Wednesday 14 August 2013

Waliojenga katikati ya makaburi wabomolewa


Na Frank Kibiki, Iringa
WATU waliovamia na kujenga nyumba katikati ya makaburi ya Mtwivila, Manispaa ya Iringa, wamebomolewa nyumba hizo.
Kazi hiyo ilifanywa jana na Halmashauri ya Manispaa hiyo, kwa madia kuwa nyumba hizo zimejengwa kinyume cha sheria.
Uhuru, lilishuhudia operesheni ya kubomoa nyumba hizo ambayo ilitekelezwa na askari mgambo wa Manispaa hiyo.
Meya wa Manispaa ya Iringa Amani Mwamwindi, alisema ni makosa kuvamia sehemu ya makaburi na kujenga nyumba, jambo ambalo kamwe hawataliacha liendelee.
“Ni kosa kujenga katikati ya makaburi, imebidi tuendeshe operesheni ya kubomoa nyumba hizi, kwa sababu hawa watu walivamia eneo hili la makaburi na kujenga nyumba zao tena bila woga wowote,” alisema Mwamwindi.
Akisimamia operesheni hiyo, Mwanasheria  wa Manispaa ya Iringa Innocent Kihaga,  alisema wamelazimika kuvunja nyumba hizo baada ya kubaini kuwaa zimejengwa maeneo ambayo si rasmi na bila kuwepo kibali cha mipango miji.
Hata hivyo, mwanasheria huyo alisema  wametoa muda wa siku 30 kwa mmiliki wa nyumba moja, ambayo tayari imekamilika, kubomoa na kuondoka eneo hilo.
Awali, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, Theresia Mahongo,  alisema manispaa haitakubali kuona watu wanajenga nyumba kiholela na kuwataka waheshimu sheria zilizopo.
Aliwataka wote waliojenga nyumba kwenye maeneo ambayo hawajaruhusiwa wabomowe kwa hiyari.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru