Wednesday 21 August 2013

Kituo cha Ubungo ‘kuzaa’ viwili


NA SELINA WILSON
HALMASHAURI ya Jiji la Dar es Salaam inatarajia kujenga vituo viwili vya mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani, inayokadiriwa kugharimu sh. bilioni 40.
Ujenzi wa vituo hivyo, unafuatia kubadilishwa kwa matumizi ya Kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo, ambacho kinafanyiwa ukarabati kwa ajili ya mabasi yaendayo haraka.
Msemaji wa Jiji Gaston Makwembe, alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) mjini Dar es Salaam.
Makwembe, alisema vituo hivyo vitajengwa katika maeneo ya Mbezi Luis na Boko Basihaya, ambapo vitatoa huduma kwa kanda.
Alisema kituo cha Boko Basihaya, kitahuduma wasafiri wanaokwenda mikoa ya kanda ya Kaskazini na cha Mbezi Luis kitahudumia wasafiri wanaoelekea mikoa ya kanda ya Kati, Nyanda za juu.
Kwa upande wa abiria wanaokwenda mikoa ya Kusini watajengewa kituo cha mabasi katika eneo la Kongowe baada ya kukamilishwa kwa awamu ya kwanza ya vituo vya Mbezi Luis na Boko Basihaya.
Alisema kwa sasa wapo katika mchakato wa kufanya upembuzi yakinifu kwa lengo la kupata gharama halizi za utekelezaji wake  na kubaini vyanzo vya fedha.
Makwembe, alisema Halmashauri ya Jiji imepanga kushirikiana na taasisi mbalimbali za fedha na wawekezaji wanao onyesha nia ya kushirikiana katika ujenzi wa vituo hivyo.
Kwa upande wake Meneja wa Kituo Kikuu cha Mabasi Ubungo, Juma Idd, alisema wakati wa maandalizi ya ujenzi wa vituo hivyo, kituo hicho bado kitaendelea kutoa huduma kwa wasafiri wa mikoani na nchi jirani.
Akizungumzia ukarabati wa kituo hicho kwa ajili ya kuhudumia mabasi yaendayo haraka, Iddi alisema eneo hilo pia litajengwa maduka makubwa na hoteli.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru