Saturday 28 December 2013

Kinondoni yaibua kidedea Dar


NA JUMANNE GUDE
MANISPAA ya Kinondoni imeongoza kutoa wanafunzi wengi waliofaulu na kujiunga na kidato cha kwanza mwakani katika mkoa wa Dar es Salaam.
Wanafunzi waliofaulu mtihani katika manispaa tatu za mkoa wa Dar es Salaam wako 46,648 ambapo kwa Kinondoni watakaojiunga kidato cha kwanza mwakani ni asilimia 80, ikifuatiwa na manispaa Ilala yenye asilimia 75 huku Temeke ikitoa asilimia 70.
Akitoa taarifa ya uchaguzi wa wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani mkoani humo, Ofisa Elimu wa Mkoa huo, Raymond Mapunda, alisema wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka huu walikuwa 63,378 ambapo kati yao 46,468 wamefaulu.
Mapunda alisema wanafunzi waliochaguliwa katika chaguo la kwanza kujiunga na kidato cha kwanza wako 34,852, huku wanafunzi 11,796 wakikosa nafasi ambapo watasubiri chaguo la pili.
Alisema wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na shule za ufaulu mzuri wako 70 ambapo wasichana ni 36 na wavulana wako 34, wakati wanafunzi waliochaguliwa kujiunga katika shule za ufundi wako 76.
Pia, Mapunda alisema wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na shule za bweni ambazo kwa vijijini ni 41, huku shule zinazomilikiwa na Mkoa wa Dar es Salaam wamepelekwa wanafunzi 1,892.
Alisema wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na shule za serikali za wananchi wako 32,773 ambapo Manispaa ya Kinondoni ina wanafunzi 12,218 huku Temeke wanafunzi wakiwa 11,179 na Ilala wako 9,376.
Naye Katibu Tawala wa Mkoa huo, Theresia Mmbando, alisema mkoa humo umebaini wanafunzi wanafaulu kutoka katika shule za msingi za mijini.
Alisema ifikapo Februari 15, mwakani, manispaa hizo zinapaswa kuwasilisha taarifa ya hali halisi ya wanafunzi wote walioripoti ili waandae chaguo la pili mapema kujaza nafasi zilizoachwa wazi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru