Saturday 21 December 2013

Wahamiaji haramu warejea, wajiita M23

Na Angela Sebastian, Kyerwa
SERIKALI imewataka wahamiaji haramu waliorudi nchini huku wakijiita M23 na ‘kuteka’ Kijiji cha Kibingo, wilayani Kyerwa, huku wakiendelea kutoa vitisho kwa wananchi, kuondoka mara moja.
Wahamiaji hao ambao wamerejea baada ya kutoa hongo kwa baadhi ya viongozi wa vijiji wasiokuwa waadilifu, wamekuwa wakiwasumbua wananchi katika eneo hilo.
Mkuu wa mkoa wa Kagera, Fabiani Massawe, amewataka watu hao kuondoka haraka alipofanya ziara wilayani humo na kumtaka Mkuu wa Wilaya, Benedict Kitenga, kutoa taarifa juu ya maendeleo ya oparesheni kimbunga awamu ya nne katika eneo lake.
ìNimepata taarifa kutoka kwa wananchi kuwa wahamiaji haramu wamerudi kwa nguvu na wanawatisha kwa kuwaeleza kuwa watawaua, serikali haitavumilia watu hao waendelee kuwatisha wananchi.
“Naagiza Kamati za Ulinzi na Usalama hususan Usalama wa Taifa kufanya uchunguzi na kuweka mtandao ambao utatoa taarifa zitakazowezesha kuwakamata na kuwafikisha katika vyombo vya sheria wahamiaji haramu hao kwa kosa la ujambazi. Kwa kweli hatuwezi kuwaita wahamiaji haramu, bali hawa ni majambazi,îalisema Massawe kwa ukali.
Alisema Rais Jakaya Kikwete alitoa sh. bilioni 3.6 na kutuma vikosi vya ulinzi na usalama mkoani Kagera ili waondoe wahamiaji haramu, majangili na majambazi wa kutumia silaha.
“Leo akisikia wamerudi tena hii ni aibu. Nawataarifu wahamiaji hao kuwa oparesheni hii ni endelevu kwa hiyo hakuna wa kubaki wala kurudi kama kauli mbiu yetu inavyosema,îalisema mkuu huyo wa mkoa.
Alisema kiongozi yeyote kuanzia ngazi ya kata hadi mkoa atakayeonekana kuwakingia kifua wahamiaji hao kwa kuchukua fedha na mifugo, atashitakiwa kwa kosa la usaliti wa taifa.
Aliwataka wananchi kuwa wazalendo kwa kutoa taarifa pindi wanapowaona watu hao katika vyombo husika na pia kupitia simu yake ya mkononi ili waweze kushughulikiwa.
Kwa upande wake, Kitenga alisema serikali kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama walipata taarifa wahamiaji haramu wamerudi kwa kasi katika kijiji hicho na kuteka eneo la kijiji hicho huku wakijiita M23 wakiwa na silaha za jadi.
Alizitaja silaha hizo kuwa mikuki, mapanga, visu na marungu ambavyo walivitumia kuwatisha wananchi na watendaji wa maeneo hayo kuwa wakiwasema watawajeruhi.
ìTulienda mpaka kijijini hapo na tulipofika katika eneo walilokuwa wamejimilikisha tulifanikiwa kukuta wahamiaji haramu zaidi 20 kutoka nchi za Uganda na Rwanda waliokuwa katika harakati za kutafuta chakula wakiwa na silaha hizo ila tulifanikiwa kuwakamata wote na kuwarudisha kwao na kuwanyangíanya silaha hizo, “ alisema mkuu huyo wa wilaya.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, George Mikindo, alisema viongozi wa maeneo hayo ndio wanaowalea wahamiaji haramu hao.
“Kwa hiyo inakuwa shida sana kuwajua kwani hawatoi ushirikiano kwa sababu viongozi hao hao wamekuwa wakiwafuata  wahamiaji hao haramu Rwanda na kuwarudisha nchini  ili wawachungie mifugo,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru