Tuesday 25 June 2013

Kapombe huyooo Uholanzi


Kapombe huyooo Uholanzi

NA SOPHIA ASHERY
BEKI wa Simba Shomari Kapombe, anatarajia kwenda Uholanzi kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa katika klabu ya FC Twente.
Klabu hiyo yenye maskani katika mji wa Enschede nchini humo, inashiriki ligi kuu ya nchi hiyo maarufu kama Eredivisie na ilianzishwa mwaka 1926.
Katibu Mkuu wa Simba Evodius Mtawala, alisema kwamba, FC Twente iliandika barua kumtaka Kapombe kwenda kufanya majaribio, akifuzu watampa mkataba.
Mtawala alisema, uongozi wa Simba umekubali na beki huyo atakwenda Uholanzi baada ya taratibu za safari kukamilika.
Alisema, Simba ingependa kuona Kapombe anafanikiwa na kusajiliwa kucheza soka Uholanzi.
Alisema, hilo likifanikiwa, itakuwa faraja kwa Simba kupeleka mchezaji kucheza soka ya kulipwa nje ya nchi.
Kapombe aliyezaliwa Januari 28, mwaka 1992, aliibukia timu ya Polisi Morogoro kabla ya kujiunga na Simba miaka mitatu iliyopita ambako anatarajiwa kumalizia mkataba wake Desemba mwaka huu.
Tovuti ya FC Twente imeripoti kuwa, Kapombe atatua Uholanzi wakati wowote kuanza majaribio hayo.
 Taarifa zaidi zinaeleza kuwa, klabu hiyo imefurahishwa na Simba kumruhusu beki huyo kufanya majaribio.
Kapombe akifuzu, atakuwa mchezaji wa kwanza kutoka ukanda wa Afrika mashariki ndani ya kikosi hicho cha FC Twente.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru