Wednesday 18 December 2013

Sheria ya mitandao kuanza rasmi Machi


NA MOHAMMED ISSA
SERIKALI imesema sheria ya kudhibiti uhalifu wa mitandao inatarajia kuanza kutumika Machi, mwakani.
Imesema sheria hiyo itadhibiti uhalifu wa mitandao ambao umekithiri nchini.
Pia, imesema inakamilisha ujenzi wa mtambo wa kudhibiti mawasiliano ya nje na ndani ya nchi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Patrick Makungu, alisema tatizo la uhalifu wa mitandao ni kubwa.
Alisema bila kudhibitiwa, linaweza kusababisha athari kwa taifa na jamii.
Alisema sheria hiyo itapunguza na kudhibiti vitendo vya uhalifu vinavyofanywa na baadhi ya watu kupitia mitandao mbalimbali.
Profesa Mangu, alisema hayo jana mjini Dar es Salaam, alipokuwa akifungua kikao cha wadau cha kujadili Rasimu ya Sheria ya Matumizi Salama ya Mtandao.
Alisema kutokana na kuwepo tishio la uhalifu kwenye mitandao, serikali imeamua kutunga sheria ya kudhibiti uhalifu huo na kwamba, itamtaka aliyekumbwa na tatizo hilo kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria.
“Hii sheria itatoa adhabu kwa yeyote atakayebainika kuhusika na uhalifu wa kwenye mitandao, ambao hivi sasa umekithiri,” alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA wa wizara hiyo, Dk. Ally Simba, alisema sheria hiyo itahusu pia uhalifu wa kumbukumbu, usalama wa mtandao na biashara ya mtandao.
Alisema sheria itamtaka aliyekumbwa na tatizo kutoa taarifa na asipotoa atawajibika.
Dk. Simba, alisema mkutano huo utasaidia ukamilishwaji wa sheria ya usalama wa mitandao.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru