Thursday 22 August 2013

Kamati Kuu CCM kujadili ya Bukoba


Na Theodos Mgomba, Dodoma
KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, inaanza kikao leo mchana, mjini hapa, ambayo pamoja na mambo mengine itajadili suala la madiwani wanane wa Manispaa ya Bukoba, mkoani Kagera.

Kikao hicho kitafanyika chini ya  Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete. Kesho  Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), itaanza kikao cha siku mbili.
Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema hayo jana, alipozungumza na waandishi wa habari.
Alisema ajenda kubwa ya kikao hicho itakuwa kupitia maoni ya wana-CCM kuhusu Rasimu ya Katiba mpya na suala la madiwani wa Bukoba, ambao walivuliwa uanachama na Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kagera, ambapo Chama kimewataka waendelee na kazi.
Nape alisema awali, kamati ilitarajiwa kuanza kikao asubuhi, lakini kimeahirishwa hadi mchana kutokana na mwenyekiti wa Chama kuwa nje ya nchi.
“Ilikuwa tuanze asubuhi lakini mwenyekiti yuko Zimbabwe, katika sherehe za kuapishwa Rais Robert Mugabe, hivyo atakuja mchana ndipo tutaanza kikao,” alisema.
Alisema moja ya ajenda kubwa ni kupitia maoni ya wana-CCM kuhusu rasimu ya kwanza ya katiba, ambayo yalikusanywa kuanzia ngazi ya matawi na sasa yatapitiwa ngazi ya taifa.
Katibu huyo alisema baada ya maoni hayo kujadiliwa na Kamati Kuu, yatapelekwa NEC, ambayo itatengeneza taarifa itakayowasilishwa kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Tofauti yetu na wenzetu, sisi tumeshirikisha wanachama, wenzetu mmeona wanakwenda kwenye mikutano ya hadhara. Tunashukuru Jaji Warioba alisema hadharani kuwa hatapokea maoni ya mikutano ya hadhara, ambapo kwa kweli sheria ilitaka watu watumie mabaraza ya taasisi,” alisema.
Nape alisema kufanyika mikutano ya hadhara kunawapotezea wananchi muda na kuwahadaa Watanzania bila sababu.
Alisema CCM imeonyesha mfano wa jinsi ya kupata maoni kwa kushirikisha wanachama katika kujadili rasimu hiyo.
Nape alisema ajenda nyingine ni hali ya kisiasa nchini, na masuala ya utumishi, ambazo ni za kawaida ndani ya Chama.
Katika hatua nyingine, alisema CCM itazindua Baraza la Ushauri la Wazee wa Chama Jumapili wiki hii. Alisema baraza hilo litawashirikisha wenyeviti wote wastaafu wa CCM na makamu wao.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru