Wednesday 14 August 2013

Polisi wanasa shehena ya bangi


 NA LILIAN JOEL, ARUSHA

POLISI Mkoani hapa wamekamata shehena ya maguni 352 ya bangi yaliyokuwa yakisafirishwa kwa ajili ya kuingia katika soko la ndani na nje ya nchi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Lebaratus Sabas, aliwaambia waandishi wa habari Jijini Arusha jana kuwa, shehena hiyo ilikamatwa baada ya Polisi kupata taarifa kutoka kwa raia wema.
Kamanda Sabas, alisema katika tukio hilo, watu watano wanawashikiliwa kwa kosa la kukutwa wakiisafirisha.
Aliwataja watuhumiwa kuwa ni Thomas Lesime (60), Esuphat Daudi, Atumii Daud, Lemali Saitoti na Lomayan Thomas, wote wakazi wa Kijiji cha Kisimiri Juu, wilayani Arumeru.
Hata hivyo, alisema tayari wameshateketeza magunia 225 na magunia 127 yameachwa kwa ajili ya kutumika kama kielelezo mahakamani.
Wilaya ya Arumeru ni miongoni mwa wilaya maarufu nchini kwa kilimo cha bangi, huku Kijiji cha Kisimiri Juu kikiongoza.
Kilimo cha zao hilo kimeendelea kushika kasi kutokana na kipato kizuri na cha uhakika wanachopata wahusika wa biashara hiyo haramu.
Imeelezwa kuwa kilimo hicho huendeshwa chini ya ufadhili wa wafanyabiashara wakubwa wakiwemo kutoka nje ya nchi.
Wafanyabiashara hao, hulipia gharama za kutunza shamba na uvunaji kama njia ya kuwahamasisha wakulima kuendelea na kilimo hicho haramu.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru