Thursday 22 August 2013

Trafiki bandia apanda kizimbani


NA SYLVIA SEBASTIAN, DSJ
MKAZI wa Kimara, Dar es Salaam, James Hassan, aliyekuwa akishikiliwa polisi, akituhumiwa kujifanya askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani, amepandishwa kizimbani kujibu mashitaka hayo.
Hassan (45), alipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, akikabiliwa na mashitaka mawili ya kujifanya mtumishi wa umma na kukutwa na sare za Jeshi la Polisi.
Wakili wa Serikali Nassoro Katuga, alimsomea mshitakiwa mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakamani hiyo, Joyce Minde.
Katuga alidai Agosti 14, mwaka huu, eneo la Kinyerezi, Mnara wa Voda, mshitakiwa kwa njia ya udanganyifu alijitambulisha kwa Inspekta wa Polisi Gabriel Chiguma, kuwa ni askari wa usalama barabarani.
Katika shitaka la pili, Hassan anadaiwa siku hiyo, kwa njia ya udanganyifu, alikutwa akiwa na sare za polisi, ambazo ni kofia, jaketi na mkanda.
Mshitakiwa alikana mashitaka, ambapo Katuga alidai upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa kwa kesi hiyo.
Hassan aliomba dhamana, ambapo Hakimu Joyce, alitaja masharti kuwa, awe na wadhamini wawili wenye makazi ya kudumu, watakaotia saini dhamana ya maandishi ya sh. milioni saba.
Mshitakiwa alishindwa kutimiza masharti hayo, hivyo alipelekwa rumande. Kesi itatajwa Septemba 5, mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru