Thursday 1 August 2013

Mahakama yamuachia Murji


NA MWANDISHI WETU
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mtwara, jana ilimfutia mashitaka Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini (CCM), Hasnein Murji, aliyeshitakiwa kwa uchochezi.
Kufutiwa mashitaka kwa Murji kunatokana na Hakimu Mkazi Dyness Lyimo, kukubaliana na hoja za Wakili wa Murji, Peter Kibatala, kwamba mashitaka dhidi ya mteja wake hayana mashiko kisheria na kwamba, hati ya mashitaka haielezi kosa.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Dyness, alisema anakubaliana na hoja za utetezi kwamba hati ya mashitaka ina upungufu.
“Nakubaliana na hoja za upande wa utetezi. Kweli hati ya mashitaka ina upungufu, hivyo naitupilia mbali na mshitakiwa yuko huru,” alisema Hakimu Dyness.
Akiwasilisha hoja za kupinga hati ya mashitaka, Wakili Kibatala, alidai kwa mujibu wa kifungu cha 129 na 132 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, vinaelezea mahakama kuikataa hati ya mashitaka yenye upungufu na vinampa Mwendesha Mashitaka jukumu la kuhakikisha hati ya mashitaka inakuwa kamili.
Kutokana na hilo, Kibatala aliomba hati ya mashitaka itupwe kwa kuwa ina upungufu.
Murji alikuwa akikabiliwa na kosa la uchochezi, ambapo anadaiwa kutenda kosa hilo, Januari 19, mwaka huu, eneo la Ligula mkoani Mtwara.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru