Thursday 17 April 2014

Kilimo kiwe cha tija-Serikali


NA SHAABAN MDOE, ARUSHA 
SERIKALI imewataka  wakulima nchini kuhakikisha kilimo chao kinakuwa chenye tija na kuondokana na kilimo cha mazoea ili kuwezesha sekta hiyo ya kilimo kukua kutoka asilimia nne ya sasa na kufikia asilimia sita inayotakiwa kitaifa.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Nkuvililwa Simkanga alitoa wito huo jana alipokuwa akizungumza na wakulima wa mbogamboga, matunda na viungo wa kikundi cha Umoja cha Midawe wakati wa uzinduzi wa kituo cha kuhifadhia mazao kilichopo kijiji cha Midawe kata ya Bang’ata wilayani Arumeru.
Alisema sekta ya kilimo inachangia asilimia 24 ya pato zima la taifa huku ikiwa inatoa ajira kwa zaidi ya asilimia 75, hivyo ili kuongeza pato zaidi, kilimo cha tija kinahitajika ili kuweza kufikia aslimia sita itakayowezesha nchi kupata chakula cha kutosheleza.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya  Chama cha
Wakulima wa Mbogamboga, Maua, Matunda na Viungo (TAHA) , Erick Ng’umanyo alisema  wakulima wengi wamekuwa wakikabiliwa na changamoto, lakini hawana chombo maalumu cha kuwasemea ,hivyo wao kama TAHA ndio wasemaji wakubwa wa wakulima hao.
Alisema uwepo wa kituo hicho ni baada ya kuchukua jukumu la kwenda wizara ya viwanda na biashara kutokana na wakulima hao kupeleka ombi hilo la changamoto ya ukosefu wa sehemu ya kuhifadhia mazao yao .
Alifafanua kuwa, baada ya wao kuwasemea wizarani, ndipo wizara ya viwanda na biashara ilipochukua jukumu la ufadhili wa jengo hilo kwa kushirikiana na TAHA na hatimaye kuweza kuwasaidia wakulima hao kuondokana na changamoto hiyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru