Friday 9 August 2013

Mhadhiri UDSM auawa kwa risasi



NA KHADIJA MUSSA
MHADHIRI Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Shule ya Uhandisi, Patrick Rweyongeza, ameuawa kwa kupigwa risasi na majambazi.
Tukio hilo ni mfululizo wa matukio ya ujambazi wa kutumia pikipiki, maarufu bodaboda, ambayo yameanza kushika kasi jijini Dar es Salaam.
Rweyongeza aliuawa juzi, saa tano asubuhi, eneo la Magomeni TANESCO, alipokuwa akitoka benki. Inadaiwa majambazi hayo yalipora sh. milioni 5.5.
Mhadhiri huyo inaelezwa alikuwa ndani ya gari na alikuwa anakwenda eneo lake la ujenzi.
Kwa mujibu wa taarifa, majambazi hayo yalimfuata yakiwa kwenye pikipiki na kumfyatulia risasi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alithibitisha tukio hilo na kuongeza kuwa, uchunguzi unaendelea.
Kwa upande wake, Mhadhiri wa chuo hicho, Dk. Mohamed Bakary, ameviomba vyombo vya usalama kufanya uchunguzi wa kina ili kuwabaini waliohusika katika tukio hilo.
Rweyongeza aliajiriwa UDSM Machi, 2008. Masomo yake ya chuo kikuu aliyapata chuoni hapo alikojiunga 2002 na kuhitimu Shahada ya Kwanza ya Uhandisi Majengo mwaka 2007.
Mwaka 2010 Rweyongeza alijiunga na Chuo Kikuu cha Glasgow, nchini Scotland, ambako mwaka 2011 alihitimu Shahada ya Uzamili ya Uhandisi Majengo na Mitambo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru