Thursday 1 August 2013

Mashahidi kesi ya vigogo TBA kufikia 13


NA FURAHA OMARY
UPANDE wa Jamhuri katika kesi inayowakabili waliokuwa vigogo wawili wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), umeieleza mahakama kuwa unatarajia kuita mashahidi 13 na vielelezo 20, wakati wa usikilizwaji wa shauri hilo.
Washitakiwa katika kesi hiyo iliyopo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ambayo imepangwa kuanza kusikilizwa Agosti 7, mwaka huu, ni  waliokuwa Mkurugenzi Mkuu wa Wakala huo, Makumba Kimweri na Msanifu Mkuu wake, Richard Maliyaga.
Kimweri na Maliyaga wanakabiliwa na mashitaka matano ya matumizi mabaya ya ofisi katika utoaji kibali cha ujenzi wa jengo la ghorofa 15 kiwanja namba 45 mtaa wa Chimara.
Mwendesha Mashitaka kutoka Taasisi ya  Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Leonard Swai, alidai hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Sundi Fimbo, baada ya kuwasomea washitakiwa maelezo ya awali.
Akiwasomea maelezo ya awali, Swai alidai Kimweri alikuwa na wadhifa huo TBA kuanzia mwaka 2002 hadi 2010 na Maliyaga aliajiriwa mwaka 2002 akiwa msanifu mkuu.
Alidai kiwanja hicho kilikuwa kinamilikiwa na TBA, ambapo hadi mwaka 2006 kilikuwa hakijaendelezwa ambapo wakala huo chini ya Sheria ya Ununuzi wa Umma iliwaalika wanaotaka kuwekeza kuwasilisha andiko la awali kwa ajili ya kuendelezaji.
Swai alidai kampuni nane ziliwasilisha maandiko ya awali ambazo zilifunguliwa katika hafla ya ufunguzi iliyofanyika Februari 19, 2006. Alidai Bodi ya Zabuni ilikutana katika mwaka wa fedha 2006/2007 kikao kilichofanyika Septemba 29, 2006 ilipendekeza wawekezaji saba ikiwemo Royale Orchard Inn Ltd.
Ilidaiwa Februari, 2007 timu ya tathmini ilikaa na kufanya tathmini kuhusu viwanja vinane kwa ajili ya kuviendeeleza ambavyo ni vya TBA, vikiwemo namba 45 na 46.
Mwendesha mashitaka huyo alidai katika ripoti hiyo walitoa mapendekezo kuhusu kampuni saba kuwasilisha taarifa zake kwa kuwa miongoni mwa kampuni za awali zilizopita ikiwemo Royale.
Alidai timu ilipitia tena na kutoa mapendekezo na kuwapitisha Royale na M/s Msasani Slipway Ltd. Ilidaiwa Kaimu Katibu wa Bodi ya Zabuni D. M. Makolo alielekeza ziliamuriwe kampuni mbili kuendelea kutoa taarifa zao na kuwasilisha mbele ya Menejimenti ya TBA na timu ya makubaliano.
Swai alidai Machi 22, 2007, Makolo aliandika barua kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu kumwita mkurugenzi mtendaji wa kampuni zilizoshinda kwa makubaliano.
Alidai Agosti 6, mwaka 2007, mikataba miwili kwa ajili ya viwanja viwili wahusuika walitia saini ambapo kwa upande wa serikali watamiliki asilimia 25 na mwekezaji asilimia 75 katika jengo la ghorofa 18. Alidai TBA ilitoa vibali vilivyotiwa saini na Maliyaga, kikiwemo za kuongeza kutoka ghorofa 15 hadi 18.
Mwendesha mashitaka huyo alidai eneo hilo lilikuwa ni kwa ajili ya ujenzi wa ghorofa tatu hadi sita na kwa makazi, na kwamba washitakiwa walitoa kibali kwa mwekezaji bila ya kupata idhini kutoka kwa mamlaka husika.
Washitakiwa hao walikubali majina yao, vyeo na kutia saini hati za kuruhusu kujenga wakati mengine yote walikataa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru