Wednesday 14 August 2013

Walioachana na mihadarati watinga Ikulu


Na Mwandishi Wetu
RAIS Jakaya Kikwete ameiagiza Wizara  ya Afya kupitia kitengo cha magonjwa ya akili,  na Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya, kushirikiana na Kituo cha Ushauri Nasaha cha Pili Misana Foundation.
Alisema lengo ni kutaka kuona kituo hicho  kinawasaidia waathirika wengi zaidi wa dawa hizo.
Aliyasema hayo juzi Ikulu, Dar es Salaam, alipokutana na vijana walioachana na matumizi ya dawa za kulevya ambao wamepata ushauri nasaha na usaidizi kutoka katika kituo cha Pili Misana, kilichopo Kigamboni, Dar es Salaam.
“Jamii lazima ishiriki katika utatuzi wa jambo hili ni tatizo kubwa na linamgusa kila mtu na inabidi wote tushiriki katika kulipiga vita,” alisema Rais Kikwete.
Hata hivyo, alimpongeza Pili Misana na Zacharia Hans Pope, ambaye ndiye mfadhili wa kituo hicho ambacho tayari vijana 203 wamepatiwa huduma ya ushauri nasaha na wameachana na matumizi ya dawa za kulevya na kurudi katika shughuli za maendeleo.
Rais Kikwete, alisema tatizo la dawa za kulevya ni la muda mrefu, lakini awali lilikuwa halisikiki kwa sababu jitihada za kuzuia dawa hizo zilikuwa hazitangazwi wala kufuatiliwa.
Vijana 35 walioacha matumizi ya dawa hizo, walikwenda Ikulu wakiwa wametoka katika shughuli za kitaaluma, elimu na kijamii na wana umri tofauti kati ya miaka 14 mpaka 53.
Alisema serikali inafanya jitihada kubwa za kuwasaidia vijana mbalimbali na itaendelea kutoa msaada huo, huku juhudi za kupambana na dawa hizo zikiendelea.
Naye mfadhili wa kituo hicho, Zacharia Hans Pope, alitoa wito kwa jamii, kushiriki kwa kuwa karibu zaidi na vijana walioathirika ili kusaidia mapambano ya dawa hizo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru