Tuesday 20 August 2013

Dk. Sheni abadili muundo wa Baraza la Mawaziri



Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,  Dk. Ali Mohammed Sheni, amefanya marekebisho katika muundo na majukumu ya baadhi ya wizara za serikali yake.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee, ilisema kwa marekebisho hayo baadhi ya shughuli za wizara zimeunganishwa na kuundwa wizara mpya, na baadhi zimehamishiwa wizara nyingine.
Hata hivyo, taarifa hiyo ilieleza marekebisho hayo hayakuongeza idadi ya wizara ambapo serikali ya Zanzibar itaendelea kubaki na wizara 16.
Kutokana na marekebisho hayo, shughuli za Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ, zimeondolewa katika ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na kuundwa wizara mpya.
Shughuli za utawala bora zimeondolewa kutoka Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kuhamishiwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, huku shughuli za kazi zikiunganishwa na shughuli za utumishi na kuundwa wizara mpya.
Aidha shughuli za uwezeshaji wananchi kiuchumi na ushirika zimeondolewa kutoka Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika na kuunganishwa na shughuli za Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto.
Shughuli za Tume ya Mipango zimeondolewa kutoka Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo na kuhamishiwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, na Idara ya Uratibu wa shughuli za SMZ  Dar es Salaam, imeondolewa kutoka Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo na kuhamishiwa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais.
Wizara mpya zilizoundwa kufuatia marekebisho hayo ni Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ, Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma, Wizara ya Fedha, na Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto.
Kutokana na kuundwa kwa Wizara hizo mpya, Rais Dk. Sheni  amefanya mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri na Watendaji Wakuu wa Wizara kwa kuwabadilisha wizara baadhi ya mawaziri, makatibu wakuu na naibu makatibu wakuu.
Katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora anakuwa Dk. Mwinyihaji  Makame, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora anakuwa Salum Maulid Salum, na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora ni Said Abdulla Natepe.
Katika Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ anakuwa Haji Omar Kheri, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ ni Joseph Abdalla Meza, wakati Naibu Katibu Mkuu (Tawala za Mikoa) ni Mwinyiussi A. Hassan na Naibu Katibu Mkuu (Idara Maalum za SMZ) ni CDR Julius Nalimy Maziku.
Katika Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa umma ni Haroun Ali Suleiman na Katibu Mkuu  Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma ni Fatma Gharib Bilal, na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma, Yakout Hassan Yakout.
Katika wizara ya fedha, waziri ni Omar Yussuf Mzee, Katibu Mkuu ni Khamis Mussa Omar, na Naibu Katibu Mkuu ni Juma Ameir Khalid.
Katika Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto, Waziri ni Zainab Omar Mohammed, Katibu Mkuu wake ni Asha Ali Abdulla na Naibu Katibu Mkuu (Uwezeshaji na Ushirika) ni Ali Khamis Juma na Naibu Katibu Mkuu (Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto) ni Msham Abdulla Khamis.
Viongozi hao waliapishwa jana jioni Ikulu mjini Zanzibar katika hafla iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali.
00000

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru