernard Wegero.
Mama mzazi wa mtoto huyo, Flora Sospeter, alisema siku ya tukio, saa 12 jioni wakati akianika nguo alimwacha mwanawe na msichana huyo aliyemtaja kwa jina la Lucia Juma.
Hata hivyo, alisema baada ya kumaliza shughuli yake alikuta msichana huyo ametoweka na mwanawe.
Wegero pamoja na kuthibitisha kuwa Lucia (20) alikuwa akiishi kwake, alidai hawezi kuzungumzia suala hilo zaidi kwa kuwa ana shughuli nyingi za kusikiliza kero za wananchi wa mtaa wake.
“Mie niko bize, ninasikiliza kesi za wananchi wa mtaa wangu, njoo kesho,” alisema lakini hata alipotafutwa siku iliyofuata, alidai pia hana muda.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Christopher Fuime, alithibitisha kutokea kwa matukio hayo na kusema Vestina amepandishwa kizimbani kujibu mashitaka yanayomkabili.
Kwa upande wa Lucia, alisema anashikiliwa kwa uchunguzi zaidi kabla ya kufikishwa mahakamani.
Kamanda Fuime alieleza kuwa, Lucia aliyekuwa akiishi kwa Wegero akitumia jina bandia la Diana, alikamatwa juzi mjini Musoma akiwa katika harakati za kutoroka.
Hivi karibuni watoto kadhaa waliripotiwa kuibwa jijini Dar es Salaam, ambapo mtoto Meryline Repyson, aligundulika kufichwa Tandale kwa Mtogole, Dar es Salaam.
Mwizi wa mtoto huyo alikuwa akifanya mawasiliano na wazazi wa mtoto huyo akidai kulipwa fidia ya sh. milioni tatu ndipo awakabidhi.
Hata hivyo, alilipwa kiasi cha sh. 300,000 ambazo alitumiwa kwa njia ya mtandao wa simu ya mkononi.

Kumekucha Bunge la Katiba


NA MWANDISHI WETU
WAKATI  Umoja wa Katiba ya Watanzania (UKAWA), wakiendelea kukaidi matamko ya serikali na viongozi wa dini ya kuwataka kurejea bungeni, vikao vya bunge hilo litaanza rasmi Agosti 5, mwaka huu.

Wajumbe wanaounda kundi la UKAWA, ambao ni kutoka CUF, CHADEMA na NCCR-Mageuzi, wakiongozwa na Mwenyekiti wa CUF Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba, walisusia vikao hivyo kwa madai ya kuwepo kwa upendeleo na ubaguzi.
Hata hivyo, baadaye walibadili hoja ya upendeleo na ubaguzi na kuibuka na mpya wakidai kuwa mgawanyo sawa wa wajumbe baina ya CCM ambayo ina wabunge wengi bungeni na vyama vya upinzani.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisi ya Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, wajumbe wote wametakiwa kuwasili mjini Dodoma kuanzia Jumapili ijayo.
Juzi, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) wakati wa kuwasilisha salamu zake kwenye sherehe za Baraza la Idd El-Fitri lililofanyika Viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam, limewataka wajumbe wa UKAWA kurudi bungeni kuendelea na mchakato.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ndiye alikuwa mgeni rasmi kwenye Baraza hilo lililohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, chama pamoja na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa Shabaan bin Simba.
BAKWATA imesema mamilioni ya shilingi za walipakodi zimetumika katika mchakato huo, hivyo kuuachia njiani ni usaliti na kitendo ambacho hakikubaliki.
Akiwasilisha salamu hizo mbele ya mamia ya mamia ya waumini wa dini ya kiislamu, Katibu Mkuu wa BAKWATA, Alhaj Suleiman Lolila, alisema kitendo cha baadhi ya wajumbe kususia bunge hilo ni pigo kwa Watanzania.
Alisema UKAWA wanapaswa kurejea bungeni kuendelea na majadiliano ili kuwawezesha Watanzania kupata Katiba Mpya na kuwa, iwapo kuna tofauti za mawazo au misimamo zinapaswa kujadiliwa ndani ya Bunge kwa kutumia Rasimu iliyowekwa mbele.
BAKWATA pia imeeleza kusikitishwa kwake kutokana na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kushindwa kuyatilia maanani mapendekezo yake katika Rasimu Mpya ya Katiba.
Hata hivyo, imesema kuwa haitakata tamaa na badala yake itaendelea kuangalia namna bora ya kuwasilisha.
Kwa muda mrefu kumekuwa na jitihada mbalimbali za kuhakikisha wajumbe wa Ukawa wanarejea bungeni baada ya kususia vikao. Viongizi wa serikali, taasisi za dini zote na asasi za kiraia, wanasiasa wamekuwa wakiwasihi wajumbe wa kundi hilo kurejea bungeni ili kukamilisha mchakato wa Katiba Mpya.
Hata hivyo, kumewepo na tuhuma mbalimbali kuwa kundi hilo limekuwa likitumiwa na baadhi ya mataifa kwa lengo la kukwamisha mchakato huo.
Yapo madai pia baadhi ya wajumbe wamekuwa wakilipwa kati ya sh. 500,000 hadi milioni moja kwa siku kwa kususia vikao vya bunge hilo na kuendeleza vuguvugu la kuwarubuni wananchi ili wawaunge mkono.

Tibaijuka: Nimejipanga kutimiza ahadi zangu


NA MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa  Anna Tibaijuka, amesema mikakati aliyojiwekea kwa sasa ni kutimiza ahadi alizowapa wapigakura na kutekeleza Ilani ya Uchanguzi ya CCM ya mwaka 2010.
Aliyasema hayo kwenye ziara ya Rais Jakaya Kikwete mikoa ya kusini mwa Tanzania, ambako walipokewa kwa shangwe na kundi la wananchi kutokana na kufanikiwa kutatua kero nyingi za ardhi zilizokuwa katika maeneo yao.
Utatuzi huo ulihusisha pia kumnyang’anya ardhi mwekezaji ambaye alikuwa akitaka kuendelea kuhodhi eneo kubwa  lililopaswa kumilikiwa na wananchi.
Sambamba na hilo, Profesa Tibaijuka alipongezwa na wananchi hao wa mikoa ya Lindi na Ruvuma kwa kulisimamia kwa makini Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), katika utekelezaji wa majukumu hali iliyosaidia kuongeza ufanisi katika uanzishaji wa miradi katika mikoa mbalimbali nchini.
“Kwa kazi inayofanywa na NHC, kweli Waziri Tibaijuka amefanya kazi. Miradi inayoendelea kutekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa kote nchini, ni chachu ya maendeleo na bila shaka miji yote itakuwa imepangika kama tulivyowahi kuota baadhi ya Watanzania juu ya mipango miji inayoeleweka katika nchi yetu,” alisema mmoja wa wananchi hao.   
Hata hivyo katika ziara hiyo, Rais Kikwete alisema serikali inamjali kila Mtanzania bila kujali eneo alipo tofauti na ilivyoaminika miaka kadhaa iliyopita, kuwa haitoi kipaumbele kwenye mikoa ya kusini.
Mkoani Ruvuma, Rais Kikwete alizindua ghala la mahindi ambalo litahifadhi tani 5,000 za mahindi ya ukanda huo, ambayo awali yalikosa hifadhi kutokana na kuongezeka kwa mavuno msimu huu.

Waliokula fedha za WAZAZI matatani


NA SHAABAN MDOE, ARUSHA
JUMUIA ya Wazazi Tanzania, imeahidi kupeleka timu ya wakaguzi wa hesabu ili kubaini chanzo cha madeni yanayoikabili Shule ya Sekondari ya Leguruki, mkoani hapa. 
Madeni hayo yanatokana na na baadhi ya watumishi waliojinufaisha na fedha za shule hiyo na kisha kutoroka na kuiacha ikiwa na madeni lukuki.
Katibu wa Wazazi Mkoa wa Arusha, Daniel Mgaya, alisema tayari makao makuu ya jumuia wameshakubali kutuma timu hiyo baada ya kumalizika kwa sikukuu ya Idd el Fitri. Aliwaomba watumishi wa shule hiyo kutoa ushirikiano kwa timu hiyo itakapofika shuleni hapo.
Alisema kabla ya ufisadi uliofanywa na baadhi ya watumishi,  shule hiyo ilikuwa na uwezo wa kujiendesha pasipo kutegemea mchango wowote kutoka nje, hivyo kusisitiza  kwamba hawatakuwa tayari kuona  ikiadhirika wakati inajulikana wazi watu walioifikisha mahali hapo.
Pia aliwatoa wasiwasi watumishi wa shule hiyo pamoja na wazazi juu ya uvumi kuwa shule imeshindwa kujiendesha na kwamba iko katika hatua za mwisho za kufungwa.
“Wazazi pamoja na walimu wangu msiwe na wasiwasi shule hii haifungwi, endeleeni kuchapa kazi na leteni watoto wenu. Ninachowaahidi  baada ya ya sikukuu hii tutatuma timu kukagua hesabu. Haiwezekani watu waibe fedha halafu wapite mitaani kutangaza shule imekufa na inafungwa,” alisema Mgaya.
Awali, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mtambo wa umeme wa jua shuleni hapo uliogharimu sh. milioni 55 kupitia ufadhili wa shirika la Energy Assistance la Ubeligiji, Mkuu wa Shule hiyo, Emanuel Loyi, alisema shule imekuwa ikishindwa kujiendesha kutokana na deni sugu la zaidi ya sh. milioni 24.
Alisema madeni hayo ameyarithi kutoka uongozi uliopita tangu mwaka 1991 ambayo ni yale ya makato ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) yaliyosababisha kufungiwa kabisa. 
Loyi aliuomba uongozi wa jumuia kupitia mgeni rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa Wazazi Mkoa wa Arusha, Bernard Murunya, kwa niaba ya Mwenyekiti wa Taifa, Abdallah Bulembo, kuandaa hafla  ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kulipa madeni hayo na mambo mengine, ikiwemo kukamilisha ujenzi wa mabweni.

Wanunua mashine za kupakilia miwa


Na Igamba Libonge, Kilombero
CHAMA cha Wakulima wa Miwa cha Msolwa Ujamaa (MUCGA), wilayani Kilombero kimenunua mashine mbili za kupakilia miwa zenye thamani ya sh. milioni 264.8.
Chama hicho pia  kwa mwaka huu kinatarajia kununua magari sita yenye thamani ya sh. milioni 400 kwa ajili ya kusombea miwa ya wanachama na kujenga ofisi mpya itakayowagharimu sh. milioni 250.
Hayo yamesemwa juzi na Mwenyekiti wa MUCGA, Sebastian Sangilindege, alipokuwa akisoma taarifa ya chama katika mkutano mkuu. Alisema hayo ni mafanikio makubwa ya chama licha ya kuanzishwa kwake mwaka 2009. 
Sangilindege alisema ununuzi wa mashine hizo hizo umerahisisha kupakiwa kwa wingi miwa ya wanachama kwa kuwa awali miwa mingi ilibaki mashambani. Pia alisema ununuzi wa magari utafanikisha kumalizwa kusombwa kwa miwa yote iliyokatwa katika mashamba.
Alitaja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na chama kurekebisha miundombinu ya barabara hasa sehemu korofi  ambazo zilikuwa hazipitiki kwa urahisi, kuokoa miwa mingi iliyoungua kwa ajali na kuzuia milipuko ya moto na kuwapatia pembejeo za kilimo wanachama wasiokuwa na fedha taslimu na baadaye kukatwa asilimia 10.

Monday 28 July 2014

Majambazi 10 mbaroni Dar.



NA WILLIAM SHECHAMBO
MAJAMBAZI 10 wanaounda mtandao hatari wa uhalifu nchini, wametiwa mbaroni wakati wa msako mkali uliofanikisha pia kukamatwa kwa silaha mbalimbali.
Silaha hizo ni bunduki tisa zikiwemo SMG tatu, bastola mbili, short gun nne na risasi 15 zilikamatwa.
Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliyasema hayo ofisini kwake kwenye mkutano na waandishi wa habari.
Kova aliyataja majina ya wahalifu hao kuwa ni, Maulid Mbwate (23), Foibe Vicent (30), Vincent Kadogoo (30), Said Mlisi (29) na Hemed Zaga wote wakazi wa Dar es Salaam.
Wengine ni Mohamed Said (31), Lucy Mwafongo (41), Rajab Ramadhan (22), Deus Chilala (30) na Marietha Mussa (18), pia wa Dar es Salaam.  
Alisema kutokana na matukio kadhaa ya kihalifu likiwemo la wizi kwenye benki ya Stanbic tawi la Kariakoo Sokoni, polisi imejizatiti kuendelea na operesheni kabambe bila kulala.
Kova alisema mpaka sasa hakuna aliyekamatwa kuhusika na uhalifu huo uliotokea juzi mchana, na kwamba wanaendelea kuwasaka majambazi wote watano waliohusika.
Akielezea tukio hilo alisema, kutokana na upelelezi wao majambazi hao hawakuweza kuiba fedha za benki kutokana na mfumo mzuri wa usalama ulioko kwenye benki hiyo, hivyo waliiba fedha za wateja waliokuwa wakisubiri huduma ya kuweka fedha.  

"Benki ile ina 'system' nzuri ya usalama vikiwemo ving'ora na milango inayotumia kadi kwa hiyo hawakuweza kuingia ndani kunakohifadhiwa pesa. Baada ya kushindwa kufanya hivyo, watumishi wa benki wakaminya ving'ora ndipo wakakimbia na fedha za wateja," alisema Kova.

Aidha Kamanda Kova alisema kiasi cha fedha zilizoibwa kwenye wizi huo wa benki ya Stanbic hakijafahamika mpaka upelelezi utakapokamilika.
Pia alisema kutokana na tukio hilo benki zote zinatakiwa kuiga mfano huo kwa kufunga mifumo mizuri ya usalama ikiwa ni pamoja na kamera, mashine za kutambua chuma ambayo hutambua silaha kama visu na bunduki mara mtu anapoingia nazo ndani ya benki husika.
Kwa kuongezea Kova alisema jeshi la polisi linaruhusu benki yoyote kuingia mkataba nao ili badala ya kulindwa na kampuni za ulinzi, ziweze kulindwa na jeshi hilo ambapo ulinzi huwa thabiti na matukio ya kihalifu kama hayo huwa hayatokei mara kwa mara.
Kuhusu sikukuu ya Idd el Fitr, Kamishna Kova alisema vikosi vyote vya Jeshi la polisi vimejipanga kuweka ulinzi kila eneo la mkoa wa Dar es Salaam kwa kuweka vituo vya polisi vya muda sehemu ambayo havipo.
Aidha aliwataka wananchi wawe makini na matumizi ya barabara kwa kuzingatia sheria na kushirikiana na jeshi hilo kwa kutoa taarifa haraka kuhusiana na shaka yoyote wanayoweza kumtilia mtu au kitu kilichopo kwenye maeneo yao.

TEKU yatimua watatu


                                                                                    Na Solomon wansele, mbeya
WAFANYAKAZI watatu wa Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU), kilichopo jijini Mbeya, wakiwemo wahasibu, wamesimamishwa kazi kwa tuhuma za upotevu wa zaidi ya sh. milioni 300, mali ya chuo hicho.
Upotevu huo umebainika kutokana na ukaguzi wa hesabu za chuo hicho kwa kipindi cha mwaka 2012/2013.
Hata hivyo, taarifa zinaeleza kuwa upotevu wa fedha unaweza kuwa zaidi ya sh. Milioni 300 kwa kuwa hesabu za kuanzia Januari hadi Juni, mwaka huu, bado hazijafanyika.
Uchunguzi uliofanywa na UHURU umebaini wizi huo wa mamilioni hayo ya shilingi, umeibua mtafuruku mkubwa ndani ya chuo hicho huku Makamu Mkuu wa TEKU, Profesa Tully Kasimotto, akidaiwa kujaribu kulificha suala hilo.
Wakizungumza kwa masharti ya kutoandikwa majina yao, baadhi ya watumishi wa chuo hicho walisema watumishi watatu wa Idara ya Uhasibu (majina yanahifadhiwa), wameshapewa barua za kusimamishwa kazi.

"Watuhumiwa wote watatu licha ya kusimamishwa kazi, wametakiwa kuendelea kuripoti kazini kila siku, lakini hawafanyi kazi yoyote na uchunguzi zaidi unaendelea. Ni kweli kiasi hicho cha fedha kimepotea kusikofahamika, lakini kuna harufu ya kulindana katika hili,” walisema baadhi ya watumishi chuoni hapo.

Walisema fedha hizo zilizopotea ni nyingi na kwamba, zingeweza kusaidia uendeshaji wa majimbo mengine ya Kanisa la Moravian Tanzania,  inayomiliki chuo hicho.
Baadhi ya majimbo ya kanisa hilo watumishi wake wamekuwa wakikabiliwa na ukosefu wa fedha ikiwemo mishahara ya watumishi.
Majimbo hayo mbali na lile Kanisa la Moravian Tanzania (KMT) Jimbo la Kusini, ambalo ndio mama, mengine ni Jimbo la Magharibi-Tabora, la Kusini Magharibi-Mbeya, Jimbo la Rukwa, Kigoma, Arusha na lile la Mashariki na Zanzibar.
Makamu Mkuu wa TEKU, Profesa Tully alipofuatwa na gazeti hili alishikwa na kigugumizi, kwa kujichanganya katika utoaji majibu huku akisema suala hilo bado linafanyiwa kazi, na kumtaka mwandishi asiandike habari yoyote kwani uchunguzi upo hatua za awali.
Alisema bado wanaendelea kuzifanyia kazi, na kumtaka mwandishi asubirie kwanza asiiandike habari yoyote na kuwa hata Baraza Kuu la TEKU lililokutana Julai 26, mwaka huu, lilikuwa la kawaida licha ya kuwepo kwa taarifa zenye uhakika kutoka ndani ya chuo hicho kuwa suala la wizi ndio lilitawala kikao hicho.

"Subiri hadi taarifa hizi zitakapo kuwa tayari tutazitoa kwenye vyombo vya habari...msemaji wa Chuo ni mimi hivyo nakueleza hili bado lipo katika hatua za awali kabisa, sitaki kabisa uliandike.

“Unapofanya utafiti huwezi kumtuhumu mtu kuwa ameiba fedha, labda alikosea mahesabu wewe utajuaje hilo," alisema Profesa Tully na kuongeza:

"Kusimamishwa kazi kwa watumishi hao, hakuna maana kuwa wameiba fedha hizo na kuwa hata kama hilo lipo kutokana na Chuo kumilikiwa na Kanisa, basi hata watuhumiwa wanaweza kusamehewa bila ya kufikishwa mahakamani”.


Wednesday 23 July 2014

UFISADI VYAMA VYA USHIRIKA


JK: Hatutabeba mizigo ya wezi

  • Aagiza vigogo kufikishwa kortini haraka
  • Aonya fedha za umma sio za kuchezewa

Na Mwandishi Wetu, Tunduru
RAIS Jakaya Kikwete amesema serikali haitalipa madeni ambayo baadhi ya Vyama vya Ushirika nchini vinadaiwa na benki.
Amesema anataka kwanza wezi waliosababisha madeni hayo wakamatwe na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.

Aidha, Rais Kikwete amesema ni jambo la kusikitisha kuwa baadhi ya maofisa wa serikali hujidhalilisha kwa kujifanya mawakala wa wanunuzi binafsi wa mazao ya wakulima, hasa wakati wa msimu wa ununuzi huo.
Pia amewataka wana-ushirika nchini kuacha kuwachagua wezi kuongoza vyama vyao, vinginevyo itafikia hatua vyama hivyo vitakufa kabisa.
Aliyasema hayo juzi wakati alipohutubia mkutano wa hadhara na wakati alipozungumza na viongozi wa mkoa huo, ambapo aliyakataa maombi ya wananchi wa Tunduru, ambao waliomba serikali ikilipie deni la sh. bilioni 2.6, ambalo Chama cha Ushirika cha TAMCU kinadaiwa na mabenki.
“Nasikitika kuwajulisheni kuwa siko tayari kuidhinisha chama chenu kilipiwe deni mpaka ithibitike deni hilo lilitengenezwa vipi kwa sababu huko nyuma tumepata kulipa madeni yote ya Vyama vya Ushirika kwa kiasi cha kati ya sh. bilioni 27 na 30. Nataka kupata maelezo ya uhakika jinsi chama chenu kilivyopata deni hilo – je ni hasara ya kawaida ama ni wizi tu wa viongozi wa chama hicho,” alisema Rais Kikwete na kuongeza:
“Serikali haiwezi kubebeshwa deni la wezi. Sharti langu kwenu na kwa uongozi wa mkoa wa Ruvuma ni kwamba kwanza wakamatwe wezi hao na kufikishwa mbele ya sheria na ndipo tuzungumzie kama tunaweza kulipa deni hilo pamoja na kujua ukweli kwamba, serikali ndiyo ilidhamini vyama vya ushirika kukopa. Kazi ya serikali haiwezi kuwa ni kutumia pesa ya umma kulipa madeni yaliyosababishwa na watu wanaochonga line na kutengeneza madeni. Hatuwezi kufidia wezi.”
Aliongeza: “Kazi kuu ya Vyama vya Ushirika ni kulinda wakulima kwa sababu hivi ni vyama vyao, tena vyama vya hiari. Hivyo, ndiyo walikuwa wanafanya akina Mzee Kahama wa BCU, akina marehemu Bomani wa Victoria na wale wa KNCU. Sasa vyama hivyo vimekuwa sehemu ya kuwadhulumu wakulima.
“Sasa hata viongozi wa ushirika nao wamekuwa mawakala wa wanunuzi binafsi. Hata maofisa wa serikali nao wamo. Wanashinda wanazunguka vijijini huko wakati wa msimu kuwafanyia kazi wanunuzi binafsi. Ni jambo la kusikitisha. Hii ndiyo inaeleza kwa nini mfumo wa Stakabadhi Ghalani umekuwa na maadui wengi kwa sababu maadui hao ni pamoja na maofisa wa Serikali.”

Mtikila ajipeleka mahakamani


Na Fadhili Abdallah, Kigoma
MWENYEKITI wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila, ameomba kuunganishwa katika kesi ya madai inayomkabili Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila.
Kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania (IPTL), imefungua kesi ya madai dhidi ya Kafulila katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, ikiomba aamriwe kuilipa fidia ya sh. bilioni 310 kutokana na kutangaza taarifa za kashfa dhidi yao.
Katika kesi yao ya msingi, wadai hao wanaiomba Mahakama Kuu katika hukumu yake, imwamuru Kafulila awalipe sh. bilioni 210 kama fidia kutokana na kashfa hizo na hasara ya taswira ya biashara na hadhi yao.
Awali, Kafulila akizungumza kwenye mjadala katika eneo la Urusi Mwanga mjini Kigoma jana, alisema Mchungaji Mtikila ameomba kuwa mshitakiwa wa pili katika kesi hiyo huku Chama chake cha DP kikiwa mshitakiwa wa tatu.
Pia alisisitiza kuwa kamwe hakukurupuka kuibua kashfa hiyo ya ufisadi katika akaunti ya Escrow na kwamba, yuko tayari kwa lolote.
“Nimefarijika kuona wenzangu wananiunga mkono katika mapambano dhidi ya ufisadi na Mchungaji Mtikila ameomba kuwa mshitakiwa wa pili,” alisema Kafulila.
Akizungumza na Uhuru kwa njia ya simu jana, Mchungaji Mtikila, alikiri kuwa amekubali kuunganishwa kwenye kesi hiyo inayomkabili Kafulila.
“Nimekubali kuunganishwa katika kesi hiyo ili kutetea haki ya wananchi wa nchi yetu kama Katiba inavyosema,” alisema.

CCM: Marufuku kutangaza nia ya kugombea urais


Na Ally Ndota, Zanzibar
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeonya viongozi na watendaji wake kuacha tabia ya kuwabeba wana-CCM wanaotangaza nia ya kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu ujao, kwani kufanya hivyo ni kukiuka kanuni na miongozo ya Chama.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Zanzibar), Vuai Ali Vuai ametoa onyo hilo alipokuwa akizungumza na wajumbe wa Kamati za Siasa za Mkoa na Wilaya za Kichama za Mjini na Amani, ikiwa ni mfululizo wa ziara ya wajumbe wa Sekretarieti ya Kamati Kuu ya NEC, Zanzibar.
Alisema CCM inaongozwa kwa kanuni na taratibu zinazotambulika kikatiba, hivyo hakitomvumilia mwanachama anayevunja  kanuni hizo kwa maslahi yake binafsi kwani kila jambo limewekewa utaratibu ambao unapaswa kufuatwa na kila mwanachama.
Alifafanua zaidi kuwa kila mtu ndani ya Chama anayo fursa ya kugombea nafasi za uongozi, lakini hana budi kufuata utaratibu, kwani kuna watu wameanza kuwatumia baadhi ya viongozi wa Chama kuwapigia kampeni za chini kwa chini wakati muda wa kufanya hivyo bado haujawadia.
“Ni marufuku kwa mwana-CCM kuanza kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyote hasa urais, ubunge, ujumbe wa Baraza la Wawakilishi au udiwani kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao, kwani muda wa kufanya hivyo bado haujafika,” alisema Vuai.
Aliwaagiza viongozi hao kuelekeza nguvu zaidi katika kubuni mbinu na mikakati madhubuti, ikiwemo kujipanga kikamilifu kwa madhumuni ya kuwaandaa watu wenye sifa za kupiga kura ili waweze kuleta ushindi wa kishindo kwa Chama katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Pia, aliwataka kufanya kila linalowezekana kuhakikisha majimbo matatu ya Mtoni, Magogoni na Mji Mkongwe yanakombolewa kutoka Chama cha CUF  na kuwa chini ya himaya ya CCM.
Kwa upande wao, wajumbe hao walisisitiza kuendeleza suala zima la umoja na mshikamano miongoni mwao na kuacha tofauti zao pale zilipojitokeza  ili waweze kutekeleza kikamilifu Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010, kwa maslahi yao, vizazi vyao na taifa kwa ujumla.
Wajumbe wa Sekretarieti ya Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya CCM Zanzibar, wamekamilisha ziara katika mikoa mitatu ya kichama ya Kaskazini, Kusini na Mjini, Unguja.

Sumaye: Kuna tishio la matajiri na masikini kutoelewana


NA MWANDISHI WETU
WAZIRI Mkuu mstaafu Frederick Sumaye, amesema kuna tishio la kutokea kutoelewana baina ya matajiri na masikini nchini.
Amesema hali hiyo inaweza kusababisha vurugu nchini kama hatua hazitachukuliwa mapema ili kunusuru hali hiyo.
Amesema katika jamii, kuna chuki inayotokana na tofauti kubwa ya kimapato baina ya makundi tofauti, hasa kati ya matajiri wachache na wenye madaraka kwa upande mmoja na masikini walio wengi kwa upande wa pili, ambavyo husababishwa na mfumo mbaya wa uchumi na ubinafsi uliokithiri usiojali wengine.
“Hali hii ni ya hatari kwa amani na utulivu wa taifa lolote kwa sababu walio wengi hawatavumilia kuona watu wachache wakiishi katika anasa za kutisha wakati walio wengi hawamudu hata mahitaji ya lazima kwa maisha. Hapa kwetu hali hii ipo na ni dalili isiyo nzuri, hivyo inahitajika kudhibitiwa kwa haraka kabla haijaleta madhara makubwa kwa taifa letu,” alifafanua Sumaye.
Aliyasema hayo katika salamu zake wakati wa mkutano mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati uliofanyika Sekondari ya Peace House mjini Arusha.
Sumaye alisema suala la umoja ni muhimu kwa kuwa bila umoja, hakutakuwa na nguvu na mshikamano na kila mmoja atajifanyia lake analolijua bila kujali kama lina athari gani kwa mtu mwingine, lakini mwisho wa yote wote watakuwa dhaifu.
Aliongeza kuwa siku hizi hata katika uchaguzi wa nafasi za uongozi kwenye nyumba za ibada, hujitokeza tabia ya watu kujitenga na viongozi waliochaguliwa, kwa sababu tu huyo aliyechaguliwa hakuwa chaguo lao, hali ambayo huwafanya viongozi kuongoza kwa shida.
“Kiongozi anayechaguliwa na wengi ndiye kiongozi wetu sote, hata wale ambao hatukumpigia kura. Ni lazima tuwe na umoja baina yetu sisi wenyewe na tuwe na umoja baina ya sisi na viongozi wetu, na pia umoja baina yetu sisi na binadamu wenzetu ambao tunaishi nao. Hapo ndipo tutakapofurahia matunda ya umoja wetu, yaani upendo, amani na maendeleo,” alisema Sumaye.
Alitoa mfano kuwa kuna nchi ambazo zimeingia katika hali ya uvunjivu wa amani, hata kupigana wenyewe kwa wenyewe kwa sababu hakuna umoja baina ya watu wake na kila upande ukipigania kuudhulumu mwingine au kunakuwa na chuki zimejengeka baina ya pande zinazohusika.
“Katika siasa, tofauti hizi huweza kutokea pale ambapo upande mmoja huhisi kuwa unadhulumiwa au unaonewa katika maamuzi ya kisiasa, hasa nyakati za kampeni, upigaji kura na wizi wa kura.
“Wakati mwingine hali hii hutokea kwa upande mmoja kukataa tu kushindwa hata kama wameshindwa kwa halali,” alisema na kusisitiza kuwa, jambo hilo la kisiasa limeleta fujo katika nchi nyingi za Afrika na kusababisha umwagaji wa damu.
Aliongeza kuonya kuwa, eneo lingine la hatari ni la chuki za kidini au zinazotokana na imani za watu ambalo vita vyake vibaya zaidi na huishia kuuana bila kuwa na mshindi.
Katika mkutano huo, Sumaye alimpongeza Askofu Mteule, Mchungaji Solomon Massangwa, kwa kuchaguliwa kuwa Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini Kati kujaza nafasi iliyoachwa wazi na marehemu Askofu Dk. Thomas Laizer.

Sita mahakamani kwa matukio ya ugaidi



  •  Ulinzi waimarishwa, wake wapigwa ‘stop’

NA SHAABAN MDOE, ARUSHA
ALIYEKUWA Imamu wa Msikiti wa Quba, Arusha, Jafari Lema na wenzake watano, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Arusha, wakikabiliwa na mashitaka manne ya ugaidi.
Katika mashitaka hayo, watuhumiwa wanadaiwa kuhusika na tukio la kulipua bomu katika mgahawa wa Vama na kuwajeruhi watu saba.
Mbali na Lema, washitakiwa wengine ni Shaaban Mmasa, Athumani Mmasa, Mohamed Nuru, Abdul Mohamed na Said Temba.
Wakili wa Serikali Augustino Kombe,  akishirikiana na Felix Rwetukia, waliwasomea washitakiwa hao mashitaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Rose Ngoka.
Shitaka la kwanza la kula njama linawahusu Mmasa na Lema, ambao wanadaiwa kuwa kati ya Februari na Julai, mwaka huu, walikula njama ya kutenda kosa la ugaidi.
Katika shitaka la pili, washitakiwa  wanadaiwa Julai 7, mwaka huu, usiku, katika mgahawa wa Vama, walilipua bomu  la kutupwa kwa mkono, katika mgahawa wa Vawa  na kusababisha madhara kwa watu saba.
Mmasa na Lema wanadaiwa pia kugawa mabomu kwa ajili ya kutekeleza tukio la ugaidi.
Katika shitaka la nne la kufadhili fedha kwa ajili ya ulipuaji wa bomu kwenye mgahawa huo, linawakabili Lema, Mohamed na Temba,  ambao wanadaiwa walifadhili fedha kwa ajili ya kufanya uhalifu.
Washitakiwa hao hawautakiwa kujibu lolote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka  kusikiliza shauri hilo.
Wakili Kombe alidai upelelezi wa shauri hilo haujakamilika na kuomba shauri hilo kuahirishwa.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Agosti 6, mwaka huu na washitakiwa walirudishwa rumande.
Wakati watuhumiwa hao wanafikishwa mahakamani jana, ulinzi uliimarisha  katika eneo la mahakama.
Washitakiwa  walipelekwa mahakamani wakiwa katika magari mawili tofauti  ambayo yalitembea barabarani kwa kupiga ving’ora na kuomba njia.
Kutokana na kesi hiyo, mahakama ililazimika kuendesha kesi nyingine asubuhi sana  kwa kuhofia mkusanyiko mkubwa wa watu mahakamani hapo.
Watuhumiwa hao walifikishwa mahakamani saa  7.26 mchana, ambapo kulikuwa kimya huku kukiwa na watu wachache.
Katika hatua nyingine, wanawake watatu walitimuliwa mahakamani hapo baada ya kujitambulisha kuwa ni wake wa washitakiwa.
Wanawake hao walidai walifika mahakamani kwa ajili ya kuwapa waume zao nguo za kubadilisha wawapo lupango.

Mbasha akana kumbaka shemejiye


NA SYLVIA SEBASTIAN
MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala, jana ilisikiliza maelezo ya awali dhidi ya Emmanuel Mbasha, anayekabiliwa na shitaka la kumbaka shemeji yake.
Mbasha, alikana maelezo yote yaliyotolewa mahakamani hapo yaliyokuwa yakielezea jinsi alivyotenda kosa.
Akisaidiwa na Wakili wake, Mathew Kakamba, Mbasha alidai mahakamani kuwa hakuhusika kwenye matukio yote mawili ya ubakaji.
Mtuhumiwa huyo alikana kutenda kosa hilo, wakati upande wa jamhuri ulipokuwa unatoa maelezo ya awali jana, mbele ya Hakimu Wilberforce Luhwago.
Mbasha (32) ambaye ni mume wa  mwimbaji wa nyimbo za Injili, Flora Mbasha, anadaiwa kumbaka shemeji yake (jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka 17.
Mapema akisoma maelezo hayo, Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga, alidai Mei 23, mwaka huu, wakati mke wa Mbasha hakuwepo nyumbani, mtuhumiwa alifanikiwa kufanya mapenzi na msichana huyo.
Ilidaiwa kuwa baada ya kumbaka, alimwambia asiseme kwa mtu yeyote.
Alidai mara ya pili, Mei 25, mwaka huu, alimtaka amsindikize kumtafuta Flora, wakati wanarudi, alimbaka tena wakiwa ndani ya gari.
Wakili huyo alidai Mei 26, mwaka huu, mlalamikaji alitoa taarifa katika kituo cha Polisi Oysterbay na kupewa fomu namba tatu ya polisi (PF3) na kwenda katika Hospitali ya Amana, ambapo ripoti ya daktari ilibaini msichana huyo aliingiliwa.
Katuga alidai baada ya mshitakiwa kufahamu kuwa taarifa ziko polisi alitoweka nyumbani kwake na alikamatwa Juni 16, mwaka huu na kupandishwa kizimbani Juni 17, mwaka huu.
Hakimu Luhwago aliahirisha shauri hilo hadi Agosti 22, mwaka huu kwa ajili ya kuanza kusikiliza upande wa Jamhuri, ambapo watakuwa na mashahidi wanne. Mshitakiwa yuko nje kwa dhamana.

Kigogo kortini kwa uhujumu uchumi


NA SOLOMON MWANSELE, MBEYA
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mkoa wa Mbeya, imempandisha kizimbani, Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya Mbeya, Gerishon Bwire.
Bwire anakabiliwa na makosa matatu tofauti, ambayo ni kutumia nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri wake, ubadhirifu na kuisababishia hasara mamlaka.
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU, Nimrod Mafwele, alidai mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa Mbeya, James Mhanusi, kuwa Bwire alifanya makosa hayo  Mei mwaka jana, akiwa ni mtumishi wa umma.
Mafwele alidai katika shitaka la kwanza, Bwire alitumia nyaraka za serikali kumdanganya mwajiri wake ambaye ni halmashauri ya wilaya ya Mbeya na kujipataia fedha kinyume cha kifungu 22 cha sheria ya TAKUKURU namba 11 ya mwaka 2007.
“Mshitakiwa akiwa ni mhasibu wa halmashauri ya wilaya ya Mbeya, alitumia risiti yenye namba 0009, iliyoandikwa jina la Rich & Mrs Mufat Decoration na kuidhinisha malipo ya mapambo yenye thamani ya sh. 1,350,000 wakati si kweli,” alidai Mafwele.
Alilitaja kosa lingine kuwa ni ubadhirifu , kinyume cha kifungu cha 28(1) namba 11 cha mwaka 2007, ambapo mshitakiwa  alijipatia kiasi cha sh. 1,350,000 alichokabidhiwa na halmashauri ya wilaya ya Mbeya.
Katika shitaka la tatu, mshitakiwa huyo anadaiwa kuisababishia hasara mamlaka kinyume cha vifungu namba 10(1),(i),57(1) na 60(2) vya sheria ya uhujumu uchumi namba 200,  iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002, ambapo halmashauri ilipata hasara ya sh. 1,350,000.
Mshtakiwa alikana mashitaka yote huku huku upande wa mashitaka ukidai kukamilisha upelelezi na  kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kusikiliza maelezo ya awali.
Kesi iliahirishwa hadi Julai 25, mwaka huu kwa ajili kusikiliza maelezo ya awali.
Hivi karibuni TAKUKURU mkoani hapa, iliwafikisha mahakamani Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Upendo Sanga  na watumishi wengine wanne kwa kosa la kuhujumu uchumi, ambapo kesi hiyo bado inaendelea.

‘Tuna imani na Askofu Massangwa’


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
WAUMINI wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Kati, wamesema  Askofu Mteule Solomon Massangwa ni chaguo la Mungu na hawana shaka naye.
Massangwa alichaguliwa juzi, kuwa Askofu wa Dayosisi hiyo baada ya kupata kura 261 kati ya kura 263, sawa na asilimia 99.98 na msaidizi wake,  Mchungaji Gidion Kivuyo alipata kura 242 kati ya kura 263.
Uchaguzi huo ulifanyika juzi, katika Shule ya Sekondari Peace House iliyoko Kata ya Mtevesi wilayani, Arumeru.
Muunini wa dayosisi hiyo Methew Mollel alisema wajumbe waliompigia kura Massangwa wametimiza sauti ya Mungu kwa kuwa na imani kubwa na mteule huyo bila ya kutia shaka yoyote katika utendaji kazi wake.
Alisema anaimani kubwa sana na utendaji kazi wake kwani kwa kipindi cha siku zaidi ya 532 amekuwa akikaimu nafasi hiyo na amefanya mambo makubwa, ikiwa ni pamoja na kuwanganisha waumini wa kanisa hilo.
Askofu huyo amechaguliwa kuziba nafasi iliyoachwa na Askofu Thomas Laizer, aliyefanyika dunia Februari 6 mwaka huu.

Tuesday 22 July 2014

Mpango mpya wa mafao wakataliwa


NA RABIA BAKARI
BAADHI ya vyama vya wafanyakazi nchini, vimepinga mchakato wa serikali ulioanza wa mapendekezo ya kuimarisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii,  unaokwenda sambamba na mapendekezo ya kupunguza viwango vya sasa vya mafao kupitia Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA).
Vimesema mchakato huo unakiuka haki za wafanyakazi kwa kuwa muda mrefu wafanyakazi nchini wamekuwa wakilalamikia mapato madogo kutokana na kodi kubwa inayotozwa kwenye mishahara yao pamoja na mafao duni .
Wakizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba na Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu nchini (THTU), Yusuph Singo, walisema vyama vyao vinakubaliana kwamba kuna baadhi ya mifuko hiyo ipo katika hali mbaya kifedha, lakini suluhisho si kupunguza  malipo ya wastaafu.
Kwa upande wa Mukoba, alisema hakuna mahala ambapo vyama vya wafanyakazi na SSRA walikubaliana kwa niaba ya wafanyakazi kuhusu mchakato wa kubadili mfumo wa ukokotoaji wa mafao, hivyo vyama hivyo vinashangaa kusikia eti walikuwa na makubaliano na SSRA.
Alitaja kiwango kilichopendekezwa kupunguzwa kwenye malipo ya pensheni ya mkupuo yanayolipwa na mifuko ya PSPF na LAPF kuwa ni kutoka asilimia 50 hadi asilimia 33.3.
Aliongeza kuwa mapendekezo hayo hayakubaliki kwani viwango vya asilimia 50 ndivyo vinafaa kubakia kwa sasa.
“Mpango huu kama utatekelezwa, utapunguza kiinua mgongo cha walimu na watumishi wengine zaidi ya nusu ya kile wanachopata kwa sheria iliyopo sasa.
“Mtumishi aliyefanya kazi kwa miaka 55 na akastaafu akiwa na mshahara wa sh. 2,445,000, kwa utaratibu  wa sasa, anastahili kulipwa sh.176,855,000 kama mkupuo na pensheni ya kila mwezi kuwa sh. 950,000, lakini kwa mapendekezo mapya ya SSRA, mtu huyo atalipwa mkupuo wa sh. milioni 77,758,543 na malipo ya pensheni kila mwezi sh. 1,052,489 sawa na ongezeko la sh. 100,000,” alisema.
Alisema sababu ya mapendekezo hayo ya kuwa mifuko ipo kwenye hali mbaya, inapingwa na wafanyakazi na kuitaka serikali isitishe mpango huo na kutafuta njia nyingine ya kukabiliana na tishio lolote kwa afya ya mifuko hiyo.
Akizungumzia msimamo wa wanachama wake, Singo alisema kutokana na hali tete inayojitokeza kwenye mifuko hiyo na malalamiko ya muda mrefu ya viwango duni vya mishahara, wanatoa wito kwa wafanyakazi wote nchini kutafakari upya kama mfumo wa sasa wa uwakilishi katika masuala mbalimbali muhimu unakidhi matarajio yao.

Dengue yaua watu 25,000 kila mwaka


Na Selina Wilson
WATU 25,000 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na ugonjwa wa homa ya dengue ulioenea katika nchi 110 duniani, ikiwemo Tanzania.
Hayo yalisemwa jana mjini Dar es Salaam na Mtaalamu wa Udhibiti na Ufuatiliaji Magonjwa wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Geofrey Mchawa, katika mafunzo ya siku moja ya waandishi wa habari za afya kuhusu ugonjwa wa dengue.
Alisema takwimu zinaonyesha kuwa watu 50 hadi 390 wanaambukizwa ugonjwa huo kila siku duniani na kwamba kwa hapa nchini, wapo waliougua na kupoteza maisha
Hata hivyo, alisema bado hakuna chanjo wala tiba ya kutibu virusi vya ugonjwa huo,
badala yake mgonjwa hutibiwa magonjwa yaliyojitokeza baada ya kuambukizwa dengue.
Alisema mara nyingi mgonjwa hutibiwa homa kwa dawa za kutuliza maumivu kama vile paracetamol na kwamba hatakiwi kupatiwa dawa kali zinazoweza kuleta madhara.
Akizungumzia hali ya ugonjwa huo nchini, Dk. Vida Makundi, alisema katika kipindi cha wiki moja sasa, hakuna mgonjwa aliyeripotiwa kuugua ugonjwa huo.
Dk. Vida alisema ugonjwa wa dengue ulisababisha vifo vya watu wanne, akiwemo daktari mmoja kabla ya wizara kuchukua hatua za kuudhibiti.
Alisema ugonjwa huo huambukizwa na mbu aina ya aedes, mwenye virusi vya dengue kwa kumng’ata mtu.

Massangwa apendekezwa kumrithi Askofu Dk. Leizer


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
WAJUMBE  wa Halmshauri Kuu ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Kati, wamependekeza jina moja la mchungaji Solomon Massangwa kuwa Askofu wa kanisa hilo.
Uamuzi huo ulifikiwa juzi usiku katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa shule ya sekondari ya Peace House iliyoko kata ya Matevesi wilayani Arumeru mkoani Arusha.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho zilisema kuwa, jina la Mchungaji Massangwa, ambaye alikuwa Kaimu Mkuu wa Dayosisi hiyo, ndilo lililopendekezwa na kikao cha Halmashauri Kuu na kupelekwa katika mkutano mkuu wa 23 wa Dayosisi wenye wajumbe 300 kwa ajili ya kuthibitishwa.
Uchaguzi huo unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa Askofu wa Dayosisi hiyo, Dk. Thomas Laizer, ambaye alifariki dunia Februal 6, mwaka jana, baada ya kuugua ugonjwa wa shinikizo la damu katika hospitali ya rufani ya Selian iliyoko Arusha.
Vyanzo vya habari viliendelea kusema kuwa, majimbo matano ya Dayosisi hiyo ya Arusha Mashariki, Arusha Magharibi, Maasai Kusini, Maasai Kaskazini na Jimbo la Babati, yote yalipendekeza jina moja la Mchungaji Massangwa kurithi kiti hicho alichokiacha marehemu Askofu Laizer.
Habari zilisema kutokana na hali hiyo, kikao cha Halmshauri Kuu cha Doyosisi hiyo kiliamua kwa kauli moja kupeleka jina moja katika mkutano mkuu huo ili kuthibitishwa.
“Tumeazimia kupeka jina moja la Mchungaji Massangwa katika mkutano mkuu, ambalo linaonekana kupendekezwa na majimbo yote matano mkuu ya dayosisi yetu,” kilisema chanzo chetu.
Aidha chanzo hicho cha habari kilisema kuwa, kazi kubwa itakayofanyika katika mkutano huo mkuu ni kupitisha jina la Masangwa kwa kuwa ameonekana kuwa chaguo la majimbo yote matano na hakuna malalamiko yeyote yaliyopatikana.
“Tunashukuru Mungu wachungaji  wote wameonekana kuridhika na jina hilo bila kuonyesha dalili zozote zile kuwa wamebaguliwa kwa njia moja au nyingine katika mchakato uliofanywa na majimbo yote, wote wanaonekana kuridhika,”alisema mtoa taarifa wetu.
Awali, wajumbe wa mkutano huo walionekana kuwa na shauku kubwa ya kusubiri majina yatakayoletwa katika mkutano huo kwa lengo la kupigiwa kura.
Mkuu wa wilaya ya Arusha, John Mongella, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo, alisema serikali inatambua mchango wa kanisa katika kusaidia jamii, hasa katika nyanja za kijamii.
Alisema matarajio ya serikali ni kuona kuwa, mrithi wa marehemu Askofu Laizer atakuwa sio tu kiongozi wa kanisa, bali ni kiongozi wa jamii husika .
Hadi gazeti hili linakwenda mtamboni, jina la Mchungaji Massangwa bado lilikuwa halijapata baraka za mkutano huo mkuu kuwa askofu wa Dayosisi hiyo