Thursday 1 August 2013

Dk. Mwakyembe afichua ufisadi mpya bandarini


NA SOLOMON MWANSELE, MBEYA
SERIKALI imetoa miezi mitatu kwa matrekta yaliyoingizwa nchini kwa ajili ya utekelezaji mpango wa Kilimo Kwanza na sasa yanabeba makontena katika Bandari ya Dar es Salaam, yawe yameondolewa.
Imeelezwa serikali ilifuta ushuru wa zana za kilimo, yakiwemo matrekta chini ya mpango wa Kilimo Kwanza, lakini mengi yameishia kufanya shughuli nyingine nje ya sekta ya kilimo.
Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, alitoa agizo hilo jana, wakati wa ufunguzi wa maonyesho ya kilimo (Nane Nane), Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, katika viwanja vya John Mwakangale, vilivyoko jijini Mbeya.
Dk. Mwakyembe alisema agizo hilo linatakiwa liwe limetekelezwa ifikapo Oktoba 30, mwaka huu, vinginevyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wote watakaokaidi.
“Hili hatuwezi kulivumilia, linavunja malengo ya serikali ya kujitosheleza katika kilimo. Matrekta mengi nimeyaona bandarini Dar es Salaam, yakitumika kubeba mizigo, yakiwemo makontena, hivyo natoa miezi mitatu yote yawe yameondolewa,” alisema.
Alisema matrekta hayo na yanayoendelea kuwepo barabarani katika maeneo mbalimbali mijini, ifikapo Oktoba 30, mwaka huu, yasiwepo.
Dk. Mwakyembe alisema atazungumza na uongozi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) na Jeshi la Polisi ili kupiga marufuku matrekta mijini, badala yake yawe mashambani kulima na kubeba mizigo.
Katika hatua nyingine, waziri alizitaka halmashauri kuondoa mambo madogo madogo yanayowakatisha tamaa wakulima.
Aliyataja mambo hayo kuwa, kodi za kukera, ambazo zinaendelea kutozwa kwa wakulima wanaotoa mazao ama shambani kwenda nyumbani au gulioni.
Dk. Mwakyembe alisema halmashauri zina wataalamu wenye ujuzi mbalimbali, lakini wanashindwa kutumia weledi na elimu yao kubuni vyanzo vipya vya mapato, ambavyo havitawakera wananchi.
Katika hatua nyingine, aliwataka wakulima wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kujiunga katika ushirika na kuviimarisha vyama vilivyoko kwa kununua hisa, kuweka akiba na amana ili kupata mitaji ya kilimo.
Alisema ushirika imara utawasaidia wanachama kupata mitaji, pembejeo za kilimo, zana bora na kutafuta masoko ya mazao ya wanachama.
TAFUTENI MASOKO NJE
Wakati huo huo, Theodos Mgomba, anaripoti kutoka Dodoma kuwa, serikali imewataka wataalamu kufikisha kwa wakulima ubunifu na majibu ya utafiti wa kilimo, badala ya kufanya hivyo kwenye maonyesho tu.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, alisema hayo jana, alipofungua maonyesho ya Nane Nane katika viwanja vya Nzuguni, mjini Dodoma.
Chiza alisema kuna utaalamu wa aina mbalimbali, ukiwemo wa nyenzo za kilimo unaoonyeshwa kwenye maonyesho, lakini hali za wakulima hazibadiliki.
Alisema jambo hilo linatoa sura kuwa, matokeo ya utafiti hayawafikii wakulima ili kuboresha kilimo.
Waziri alisema hakuna sababu ya kuendelea kuweka vikwazo katika biashara za mazao ya chakula. Alisema hivi sasa kuna ongezeko la chakula kutoka nchini kuuzwa nje na watu wa nchi jirani.
“Sioni sababu ya kuweka vikwazo katika biashara ya chakula, unapokwenda Sudan kuna chakula kingi kinachotoka nchini, lakini wanaokiuza huko si Watanzania,” alisema.
Alisema wakati umefika kwa Watanzania kutafuta masoko nje ya nchini na kuuza mazao yao.
Kuhusu ajira kwa vijana, alisema hakuna sababu ya wao kulalamikia ukosefu wa ajira, wakati ardhi kwa ajili ya kilimo ipo ya kutosha.
Chiza alisema hakuna sababu ya vijana kuandamana barabarani kudai ajira, huku wakiacha kilimo kama kazi ya wazee au watu ambao hawana elimu.
“Nitafurahi kama kuna vijana wataandamana na kuja kwangu kuomba ardhi kwa ajili ya kuanzisha kilimo kama ajira kwao,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru