Friday 9 August 2013

Wataka Kiswahili kitumike kimataifa


WAJUMBE wa Baraza la Katiba  la Halmashauri ya Kibaha, wametaka lugha ya Kiswahili itumike katika mawasiliano rasmi ya kitaifa na kimataifa.
Wakichangia mjadala wa katiba mpya mjini Kibaha, pia walitaka Kiswahili kitumike kama lugha rasmi ya kufundishia kuanzia darasa la kwanza hadi vyuoni.
Akichangia katika sura ya kwanza, ibara ya nne ya rasimu hiyo, Selina Wilson, kutoka kata ya Maili Moja, hilo litawezesha kuharakisha maendeleo ya kiuchumi.
“Hakuna taifa lililopiga hatua kiuchumi kwa kutumia lugha za kigeni, inabidi Kiswahili kiwe lugha rasmi ya kufundishia na mawasiliano ya kitaifa na kimataifa.
“Vijana wa Kitanzania wamekuwa wakibuni teknolojia mbalimbali, lakini kutokana na matumizi ya Kingereza inabidi zipewe majina kwa lugha hiyo,” alisema.
Alisema ni wakati sasa katiba itamke wazi ili kuhakikisha Kiswahili kinachukua nafasi yake, kwani ni moja kati ya tunu za taifa.
Mjumbe mwingine, Issa Mkuwili, kutoka kata ya Mkuza, alisema Kiswahili kimeshaanza kutumiwa na mataifa mbalimbali lakini Watanzania wanarudi nyuma katika kukiendeleza.
Mwenyekiti wa kundi la sita la kukusanya maoni ya rasimu hiyo, Profesa Palamagamba Kabudi, alisema Kiswahili kinatumiwa kibiashara na kinawaingizia fedha nyingi wajanja kutoka Kenya na Uganda.
Alisema watu wa mataifa mengi duniani, yakiwemo ya Ulaya, wanapenda kujifunza Kiswahili na kinazungumzwa na mataifa mengi, hivyo kinaweza kutumika kimataifa.
“Unapokwenda nchi za Ulaya utakuta walimu wa Kiswahili wengi wanatoka Kenya, hata mabalozi wanapokuja nchini wanakwenda chuo kikuu kujifunza Kiswahili, utakuta mwongozaji wao ametoka Uganda,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru