Wednesday 18 December 2013

Ulaji usiofaa hatari kwa afya


ULAJI usiofaa, matumizi ya pombe kupita kiasi na kutofanya mazoezi husababisha magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
Magonjwa hayo ni ya moyo na mishipa ya damu, saratani, kisukari, magonjwa sugu ya njia ya hewa, kuoza meno na magonjwa ya fizi.
Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid, alisema hayo bungeni jana alipojibu swali la Dk. Maua Daftari, aliyetaka kujua athari za ulaji pipi na ushari wa kitaalamu kwa Bunge ili kutafuta kitu kingine mbadala wa pipi wanazotoa kwa wabunge.
Dk. Seif alisema ulaji pipi na vyakula au vinywaji vyenye sukari ni kiashiria hatarishi cha ulaji usiofaa na husababisha madhara mwilini.
Alisema mgonjwa wa kisukari anapokula pipi anaongeza sukari zaidi mwilini, ambapo tayari mwili unashindwa kutumia sukari iliyopo.
Naibu waziri alisema mtu wa aina hiyo anaongeza uwezekano wa kupata matatizo yatokanayo na sukari kama vile figo kushindwa kufanya kazi, magonjwa ya moyo na mishipa ya fahamu na macho.
Dk. Seif alisema kwa kuwa ulaji pipi unaleta athari kwa meno, ni vyema watumiaji wakapiga mswaki kwa kutumia dawa za meno zenye ‘floraidi’ baada ya kutumia vyakula vyenye sukari.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru