Thursday 1 August 2013

Mchumba wa Slaa alikoroga


NA FURAHA OMARY
JOSEPHINE Slaa Mushumbusi, mchumba wa Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, ametoa kioja mahakamani, alipokuwa akimtambua mshitakiwa.
Josephine alitoa kioja hicho jana, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alipokuwa akimtambua mshitakiwa katika kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha inayomuhusu akiwa mlalamikaji.
Mwanamama huyo aliyehojiwa na wakili iwapo anamtambua mshitakiwa, alikiri kumtambua lakini aliishia kumuonyesha mtu mwingine asiyehusika.
Wakili alimtaka kumtambua mshitakiwa aliyemvamia na kumpora mali zake, kwenye makutano ya SUMA JKT, katika Barabara ya Ali Hassan Mwinyi.
Josephine aliyefuatana mahakamani na Dk. Slaa, alipanda kwenye kizimba mbele ya Hakimu Mkazi Hellen Riwa, kutoa ushahidi. Washitakiwa katika kesi hiyo ni Getisi Mturi, Gake Mwita, Salum Mpanda na Charles Chasens.
Mturi na wenzake wanadaiwa Julai 13, 2011, katika eneo la SUMA JKT, walimvamia Josephine na kumpora vitu mbalimbali, na kabla ya uhalifu huo, walimtishia kwa bastola.
Akiongozwa na Wakili wa Serikali Leonard Chalo, kutoa ushahidi, Josephine alidai Julai 13, mwaka 2011, saa mbili asubuhi, aliingia ofisini kwake kwenye jengo la Mawasiliano Tower.
Josephine alidai alitoka ofisini  saa 11 jioni na kuanza safari ya kurejea nyumbani kwake Boko, akiendesha gari lenye namba ya usajili T 932 ASH, aina ya Toyota Harrier.
Alidai akiwa kwenye foleni eneo la tukio, aliona mtu akipita upande wa kushoto. Alidai kupitia kioo kidogo cha pembeni mwa gari lake, alimuona mtu huyo akivunja kioo cha gari lake.
“Nilimuona vizuri mtu huyo tangu alipotembea kwenda nyuma ya gari, ambako ghafla alianza kuvunja dirisha,” alidai.
Josephine alidai alitahamaki na kwamba, alisikia milio ya risasi,  hivyo alitafuta njia ya kujiokoa kwa kuondoa gari eneo hilo na kwenda kwenye geti, jirani na SUMA JKT.
“Nilikatisha barabara upande wa pili, ambako niligundua kuna mtu mwingine, nako kulikuwa na risasi zikilia.
“Kabla sijafika nilikotarajia kwenda, gari lilipinduka katikati ya mtaro, nilijaribu kufungua mlango ili nikimbie lakini nilikutana na mtu akiwa na bastola, hivyo sikufanikiwa kukimbia,” alidai.
Shahidi huyo alidai alimuona mtu huyo kwa sura, kwa kuwa walisimama wote kwa takriban dakika nane.
Wakili Chalo alimtaka Josephine kuangalia watu walioko mahakamani iwapo atamuona mtu huyo na kumtambua.  Sehemu hiyo ilikuwa ifuatavyo:
Josephine: Mheshimiwa naweza kumshika mkono iwapo nikimuona?
Hakimu: Ndiyo.
Josephine: Mheshimiwa naomba watu wote wasimame ili niweze kuwaona vizuri, kwani kipindi hicho nakumbuka alikuwa na uso mpana, lakini ni kama amebadilika, kwani hata mimi nilivyokuwa wakati huo si sawa na sasa.
Hakimu: Naomba wote msimame, isipokuwa mimi.
Watu wote waliokuwamo katika chumba cha mahakama walisimama, wakiwemo mawakili.
Josephine: Mheshimiwa huyu hapa, huku akimshika.
Aliyeguswa na Josephine alisogea mbele ya hakimu na kueleza kuwa, hahusiki na kesi hiyo, kwani yuko hapo akisubiri kudhaminiwa.
Mtuhumiwa: Mheshimiwa naomba tu nidhaminiwe, mimi sihusiki, wakati hayo yanatokea nilikuwa Malawi. Hili ni ‘gundu’. Mheshimiwa naomba nidhaminiwe kama barua moja haijahakikiwa, nidhaminiwe vivyo hivyo.
Kutokana na tukio hilo, waliokuwamo mahakamani waliangua vicheko, huku Josephine akisisitiza anakumbuka mtu huyo alikuwa sawa na huyo aliyekuwamo mahakamani.
Akiendelea na ushahidi, Josephine alidai anakumbuka waliomvamia walikuwa si chini ya sita na kwamba, walimwibia vitu mbalimbali, ikiwemo pochi, kamera, simu mbili, kadi za benki na leseni ya udereva. Alidai watuhumiwa waliondoka na pikipiki.
Alidai wakati wa tukio hilo alikuwa mjamzito, hivyo alikwenda hospitali ya Mwananyamala kuangalia afya yake.
Mwanamama huyo alidai kati ya saa sita au saba usiku wa siku ya tukio, alipigiwa simu na askari kutoka kituo cha polisi Chang’ombe na kutakuwa kwenda kufuata mali zake.
Alidai aliipata pochi, kadi za simu na leseni. Kesi hiyo itaendelea kusikilizwa Agosti 7, mwaka hu

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru