Thursday 13 November 2014

DUCE kupunguza uhaba wa walimu


NA EMMANUEL MOHAMED


CHUO Kikuu Kishiriki cha Elimu,(DUCE), kimeanza mkakati wa kupunguza uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi nchini kwa kuongeza udahili wa wanafunzi wa masomo hayo.
Mkakati huo umeongeza wadahiliwa 1700 wa masomo hayo kwa mwaka huu, katika chuo hicho, huku kukiwa na jumla ya walimu 20,000 wa masomo hayo nchi nzima.
Hayo yalielezwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala, jana , wakati akiwakaribisha wanafunzi wa mwaka wa kwanza DUCE.
Profesa Mukandala alisema mkakati huo umeanza vizuri, kwani serikali imeanza kuboresha miundombinu ya Mfumo wa Habari na Mawasiliano, (TEHAMA) kwa lengo la kuongeza maarifa ya ziada kwa masomo hayo kwa wanafunzi.
Alisema juhudi za serikali na  DUCE imefanikiwa kujenga maabara kubwa tatu za sayansi, ili kuongeza uwezo wa mkakati huo wa kupokea  wanafunzi  wengi zaidi wa masomo hayo ya sayansi.

“Tuliomba kuongezewa idadi ya wadahiliwa  wa masomo ya sayansi kwa Taasisi ya Usajili wa Vyuo Vikuu, (TCU), kwa mwaka huu na walituunga mkono katika juhudi za mkakati huo,” alisema.

Naye Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Godliving Mtui, alisema  awali chuo  kilikuwa na uwezo wa kupokea  wanafunzi  wachache wa masomo ya sayansi, hivyo mkakati huo utapunguza uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi.
 

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru