Friday 28 June 2013

Smart partnership kuinua sekta ya utalii

Na Mwandishi Wetu
 NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu, amesema majadiliano ya pamoja kwa manufaa wa yote ‘smart partnership dialogue’ yatasaidia kuinua sekta ya utalii nchini.
Pia, alisema mkutano huo utasaidia kubadilisha mtazamo wa jamii katika sekta ya utalii na maliasili pamoja na kuanza utafutaji wa masoko ya utalii kiteknolojia.
Nyalandu aliyasema hayo jana muda mfupi baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza kutembelea mabanda ya maonyesho ya mkutano huo. Mkutano huo utadumu kwa siku tatu na ulianza jana.
Alisema majadiliano haya ni muhimu kwani yanashirikisha watu wengi ambao watakuwa dira ya kubadilisha fikra na mtazamo wa sekta ya utalii na kuwezesha utafutaji wa masoko kiteknolojia.
“Kukua kwa teknolojia ni jambo la muhimu na kila nchi iliyoendelea na kupiga hatua ipo juu kiteknolojia, hivyo, naamini majadiliano haya ni chachu ya kupiga hatua zaidi,’’ alisema.
Nyalandu aliwataka Watanzania waliobahatika kushiriki katika majadiliano hayo, kuwa mabalozi wazuri kwa wenzao kwa kuwa wamepata fursa muhimu.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri huyo alisema serikali imeanza kupiga hatua kubwa katika sekta ya utalii kwa kuutangaza kimataifa.
Awali tulikuwa tunaielezea sekta ya utalii kupitia makabrasha au vipeperushi, lakini sasa tumeingia katika mitandao, haya ni mafanikio, ninatumaini mkutano huu utatupa watalii zaidi,’’ alisema Nyalandu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru