Wednesday 21 August 2013

Waliojitoa NSSF walipwa mafao


NA MWANDISHI WETU
MFUKO wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), umelipa mafao yenye thamani ya sh. bilioni 199 kwa wanachama wake mwaka uliopita wa fedha.
Asilimia 70 ya fedha hizo, imeelezwa kuwa  zimelipwa kwa wanachama waliojitoa.
Pia, thamani ya NSSF imeendelea kupanda na kufikia trilioni 2.6 na pia, inawekeza sh.bilioni 950 kila mwaka.
Hayo yalisemwa na Meneja Kiongozi, Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa NSSF, Eunice Chiume, alipozungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) jana.
Alisema fedha hizo zimelipwa kwa ajili ya mafao mbalimbali kwa wanachama wake ikiwemo wanaojitoa kwa sababu mbali mbali ikiwemo kuacha kazi.
Alipoulizwa kuhusu watu kujitoa, alisema hali hiyo inatokana na uelewa duni juu ya hifadhi ya jamii kuhusiana na suala ambalo ni changamoto kubwa kwa taifa.
“Wengi hawana uelewa juu ya hifadhi ya jamii, mwanachama hata akiacha kazi eneo moja, anaweza kuendelea kuwa mwanachama na akahama na namba yake anapoajiriwa mahali pengine,” alisema.
Hata hivyo, alisema NSSF hakuna changamoto yoyote kwa lakini kwa taifa ni tatizo kubwa kwa sababu, wote wanajitoa ndio hao watakaokuja kuhitaji pensheni ya uzeeni, ambayo imeanza kuzungumzwa itolewe kwa wazee wote hata wasiojiwekea akiba.
“Yaani kitakachotokea ni kwamba, wanaojitoa sasa, wakizeeka itabidi kodi na michango ya wengine, itumike kuwalipa mafao, jambo ambalo ni mzigo mkubwa,”alisema.
Akizungumzia kuhusu uwekezaji, Eunice alisema NSSF kwa mwaka huu wa fedha, inatarajia kuwekeza sh. bilioni 951 .4.
Alisema sawa na ongezeko la asilimia 21 ikilinganishwa na mwaka uliopita wa fedha, ambapo iliwekeza sh. bilioni 751.4.
Kwa mujibu wa Eunice, NSSF imekuwa ikiwekeza kwenye miradi mikubwa hapa nchini na mingi ni ya serikali na urejeshaji wake ni wa uhakika.
Alitoa mfano wa ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), ambapo serikali imeshaanza kurejesha sh. bilioni 14 kwa mujibu wa mkataba wa mkopo wa bilioni 232.
NSSF kwa mwaka huu, inatarajia kukusanya sh. bilioni 181.1 kutoka kwenye vitega uchumi vyake na inatarajia kulipa sh. bilioni 5.19 kwa ajili ya mafao ya matibabu kwa wanachama wake.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru