Tuesday 24 December 2013

Heroin yawatupa selo vijana wanne


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
VIJANA wanne wanashikiliwa na polisi baada ya kukamatwa eneo la Elikyurei, wilayani Arumeru, wakiwa na dawa za kulevya aina ya heroin.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi, saa 12.30 jioni, wakiwa na gramu 100 za dawa hizo, ambazo zingeuzwa sh. milioni 10 zingepatikana.
Kamanda Sabas aliwataja vijana hao kuwa, Seif Bakari (28), Hamid Makame (29), Evance Gidion (29), mkazi wa Ngarenaro na Abraham Hamis (23) wa Kaloleni.
Alisema kukamatwa kwao kunatokana na taarifa kutoka kwa wasamaria wema.
Sabas alisema watuhumiwa walikamatwa wakiwa ndani ya chumba cha mmoja wao, wakiwa wametengeneza kete 25 za dawa hiyo.
Alisema polisi wanaendelea kuwahoji watuhumiwa na uchunguzi utakapokamilika watafikishwa mahakamani.
Wakati huo huo, watu wanne wamekamatwa eneo la daraja la Engotooleshokopeyi, wilayani Ngorongoro, wakiwa na bunduki iliyofutwa namba aina ya SMG, ikiwa na risasi tano.
Aliwataja waliokamatwa kuwa, Papai Tooko (40), Leshnga Mawoi (45), Silanga Olesitoi (42) na Sombe Ngaina (30).


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru