Thursday 13 November 2014

Mabomu hatari yanaswa



NA CLARENCE CHILUMBA, MASASI
JESHI la Polisi mkoani Mtwara, linawashilkilia watu wawili kwa tuhuma za kukutwa na mabomu 18 ya kutengenezwa kwa kutumia vifaa hatari vya kupasulia miamba.
Habari za kuaminika zinasema watuhumiwa hao walikamatwa kwa nyakati tofauti kutokana na kuishi maeneo tofauti. Pia walinaswa na nyaya na unga maalumu ambao ni malighafi zinazotumika katika kutengeneza mabomu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Augustino Ullomi, alisema watuhumiwa hao walitiwa mbaroni mapema wiki hii, ambapo kila mmoja alikutwa akiwa nyumbani kwake.
Alisema watuhumiwa wote walikutwa na mabomu hayo wakiwa wameyahifadhi na kuwa kukamatwa kwao kumefanikishwa na raia wema.
Kamanda Ullomi aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Abdallah Hamisi (25) na Kibode Dua (37).
Alisema mtuhumiwa wa kwanza kutiwa mbaroni alikuwa Abdallah, ambaye baada ya kubanwa alieleza yalipo mabomu hayo na kuwa aliyapata kutoka Nanyumbu kwa Dua.
Kamanda Ullomi alisema askari walikwenda na mtuhumiwa huyo nyumbani kwa Dua na kufanikiwa kunasa mabomu mengine 17, barua, unga na nyaya zinazotumika katika utengenezaji wa mabomu hayo.
Kwa mujibu wa Kamanda Ullomi, watuhumiwa hao walipohojiwa zaidi, walidai waliyapata Tunduru mkoani Ruvuma na mengine Nachingwea mkoani Lindi.
Aliongeza kuwa baada ya uchunguzi kwa kushirikiana na wataalamu wa Jeshi la Polisi kutoka Makao Makuu, walibaini mabomu hayo ni hatari na yana uwezo wa kuuawa watu wengi kwa wakati mmoja.
Kwa mujibu wa Kamanda Ullomi, watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani wakati wowote baada ya uchunguzi kukamilika.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru