Friday 25 April 2014

Tuenzi mawazo ya waasisi - Pinda


NA THEODOS MGOMBA, DODOMA
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, amewataka Watanzania kuendelea kuenzi mawazo ya waasisi wa taifa, katika kudumisha Muungano wa serikali mbili, uliopo hivi sasa.
Pinda alisema, hayo jana alipokuwa akichangia katika mkutano wa Bunge Maalumu la Katiba.


Pinda alisema, Muungano uliopo wa Nchi mbili za Zanzibar na Tanganyika ni muungano tofauti na wa kipekee.
Alisema, hata waasisi wa serikali hizo walifikiri kwa kina ndiyo maaana wakaamua kuweka Muungano uliokuwa unafanana na mazingira ya Watanzania.
Huu ni Muungano tofauti na mingine iliyopo na ndiyo maana unasifiwa na nchi mbalimbali hivyo ni vyema ukalindwa,alisema.
Aliongeza kuwa ingawa Muungano una kero mbalimbali, lakini bado ni muhimu kuwepo na wala muundo wa serikali tatu hauwezi kupunguza kero hizo.
Pinda alisema suala ya kero za Muungano kwa kiasi kikubwa limeshughulikiwa, kwani kwa sasa kero hizo zimepunguzwa kutoka 31 hadi kufikia sita.
"Mimi naamini vyovyote mtakavyosema, kama ni serikali tatu au nne, lakini kero hazitakwisha kwani kila siku kero zinajitokeza kutokana na mazingira yaliyopo,íí alisema .
Alisema, binafsi anashangwaza na watu wanaodai uwepo wa Tanganyika na kuhoji kuwa hiyo Tanganyika imetoka wapi.
Akizungumzia katiba, Waziri Mkuu alisema ni vyema wajumbe wa UKAWA wakarudi bungeni ili kuendelea na utungaji wa katiba hiyo kwani wananchi wanategemea kupata katiba hiyo.

Kingunge alonga
Akizungumzia katiba,  Mjumbe wa bunge hilo, Kingunge Ngombale Mwiru, alisema ni lazima katiba ijayo ilinde mafanikio ya Muungano yaliyopatokana katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.
Alisema, katika kipindi hicho chini ya muungano wa serikali mbili kumekuwa na mafanikio mengi katika nchi hizo mbili.
Kingunge alisema katika katiba ya sasa kuna mambo ambayo hayamo nayo ni vyema yakaangaliwa ili yawepo katika katiba mpya ijayo.
Alisema jambo la msingi  ni kuhakikisha kuwa mambo ya msingi yanaingizwa katika katiba mpya ijayo jambo kubwa likiwa, ni jinsi gani Watanzania wataondokana na umasikini.
Kwa mujibu wa Kingunge, hivi sasa zaidi ya Watanzania milioni 15 wanaishi chini ya dola moja kwa siku na wengine chini ya hapo.
"Ni lazima katiba ijayo ikazingatia pia makundi yote wakiemo wafugaji, wakulima na wavuvi kwani nao katika katiba ya sasa wamesahaulika,íí alisema.
Hata hivyo,  alisema ni vyema kukafanyika mazungumzo kati ya viongozi wakubwa na wengine  ili kuhakikisha kuwa kunapatikana maelewano na maridhiano ili katiba iweze kupatikana.
Pia mjumbe huyo alisema, si vyema kumtusi aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Marekebisho ya Katiba, Jaji Joseph warioba.
Alisema kitendo cha baadhi ya wajumbe kumshambulia mwenyekiti huyo si  chema kwani hakuwa pekee yake.
Alisema baadhi ya wajumbe wamekuwa wakimshambulia Jaji Warioba kwa kutumia msimamo wa chama jambo ambalo ni sawa na kuwatukanisha wanachama wote.
 Kwa upande wa Makamu wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi wa Zanzibar, balozi Seif Ali Idd, alisema Muungano wa sasa unafaida kubwa kwa wananchi wa pande zote mbili za Muungano.
Alisema hivi sasa wananchi wa pande hizo mbili wamekuwa ndugu huku wakiishi kila upande wa Muungano bila tatizo. Bunge hilo Maalumu la Katiba limeahirishwa hadi Agosti 5, mwaka huu ambako litaendelea na vikao vyake kwa muda wa siku 60.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru