Wednesday 14 August 2013

Tume yatoa ukomo wa muda wa maoni


NA MWANDISHI WETU
TUME ya Mabadiliko ya Katiba, imezitaka asasi, taasisi na makundi ya watu wenye malengo yanayofana, kuwasilisha maoni yao kabla ya muda wa mwisho uliowekwa.
Makundi hayo ni yale yaliyounda Mabaraza ya Katiba kwa wanachama wake kwa ajili ya kuijadili na kuitolea maoni Rasimu ya kwanza ya Katiba Mpya iliyotolewa na Tume.
Kwa mujibu wa Tume hiyo, mwisho wa kuwasilisha maoni ni Agosti 31, mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa jana kwa Vyombo vya habari na Katibu wa Tume hiyo, Assaa Rashid, ilisema ukomo wa tarehe ya kuwasilisha maoni kwa mujibu wa mwongozo wa Uundaji wa Mabaraza ya Katiba ya asasi, taasisi na makundi ya watu wenye malengo yanayofanana ulianza kutumika Juni Mosi, mwaka huu.
Assaa, alisema Tume haitaongeza muda wa kupokea maoni kwa makundi hayo kwa kuwa baada ya tarehe iliyotajwa, Tume itakuwa na kazi ya kuyapitia na kuyachambua maoni hayo kwa ajili ya kuiboresha Rasimu.
Katibu huyo alizitaka kuwasilisha maoni yao moja kwa moja katika ofisi za Tume zilizopo Jijini Dar es Salaam, Mtaa wa Ohio au ofisi ndogo ya Zanzibar, Mtaa wa Kikwajuni Gofu, katika Jengo la Mfuko wa Barabara.
“Kwa mujibu wa Aya Na. 4.0 ya Mwongozo, Asasi, Taasisi na Makundi ya watu wenye Malengo yanayofanana, yanatakiwa kuwasilisha kwa Tume maoni hayo kwa njia ya randama, barua, andiko au muhtasari wa makubaliano,” alisema Assaa.
Aidha, alisema wanaweza kutuma kwa njia ya barua pepe; katibu@katiba.go.tz au anuani za posta za Tume ya Mabadiliko ya Katiba, S.L.P 1681 Dar es Salaam pamoja na ile ya S.L.P 2775 Zanzibar.
Hata hivyo, aliyataka makundi hayo kuzingatia tarehe ya mwisho ya kuwasilisha maoni iliyopangwa naTume.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru