Thursday 22 August 2013

LAAC yabaini upotevu wa 1.2bil/- Mvomero


Na Mohammed Issa
KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), imegundua upotevu wa sh. bilioni 1.2 katika Halmashauri ya Mvomero, mkoani Morogoro.
Kutokana na hilo, kamati imemuita aliyekuwa Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Sara Niluma, na aliyekuwa Mweka Hazina, Kabilile Stim, kufika mbele yake kueleza jinsi fedha hizo zilivyotumika.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, katika ofisi ndogo za Bunge, Dar es Salaam, Makamu Mwenyekiti wa LAAC, Seleman Zedi, alisema fedha hizo haijafahamika zimepelekwa wapi.
Kwa mujibu wa Zedi, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), alipofanya ukaguzi kwenye halmashauri hiyo, alibaini kiasi hicho cha fedha kilitumika bila kuonyeshwa zimetumikaje. Fedha hizo ni za mwaka 2011/2012.
Kutokana na upotevu wa fedha hizo, kamati imeamua kumuita Sara, ambaye amestaafu na Stim, ambaye ni Mweka Hazina wa Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam, ili waeleze fedha hizo zilikwenda wapi.
Zedi alisema wajumbe wa kamati wamebaini kuna matumizi ya fedha yasiyofaa katika halmashauri hiyo.
Alisema fedha zilizopelekwa kwa ajili ya kinamama na vijana zilitumika vibaya na kwamba, kamati inapiga marufuku fedha hizo kutumika kwa matumizi yasiyokusudiwa.
Makamu mwenyekiti alisema kamati inamtaka mkandarasi aliyekuwa akijenga ofisi ya mkurugenzi kurudisha fedha zilizozidi.
Alisema kamati inaiomba halmashauri kuongeza uwezo wa kujitegemea kwa asilimia 10.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru