Thursday 22 August 2013

Kikwete: Mazingira ya uwekezaji kuboreshwa


NA MWANDISHI WETU
RAIS Jakaya Kikwete, amesema serikali itaendelea kuboresha na kuimarisha mazingira ya kufanyia biashara ili kutoa fursa kwa wawekezaji kuendesha shughuli zao kwa ufanisi.
Alisema hayo wiki hii, mjini Dar es Salaam, katika hafla maalumu ya kukabidhi tunzo kutambua mchango wa taasisi zinazohusika na shughuli za uchimbaji madini na nishati nchini.
Rais Kikwete alisema kwa muda mrefu kumekuwepo na manung’uniko kutoka kwa baadhi ya watu wanaodai rasilimali za taifa kutosaidia maendeleo ya nchi, lakini serikali imejitahidi kufanyia kazi eneo hilo na kuleta mabadiliko.
Alisema moja ya hatua zilizochukuliwa na serikali kuboresha mazingira ya uwekezaji ni kusimamia amani na ustawi wa nchi, unaotoa fursa kwa wawekezaji kuendesha shughuli zao kwa mafanikio.
Kuhusu tunzo hizo, alisema zimebuniwa maalumu kwa ajili ya kuzihamasisha kampuni zinazohusika na sekta hizo kuongeza ushiriki katika maendeleo ya jamii.
Kwa upande wake, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kampuni za uchimbaji madini na zile za nishati zimeongeza ushiriki katika maendeleo ya huduma mbalimbali za kijamii.
Profesa Muhongo alisema tunzo hizo zilizohusisha vyeti na ngao maalumu ni kielelezo cha ushiriki wa kampuni hizo katika maendeleo ya jamii kupitia miradi ya miundombinu, kuchangia huduma za afya, elimu, maji, ajira na uwezeshaji.
Awali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, alisema kampuni 14 zilihusishwa kwenye mchakato wa kuwapata washindi, ambao ni kampuni zinazojitoa zaidi kwenye huduma mbalimbali za kijamii.
Maswi alisema baada ya tunzo hizo kuzinduliwa na Rais Kikwete mwaka jana, liliundwa jopo la majaji saba waliozunguka kwenye maeneo mbalimbali na hatimaye kuwapata washindi.
Washindi wa jumla wa kwa kampuni zenye mtaji mkubwa ni mgodi wa almasi wa Williamsons na migodi ya dhahabu ya Geita (GGM) na Bulyanhulu.
Kwa upande wa kampuni zenye mtaji wa kati, washindi wa jumla ni Kiwanda cha Saruji Mbeya, Tanzanite One na Kiwanda cha Saruji cha Twiga.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru