Friday 9 August 2013

Serikali yatahadharishwa


SERIKALI imetahadharishwa kuweka mipaka na ukomo wa uwezo wa kampuni binafsi za ulinzi, kwenye eneo la ulinzi na usalama wa taifa katika katiba mpya.
Hatua hiyo imeelezwa itasaidia kudhibiti ulinzi na usalama wa taifa, badala ya sasa ambapo kila kampuni inajiimarisha kwa kadri ya uwezo wake, zingine zikifanya kazi nchi nzima kama vile jeshi.
Hayo yalijitokeza katika mjadala wa Rasimu ya Katiba mpya unaoendelea mjini Kibaha.
Akichangia katika sura ya 15 ya rasimu hiyo inayozungumzia ulinzi na usalama katika Jamhuri ya Muungano, mjumbe wa baraza kutoka kata ya Visiga, Dk. Eliud Eseko, alitaka katiba itamke wazi kuhusu mipaka ya kampuni hizo.
Dk. Eseko alisema ibara ya 220 ya rasimu hiyo inazungumzia taasisi za ulinzi na usalama wa taifa, hivyo pia izungumzie kampuni binafsi za ulinzi na ziwekewe mipaka.
“Kampuni hizi zinaweza kufanya kazi kwa kuwekewa masharti ya ukubwa wake ama zipangiwe mikoa au kanda ili zisiwe kubwa zikaenea nchi nzima,” alisema.
Alisema baadhi ya kampuni hizo zinaongozwa na askari wastaafu wenye uwezo mkubwa, hivyo ikitokea mambo yakaenda ovyo, zinaweza kuleta changamoto kwa majeshi nchini.
“Wasiwasi wangu ni kuwa, mtu aliyepata mafunzo jeshini na kuwa mtaalamu wa mabomu, sasa anaongoza mtandao wa walinzi binafsi nchi nzima, akiamua kuasi itakuwa kazi kubwa, hivyo nashauri kampuni hizo zibanwe zisiwe na ukubwa huo,” alisema.
Naye Tatu Jamadi, akiwasilisha maoni ya kundi E, alitaka Jeshi la Magereza na Uhamiaji, yawe katika orodha ya taasisi za ulinzi na usalama wa taifa, kwani taasisi hizo hazikutajwa.
Katika ibara hiyo, taasisi zilizotajwa ni Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi na Idara ya Usalama wa Taifa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru