Wednesday 21 August 2013

Watuhumiwa mauji ya Msuya kizimbani


NA MWANDISHI WETU, MOSHI
WATU watatu wamepandishwa kizimbani wakikabiliwa na shitaka la kumuua mfanyabiashara maarufu wa madini ya Tanzanite, Erasto Msuya (43).
Washitakiwa hao ni Sharifu Mohammed mkazi wa Kimandolu mkoani Arusha, Shaibu Mpungi, mkazi wa Kijiji cha Songambele na Musa Mangu mkazi wa Shagarai kwa Mrefu, mkoani Arusha.
Mohammed na wenzake walipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, mbele ya Hakimu Mkazi Munga Sabuni.
Wakili wa Serikali Stella Majaliwa, alidai kuwa washitakiwa hao walimuua Msuya kwa kukusudia.
Hata hivyo, washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza kesi hiyo.
Kwa upande wake wakili wa utetezi Lucie Paul, alidai mahakamani hapo kuwa wateja wake walikamatwa Agosti 12, mwaka huu, wamekaa rumande bila ya kupewa fursa ya kuwasiliana na ndugu zao au wakili, jambo ambalo si haki.
Msuya aliuawa Agosti 7, mwaka huu, saa 6.30 mchana, kwa kupigwa risasi kando ya barabara kuu ya Arusha – Moshi, katika eneo la Mjohoroni, wilayani Hai, karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
Kesi hiyo itatajwa Septemba 4, mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru