Thursday 19 December 2013

Katibu wa CCM Iringa afariki dunia



NA MOI DODO, UoI
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimepata pigo baada ya Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Emmanuel Mteming’ombe, kufariki dunia usiku wa kumkia jana.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Jesca Msambatavangu, alisema Mteming’ombe alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa pumu uliosababisha kifo chake.
“Ni ugonjwa aliokuwa nao kwa muda mrefu tangu utotoni, lakini haukuwahi kumsumbua kwa muda mrefu,” alisema Jesca.
Alisema wanachama wa CCM wameupokea msiba huo kwa mshituko mkubwa kutokana na kumpoteza kiongozi mahiri na makini na kwamba, alikitumikia Chama hadi dakika ya mwisho ya uhai wake.
“Ni pigo kwa Chama mkoa na taifa, tumempoteza mpiganaji wa kweli na aliyekuwa akijituma kipindi chote kukiimarisha Chama. Ila yote ni mipango ya Mungu kwahiyo hatuna budi kukubali,” alisema.
Alisema mwili wa marehemu utasafirishwa leo kwenda kijijini kwao Rujewa wilayani Mbarali, ambapo mazishi yake yatafanyika kesho.
“Kila kitu kimekamilika na baada ya Misa ya kumuombea itakayofanyika katika Kanisa Katoliki la Kihesa tutausafirisha mwili mpaka Rujewa tayari kwa maziko kesho,” alisema Jesca.
Baba mzazi wa marehemu, Mzee Yustin Mteming’ombe, alisema kifo cha mwanae kimeacha pengo kubwa kwake na kwa familia.
“Kifo hiki kimenipa wakati mgumu mno. Alikuwa tegemeo langu, licha ya kuwa mtoto, lakini alikuwa rafiki yangu,” alisema Mteming’ombe.
Marehemu ameacha mjane, watoto wanne na wajukuu watatu.
Kutokana na msiba huo, Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Iringa, Tumaini Msowoya, ameahirisha ziara yake iliyokuwa imepangwa kuanza jana.
Ziara hiyo ilikuwa na lengo la kuboresha na kuimarisha uhai wa Chama na Jumuia ya Vijana.



Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru